Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote na mimi niungane na wenzangu kukupongeza. Pamoja na hayo yote pia niendelee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya yako na unavyoendelea kutuongoza.

Mheshimiwa Spika, naomba niunge mkono hoja nzuri iliyowekwa mezani hapa na Kamati yetu, kwa sababu ukiangalia hoja zao zote wametoa mawazo mazuri. Mawazo ambayo yanaendelea kutuimarisha sisi kama Wizara ya Ardhi, lakini pia kuishauri Serikali juu ya nini kifanyike. Yapo maeneo ambayo nataka nichangie kidogo ili kuweka zile taarifa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza limezungumzwa hoja ya kukwama kwa miradi mikubwa minne ya Shirika la Nyumba. Pale katika Mkoa wa Dar es Salaam wakimaanisha Plot No. 300 ya Regent, Plot No. 711 na nyingineyo ikiwemo ya Morocco Square.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika moja ya mawazo mazuri yaliyotolewa na Kamati ni kwa…

Mheshimiwa Spika, nisamehe kidogo unajua tumeshazoea. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Hakuna neno Naibu Spika ni msaidizi wangu kwa hiyo usiwe na wasiwasi. (Makofi/Kicheko)

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wewe ndio mkuu wa Mhimili basi watu wote wako chini yako.

Mheshimiwa Spika, nataka nieleze kwamba Serikali imefanya juhudi kubwa sana kuhakikisha kwamba, miradi ile inakwamuka kutoka pale ilipokwama ili sasa iweze kukaa vizuri. Katika hatua ambazo tumefanya ndani ya Wizara ilikuwa ni kuomba Serikali itupe ruhusa, ya kuchukua fedha au kupata fedha kutoka ndani ya vyanzo vyetu. Ikiwepo almost karibu Shilingi bilioni 700 ili twende tukafanye utaratibu huo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan akaelekeza Kamati, inayosimamia madeni iangalie vizuri juu ya yale ambayo sisi tumeyaomba. Katika kuchakata kwake ikaturuhusu tukope, Shilingi bilioni 44.7 ili tuweze kumalizia miradi hiyo. Katika fedha hizo ambazo zilielekezwa Shilingi bilioni 19 ilikuwa ni kwa ajili ya mradi uliopo katika Plot No. 300 na iliyobakia iende kumalizia Morocco Square.

Mheshimiwa Spika, juu ya lile eneo la Kawe maelekezo yako wazi kwamba, tukae na mbia katika ule Mradi wa Kawe ili tuweze kuzungumza naye na baada ya kumaliza kuzungumza naye, basi makubaliano tutakayokubaliana nayo tuone tunakwendaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua iliyofikiwa mpaka sasa baada ya mikutano mitatu ni kwamba mbia wetu anakwenda kuwasiliana na wenzake ndani ya Bodi yao, ili yatakayokuwa yamekubaliwa basi tuje kuzungumza kwa pamoja ili tuweze kwenda vizuri. Kwa faida ya kikao hiki eneo ambalo limejengwa yale maghorofa unayoona Kawe pale, ni eneo ambalo miliki yake iko chini ya National Housing. Kwa hiyo, mazungumzo yanayofanyika ikiwezekana ni kutoa kile kipande, cha lile eneo ili sasa tuweze kupewa nafasi sisi wenyewe. Tuweze kujenga majengo yale ili majengo yakae vizuri na Watanzania, wapangishe na yanayouzwa yauzwe ili sasa tuweze kupata faida ya mradi ule.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo pia ndani yake limezungumzwa na ushauri mzuri umetolewa na Kamati, juu ya Serikali kutochangia fedha katika miradi ya upimaji, upangaji na umilikishaji. Nataka nilihakikishie Bunge lako kwamba, neno hili halina ukweli wowote. Serikali imekwishatoa fedha na maelekezo yametolewa juu ya kuhakikisha kwamba, miradi hii inakwenda kupangwa vizuri. Katika kufanya jambo hilo fedha Shilingi bilioni 50 zimetolewa na zimekwenda kwenye Halmashauri zaidi ya 44 ili Serikali au Halmashauri zetu zikapime vizuri maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa furaha kubwa zaidi katika bajeti inayokuja Serikali inapanga kutumia zaidi ya Dola milioni 150, ambayo ni sawa na Shilingi bilioni 400 kwenda kuwasaidia zaidi kuendelea kupanga nchi yetu. Pia kuendelea ku-finance hii miradi ya upimaji, upangaji na umilikishaji.

Mheshimiwa Spika, yako mengi ambayo Serikali inaendelea kufanya, lakini nataka niwahakikishie kwamba mifumo, iko tayari kwa ajili ya kukabiliana na changamoto za ardhi nasi ndani ya WIzara tunaendelea kutoa elimu pale ambapo tunapata nafasi. Sera zile ambazo zimepitwa na wakati, zimeendelea kupelekwa katika vikao husika ili ziweze kuhusishwa. Halafu baada ya hapo Serikali au wadau mbalimbali, tuendelee kuhimiza katika mipango mizuri ya usimamizi wa ardhi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa. Ahsante. (Makofi)