Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyopo mezani kwetu. Nianze kwa kuunga hoja mkono, lakini nitajikita katika maeneo matatu. Eneo la kwanza ni lile ambalo ameishia dada yangu Mheshimiwa Husna, ni kuhusu upungufu wa watumishi katika sekta hizi mbili ambazo Kamati yetu inahusika, idara ya elimu na idara ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi katika kada hizi mbili. Waheshimiwa Wabunge humu wakitaka watoe takwimu wataonesha wazi kwamba, kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa au kwenye Majimbo kuna changamoto kubwa ya upungufu wa idadi ya Walimu na watumishi katika sekta ya afya. Kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan na ujenzi wa madarasa zaidi ya 15,000 na hostels 50 na vituo vya afya impact yake haitaonekena vizuri sana upungufu huu ukiendelea. Kwa hiyo, naomba Serikali sasa ichukue hatua za makusudi kuhakikisha kwamba, kibali maalum kinatolewa kwa ajili ya ajira ya Walimu na ajira ya watumishi wa sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma kulikuwa na upungufu wa Wahasibu katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Serikali ikafumba macho ikatoa ajira ya Wahasibu watano kila halmashauri. Naiomba Serikali yangu sikivu ifanye hivyo, itoe kibali maalum kwa ajili ya watumishi wa sekta ya afya na watumishi wa sekta ya elimu

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taarifa yetu tumezungumzia vilevile kuhusu Chuo Cha Ualimu Mtwara. Wakati tunatekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari mwaka 2005 hadi 2009 kulikuwa na mapendekezo, ili kuongeza idadi ya Walimu wa sayansi vyuo vitatu vibadilishwe kuwa vyuo vikuu vishiriki; Chuo Cha Ualimu Mtwara, Chuo Cha Ualimu Dar-es-Salaam na Chuo Cha Ualimu Mkwawa. Vyuo viwili hivi vimeshabadilishwa kuwa vyuo vikuu vishiriki, Chuo Cha Ualimu Dar es Salaam ni DUCE sasa hivi na Chuo Cha Mkwawa kimeshabadilishwa kuwa MUSE, ni chuo kikuu kishiriki cha Mkwawa, bado Chuo Cha Ualimu Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo cha Ualimu Mtwara kina facilities zote; kuna eneo la kutosha kwa ajili ya upanuzi, kuna bwalo la kutosha, madarasa ya kutosha na majengo ya utawala na vyumba vya mihadhara vya kuanzia vipo tayari. Kwa hiyo, naomba Serikali itekeleze ile azma yake ya kukibadilisha Chuo cha ualimu Mtwara kuwa Chuo Kikuu Kishiriki cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Facilities zote kama nilivyosema zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye elimu kuna kitu kinaitwa skill over effect; tukijenga Chuo Kikuu Kishiriki Mtwara Wana-Mtwara wengi watahamasika kusoma kutoma elimu ya Chuo Kikuu kwa sababu wataona Chuo Kikuu kipo jirani yao. Kwa hiyo, naomba azma hiyo itekelezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine, wakati tunafanya mahojiano na Wizara hizi mbili za kisekta; elimu na afya, kuna kuingiliana kwa majukumu kati ya TAMISEMI na Wizara za kisekta; elimu na afya. Hata juzi tulifanya kikao cha kuwakutanisha TAMISEMI na Wizara ya Elimu. Hata kama tunafahamu kwamba kuna collective responsibility, siyo vizuri mtumishi au mtumishi wa Wizara fulani kusema Wizara fulani inamwingilia, lakini ukienda kwenye utekelezaji, tunaona kuna changamoto ya kuingiliana, yaani Wizara za kisekta na TAMISEMI wanaingiliana. Hili liko wazi tu kwamba ile (D by D) ugatuaji bado haujaeleweka vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watumishi wa Serikali bado dhana ya ugatuaji hawajaielewa, lakini mpaka kuna baadhi ya viongozi vile vile dhana ya ugatuaji bado haijaeleweka. Udhaifu mwingine ni kwamba hakuna sheria ambayo inalinda ugatuaji. Ugatuaji unaongozwa na policy paper ya mwaka 1998. Kwa hiyo, naomba vitu viwili kama tulivyoshauri kwenye kamati yetu; kwanza, elimu ya ugatuaji itolewe kwa watendaji na viongozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, muda sasa umefika wa kuhakikisha kwamba Serikali inaleta sheria ya kusimamia huu ugatuaji ili kusiwe na kuingiliana kati ya Wizara na TAMISEMI. Tukifanya hivyo, tutarahisisha utekelezaji wa majukumu katika ngazi ya chini. Huko chini kuna kuingiliana sana kati ya TAMISEMI na Wizara nyingine za kisekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)

MWENYEKITI: Umeunga mkono hoja Mheshimiwa?

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishaunga mkono hoja mwanzoni. Kwa hiyo naunga mkono hoja kwa mara ya pili sasa hivi.