Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami nipongeze kwa kazi nzuri inayofanywa na Serikali kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika kwenye sekta ya elimu na afya. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, ametembelea Mkoa wetu wa Manyara hasa Wilaya yetu ya Hanang, amehimiza wananchi na wananchi wamechangamka, wameelewa Serikali yao inachapa kazi kweli kweli na kazi inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie eneo la usambazaji wa dawa ambayo inafanywa na MSD. Kweli kuna changamoto kubwa kwenye maeneo na vituo vyetu vya afya kuna uhaba mkubwa wa dawa. Ninachoshauri, Serikali iangalie namna ya muundo mzima wa MSD. Tukiiacha MSD kwenye utaratibu huu wa kawaida wakati, wengine mtu akiamka anaweza akanunua akapelekwa kwenye maduka, lakini MSD inapita kwenye mchakato wa manunuzi. Tuangalie namna muundo mwenyewe wa MSD ulivyokaa na namna ambavyo watatekeleza taratibu za manunuzi ya dawa kwa urahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ifanyike tathimini ya kina ya wadau wa MSD kwenye ule mnyororo wa usambazaji wa dawa. Ifanyike tathmini ya kina: Je, ni kweli kwamba wale wadau wote sio washindani wa MSD ambao wakati mwingine wako kwenye vituo vyetu na wao ni wafanyabiashara? Kwa sababu wanataka kufanya biashara, wanasababisha kwa makusudi dawa zisifike kwa wakati kwenye vituo ili zile dawa zilizoko kwenye maduka yao ziweze kuuzwa? Kwa hiyo, tathmini ya kina hiyo ifanyike ili tujue nani ambaye wakati mwingine anakwamisha dawa hizi kufika kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Mamalaka ya Dawa na Vifaatiba; kwenye eneo la kufuatilia ufanisi na ubora wa vifaa vile vikubwa, hasa vinavyotumika kwenye uchunguzi na tiba; Serikali imewekeza sana faida nyingi kwenye eneo hilo. Hivyo vifaa vikinunuliwa tuvifuatilie ufanisi wake. Hata hivyo ili vifaa hivyo vifanye kazi vizuri, vinahitaji matangenezo kinga (prevent maintenance).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuhakikishe kwamba tunawaajiri wataalam wa kutosha wa kufanya hiyo kazi ya matengenezo ya vifaa tiba, lakini tuhakikishe kwamba tunawashirikisha kwenye hatua za awali zile za kufanya manunuzi kwa maana ya kufanya uchaguzi wa teknolojia sahihi, lakini kufanya uchambuzi wa kina wa teknolojia wa vifaa tiba na hatimaye tuwashirikishe kwenye hatua ya uhamishaji wa teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwashirikishe vizuri hao wataalam. Sasa tunao wataalam wa kutosha wa vifaatiba, lakini Serikalini bado wataalam hao hawapo. Ninaishauri Serikali watoe ajira kwa wataalam kwa wataalam wa vifaa tiba. Tunavyo vifaa vingi kwenye sehemu zetu na vifaa vingi havifanyi kazi na sehemu kubwa ukiangalia, hatuna wataalam wa kuviangalia hivyo vifaa. Serikali iwekeze kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwekeze kwenye eneo la mafunzo ya wataalam wa vifaatiba. Walipo, ngazi ya mwisho ni Shahada. Tuwekeze kwenye Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu ili tafiti zifanyike hapa nchini tuanze kutengeneza vifaatiba vyetu wenyewe na hatimaye tuanze kujitegemea kama nchi badala ya kutegemea vifaa vingi tunavyoviagiza kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)