Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja iliyopo mezani ya Kamati ya Nishati na Madini. Yako masuala mengi mengine tutayajibu kwa maandishi na sitaweza kuyafikia yote lakini nitachangia kwenye masuala mawili matatu. La kwanza ni bei ya mafuta ambayo nadhani wote tunafahamu mwenendo wa bei ya mafuta duniani, ukitazama ile shepu ya curve ya bei kuanzia mwaka 2014 ambapo bei ya sasa ya mafuta iko juu kama iliyokuwa 2014. Kwa hiyo, unapata bakuli kwamba 2014 ilikuwa inashuka halafu inashuka ikaanza kupanda mwaka 2021 mpaka sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna dhana kwamba Mheshimiwa Rais ameingia mama Samia bei ya mafuta imepanda kila kitu kimepanda lakini kazi kubwa imefanyika, ya kuondoa tozo mbalimbali kuhakikisha kwamba wananchi wanapata nafuu ya bei ya mafuta. Sasa bei ya mafuta asilimia zaidi ya 50 inachangiwa na bei ya mafuta duniani asilimia 39 ni kodi na tozo mbalimbali hapa nchini. Kwa hiyo, yale mengineyo ya miundombinu ni kama asilimia 10 asilimia 11 ukitazama, ukiondoa tu kodi zile za TRA mapato ambayo yapo Ring-fenced kwenye mafuta ni shilingi 513. Tuna shilingi 263 ya Mfuko wa Barabara tuna shilingi 100 ya TARURA, tuna shilingi 100 ya REA, tuna shilingi tano ya maji jumla ni shilingi 513. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiamua kuzitoa zote hizo mafuta tunaweza kununua kwa shilingi 1,800/=, lakini tunanunua shilingi 3,000, shilingi 2,300 kwa sababu kuna hizo na zile kodi nyingine. Kwa hiyo, kupanga ni kuchagua tunataka bei ya chini ya mafuta maana yake either tuondoe kwenye maji, tuondoe kwenye REA, tuondoe kwenye TARURA au tuondoe kwenye Mfuko wa Barabara. Sasa, huo ndio uhalisia Serikali imechukua na itaendelea kuchukua hatua mbalimbali, za kupunguza makali kwenye bei na tumefanya tumetoa fedha nyingi. Kwa sababu, kama sio hatua za Serikali leo bei ya mafuta watu wangekuwa, wananunua hata shilingi 2,600 lakini tumezishusha kupunguza makali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kufanya hivyo lakini mazingira ya dunia mnayajua moja ya nchi kubwa zinazozalisha mafuta kwa wingi Duniani, ni Urusi na sasa hivi kuna shamrashamra ya vita kule na leo pipa limeenda dola 90 na kama vita ikitokea itafika dola 100. Kwa hiyo, ni vizuri tukawaeleza wananchi uhalisia kwa sababu tunaweza tukaja hapa, tukasema Serikali haijafanya kitu kupunguza ifanye zaidi lakini uhalisia ndio huo. Tutaendelea kuchukua hatua bila shaka na siajabu tukachukua maamuzi magumu kuhakikisha kwamba, bei kubwa ya mafuta haiathiri shughuli za uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Suala la miundombinu limezungumzwa kwamba miaka yote limekuwa linazungumzwa na halifanyiwi kazi ni kweli. Kuna meli hapa zinakuja zinachukua siku mpaka 19 hazijashusha nyingine mpaka zinaondoka na sio tu za mafuta ,hata meli nyingine zinakaa pale kwenye outer and carriage mpaka siku za kwenda mahali pengine zinaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niwape habari njema kwamba kabla ya mwisho wa mwezi huu tutasaini IMU na makampuni makubwa mawili ya kuweza kufumua miundombinu yote ya uingizaji/ushusha na uingizaji wa mafuta. Tunakwenda kuibadilisha TIPPER na kuweka uwekezaji mkubwa ambao utaongeza uwezo mara tatu kwa TIPPER. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi meli ikija ya mafuta ya dizeli inashusha kwenye kituo kinaitwa SPM ambalo bomba lake ni jembamba kwa hiyo, meli ina pressure kubwa bomba jembamba na hatuwezi kufuta kushusha mafuta Dar es Salaam mpaka twende Tanga ambapo bandari ni ndogo. Kwa hiyo, tumeamua tutaweka mabomba makubwa zaidi na sio dizeli peke yake tutaboresha matanki na tutabadilisha. Hiyo kazi itachukua kama miaka mitatu lakini itabadilisha kabisa mfumo mzima wa ushushaji wa mafuta hapa nchini. Hilo ni jambo liko tayari tumelifanyia kazi katika kipindi cha miezi hii michache iliyopita kwa siku zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kilio kile kwamba miaka yote linazungumzwa halifanyiki basi safari hii, linafanyika sawasawa kutokana na uongozi wa Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, nilizungumza ya mafuta amezungumza vizuri sana Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya hapa kwa siku sekta yetu ya mafuta sisi inachangia shilingi bilioni 5.1 kwenye shughuli za maendeleo. Kwa mwaka shilingi 1.8 trillion ni sekta ambayo ni very sensitive ni sekta ambayo lazima tuilee na kuikuza vizuri sasa la mafuta hilo limeisha hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni la kukatikakatika kwa umeme limezungumzwa sana na niseme tu kwamba na Wabunge baadhi wamezungumza vizuri sana hapa na lina dimensions nyingi; na nimesikia Mbunge hapa mmoja akisema watu mnatudanganya na nini. Hakuna mtu kwenye Wizara/TANESCO anapenda umeme ukatike na hakuna mtu anafanya makusudi kukata umeme in fact, watu wetu wa TANESCO sasa hivi hata saa 8 usiku ukipiga simu mahali umeme umekatika wako field wanajaribu kurudisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto iliyopo ni changamoto ya legacy ya muda mrefu kimataifa inabidi utenge asilimia 10 mpaka asilimia 12 ya pato ghafi la kampuni (utility) kwa ajili ya (R&M) Repair and Maintenance. TANESCO mwaka jana imepata mapato ya 1.8 trillion shillings maana yake Repair and Maintenance ilipaswa kuwa shilingi bilioni 180 mwaka juzi imepata Shilingi 1.7 trillion, Repair and Maintenance ilipaswa kuwa shilingi bilioni 170 na hivyo na hivyo na hivyo. Sasa uliza ngapi zimetengwa for the past ten years sasa hauwezi, kutotenga na hao walioweka hizi standards ni wanasayansi na kote duniani wanafanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sasa utakuja utalaumu Waziri kaja umeme unakatika lakini we have to do the necessary things ili turekebishe. Hapa nataka niwaambie kuna line za ugavi za usambazaji wa umeme ambazo nyingi ni 33KV na 11KV, ndio 33KV unasambaza umeme mitaani na standard ni kilomita 100 kwa 33KV umeme. Sasa kuna line inatoka Dodoma inakwenda Kongwa inakwenda Mpwapwa inakwenda Gairo inakwenda Kiteto ya 33KV kilomita 1,600 wakati inapaswa kufanya kilomita 100. Kuna line ya 11KV inapaswa kupeleka umeme kule Chanika kilomita 30 lakini inapeleka umeme 206.

Mheshimiwa Mwenyekiti, line inakwenda Lindi kutoka Mkuranga pale ni ya kusambaza umeme mitaani 33KV sasa umeme Lindi unategemea utakuwaje, watu wanajenga wanaanzisha biashara wanaanzisha viwanda lazima kutakuwa unstable na hii yote amezungumza Mheshimiwa Gulamali kule Igunga ni nchi nzima. Sasa, sisi tumeyakuta hayo lazima tufanye kwa hiyo tume-design mradi mkubwa wa dollar bilioni 1.9 wa ku-upgrade sub-stations na hizi lines zote ambazo zinazungumzwa kuhakikisha kwamba umeme kwenye gridi upo stable. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Wabunge mtu- support sub-stations kwa mfano, nchi nzima kuna distribution sub-stations 67 tu wakati kimuundo TANESCO ina Wilaya 132 lakini una sub-stations 67 na kati ya hizo 39 ziko Dar es Salaam sasa unategemea stability ya umeme itapatikana vipi wakati, hauna sub-stations nchini na katika hiyo sub-stations uliza ambazo zimechakaa ni majority. Tumetafuta fedha tumetenga kwanza ku-refurbish sub-stations 19 na kujenga nyingine mpya 59. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeyakuta matatizo na tunayashughulikia kwa uhakika hapa juzi kulikuwa na habari ya mgao umekwenda umetokea kutokana na kule visimani tumesimamisha kufanya mgao pale Ubungo kwa Mheshimiwa hapa kaka yangu. Zile wire za sub-stations zile ziko wazi haziko insulated ukitokea upepo zikigusana tu Ubungo sub-station inachomoka. Ikichomoka Ubungo sub-station half of Dar es Salaam haina umeme na kingine ni kuzivalisha tu juzi tumefanya hiyo kazi nchi nzima tumezivalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vikombe vina-cracks ikinyesha mvua vina-conduct umeme unakatika. Sasa hatutaki kusema haya maneno sana sisi tunaomba mtupe muda Mheshimiwa Waziri aliyepita kaka yangu Kalemani alikuwa na miaka minne kwenye … (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri nitakuongezea dakika tatu ili uweze kuhitimisha hoja yako.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante alikuwa na miaka minne kwenye nafasi hii na amefanya kazi nzuri mimi nina miezi minne tuombe uhai, nina imani na Rais na mimi nipate miaka minne halafu tuone kama tutakuja kuzungumza haya mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais aliyepita marehemu mpendwa wetu alikuwa na miaka sita kwenye nafasi hii mama Samia ana mwaka mmoja na yeye, tuombe uhai apate miaka sita halafu tuone kama tutakuja kuzungumza matatizo kama haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuvumiliane tupeane muda maneno ya kushambuliana binafsi yanasikitisha kwamba Waziri kapanda helicopter kaweka hivi na nini hii sio sifa ya Mbunge. Hatuko hapa kutupiana mawe hii ni meli yetu wote nikifeli mimi imefeli nchi akifeli Rais imefeli nchi. Kama una matatizo ya Mheshimiwa Samia Suluhu kuwa Rais au mimi kuwa Waziri tutafute jambo lingine sio mambo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni Julius Nyerere nimebakia dakika mbili katika ulizonipa. Julius Nyerere nilivyoripoti kwenye ofisi hii status ya kwanza kuomba ni ya mradi kwa wataalam nao wakanipa taarifa kwamba mradi mpaka leo umechelewa kwa siku 477. Nikawaambia mbona mtaani mimi nilikuwa sijui Wabunge/wananchi wanajua? Wakasema hatujawaambia kazi yangu ya kwanza ilikuwa kwenda kwenye Kamati na kuwaambia ukweli kwamba kwa mujibu wa wataalam mradi umechelewa na sababu ni hizi. Kwa sababu, huu mradi sio wa kwangu binafsi ni mradi wa nchi na ninapowaeleza Wabunge na Kamati nataka tusaidiane namna ya kutoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo linatupwa kama zigo la Waziri in fact katika hizi changamoto tulizozisema, zimetokana na sisi kubadilisha mfumo wa usimamizi wa mradi ule. Leo hii mkandarasi yule anasimamiwa kwa ukaribu kuliko ambavyo amewahi kusimamiwa siku zote sisi jukumu letu ni kuhakikisha kwamba, mradi huu unakwisha ukiwa salama na ukiwa imara na hicho ndicho tutakachofanya na hicho ndicho tunachoendelea nacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mengine ya REA tutaendelea nilivyozungumza naomba kauli yangu niliyoitoa hapo nyuma kwamba tunakwenda kwenye vitongoji. Tumeyapokea maoni ya Wabunge kuhusu hii classification ya miji na vijiji tutakwenda kuifanyia kazi vizuri tuje tutoe tamko sahihi, tutakuja na mpango wa kupeleka umeme kwenye vitongoji. Kuna fedha nyingi tumepata karibu shilingi bilioni 400 ambazo zitatupeleka kilomita mbili mbili sasa, kwa Kijiji kuliko kilomita moja moja kama kwenye REA II round III. La mwisho kabisa… (Makofi)

MWEYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe hoja moja ya mwisho. Hapa ninayo taarifa ya TRA ya mapato ya quarter ya nne ya 2020 na quarter ya nne ya 2021. Ukiangalia mapato ya TRA kwa Novemba 2020/2021 ilikuwa ni shilingi trilioni 1.3, Novemba mwaka huu ni shilingi trilioni 1.7 imeongezeka. Ukiangalia mapato ya mwaka juzi Disemba yalikuwa shilingi trilioni 20.0 mwaka huu ni shilingi trilioni 2.4 sehemu kubwa ya mapato inalipwa na watu wanaozalisha shughuli za viwandani. Ukiangalia growth ya quarter ya mwaka jana ya mwisho na growth ya quarter ya mwaka huu wa mwisho kuna ongezeko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna hii steria kwamba hali imedondoka uchumi umeharibika nenda kwenye takwimu za mapato na hawa ni watu wa viwandani. Sisi tumefanya hivyo kwa sababu tunajua kwamba katika changamoto hii lazima uwapelekee umeme pia watu wa viwandani na watu wa mitaani. Huku pia na wenyewe wapunjike wakati wengine wa mitaani wanapata wa viwandani wanakosa ndivyo inavyokwenda. Tungeweza kabisa kuwaambia watu wenye viwanda vitatu funga viwanda funga mdomo umeme, tupeleke mitaani watu wafurahi lakini haya mapato ya kodi yasingepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumeamua kufanya hivyo kwa maslahi ya nchi vile vile lakini tunajua jukumu letu kubwa, ni kuongeza uzalishaji wa umeme kuimarisha miundombinu ya usafirishaji na usambazaji. Kazi hiyo tutaifanya tunaiweza tunayo maarifa tuna-management nzuri ya TANESCO tuna bodi nzuri ya TANESCO; na ninataka nilihakikishie Bunge hili na watanzania kwamba watupe muda watupime kwa matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)