Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nami ningependa sana kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza katika mjadala huu wa Sheria Ndogo juu ya mabadiliko au mapungufu ambayo tumeyaona katika uchambuzi tulioufanya ndani ya Kamati yetu. Leo sitakuwa na mengi sana ya kusema isipokuwa ni kukumbushana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ya msingi ambayo yamekuwa mara kwa mara tunapoleta taarifa zetu hapa yamekuwa yanatokea. Jambo la kwanza ambalo kwangu mimi ninaona ni la kwanza kwa umuhimu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria Ndogo nyingi zinazoandikwa zimeendelea kuwa sheria zinazokinzana na hali halisi kwa maana ya utekelezaji wa majukumu yake. Kwa mfano, ipo sheria ambayo ndani ya taarifa yetu inaonekana inahusu Sheria ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sheria ile yameelezwa masharti ambayo mvuvi au mfanyabiashara wa samaki anatakiwa kuyatimiza ili aweze kupata vibali kwa ajili ya kufanya biashara hiyo, lakini kwangu mimi na wenzangu ndani ya uchambuzi wetu tumelitazama jambo hili katika upanda wake hasa katika lile hitaji la kumfanya huyu anayeomba kibali kwa ajili ya kufanya biashara hiyo aweze kuwa na vitambulisho muhimu ikiwemo kile cheti kinachoonesha uthibitisho wa yeye kuwa amezaliwa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sheria zetu za nchi sasa hivi ni wazi zimeweka kwamba mwananchi ili aweze kuthibitishwa mojawapo lazima awe na kitambulisho cha uraia, lakini bado sheria hii inataka kuangalia zaidi ya kile kitambulisho chake cha uraia, kwa maana ya kuthibitisha kama ambavyo wenzetu nchi nyingine wanafanya, tukitolea mfano kwa mfano Japan kule ambapo mtoto au mimba tu inapotungwa tayari mzazi anapewa kitabu na kijiji kinamsajili kwa maana ya kwamba sasa kuna kiumbe kipya tunamtarajia katika maeneo hayo. Sheria ambayo katika Tanzania haipo na wala haizungumzwi hivyo, masharti yenyewe yalivyowekwa ni magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa upande mwingine imeelezwa hapa sheria hii inamnyima haki yule mvuvi wa kawaida aliopo pale Kigoma aweze kufanya biashara hii. Kwa sababu inamtaka mvuvi huyo aweze kufungua kampuni, lakini kwa kufungua kampuni maana yake pia anatakiwa awe na tin number. Sasa Bunge lako linajua hali za wavuvi wetu, lakini pia ni moto wa Serikali yetu kuona jinsi gani inawasaidia wale wanyonge wa Tanzania ili waweze kujikomboa katika hali ya umaskini walionayo. Sasa leo hii mtu mwenye mifuko yake miwili ya samaki naye pia anatakiwa awe na hivyo vibali jambo ambalo kwa kweli kama kamati tuliona haliendani na hali halisi ya maeneo yetu haya ambayo tunaishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu pia lipo jambo la sheria zetu hizi kusahau msingi wa uandishi au utungaji wa sheria zetu yaani drafting principles. Mara kwa mara tunaposimama Bungeni hapa tunaendelea kukumbusha Serikali, wakati mwingine sheria hizi si jambo la dharura ndani ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kwa maana ya kwamba wanatakiwa wakae chini, watunge sheria wakiwa wametulia, wakague katika principles kama zimetimia, lakini kila siku zinapokuja sheria kumekuwa na mapungufu hayo kwa hiyo kwangu la msingi zaidi narudi tena kuikumbusha Serikali, utaratibu wetu ulivyo upo wazi, sheria hizi wanaanza wao wenyewe katika Ofisi za Attorney General huko kuzitengeneza siamini kwamba sheria hizi labda zinaandikwa na mtu mmoja na kwamba zinafika hapa iwe sisi kazi yetu badala ya kusimamia maendeleo ya nchi iwe kazi yetu kuangalia na kugundua makosa yakiwemo yale ambayo yanatakiwa ndani ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu yawe yanaangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia yapo matatizo mengine ambayo sheria hizi zinakosewa sana na katika jambo kubwa ambalo kwa wanasheria tunasema hizi ni fundamental error katika uandishi au tafsiri ya sheria ya kukosea kuweka vifungu vinavyohusika au vifungu halisi katika sheria. Kwa mfano, yapo baadhi ya majedwali yanaonekana katika uandishi huu, mtu kwa mfano jedwali la kwanza la sheria linanukuu kipengele au kanuni ya tatu ya sheria wakati Kanuni halisi ya jedwali hilo labda ni kanuni ya nne. Kwa hiyo imekuwa mara kwa mara jambo hilo linatokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sheria kwa mfano nikizungumzia kwa sheria hii ya samaki maana yake kwa yeye ambaye anataka kwenda kutafuta hivyo vibali maana yake akienda akitumia sheria hii ni wazi anakuwa yuko nje ya utaratibu na anaweza akajikuta sheria yenyewe pia haiwezi kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini siyo mwisho kwa umuhimu naomba niikumbushe tena Serikali lakini hasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kuendelea kukumbuka kwamba nchi hii katika sheria zake zinaanzia kwenye Katiba ambayo ndiyo Sheria Mama na ndiyo mwongozo wake, lakini siyo Katiba peke yake, lakini pia kwa Sheria Ndogo zinaanzia kwenye Sheria Mama ambayo inampa mamlaka yule ambaye anakwenda kutunga Sheria Ndogo hizi, lakini mara nyingi sana kumetokea matatizo ya kwamba waandishi wetu wanasahau kwenye uandishi mamlaka hayo au kutambua mamlaka hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu kutambua mamlaka pia tumeona katika baadhi ya sheria, zikiwemo sheria zile zinazozungumzia masuala ya mazingira kwamba unakwenda unakuta sheria ambayo inapewa references haifanani kabisa na sheria ambayo imeletwa mbele yetu kama Kamati yako ya Sheria ya Bunge. Kwa hiyo, kwangu nilianza kusema kwamba leo nasimama kuendelea kuikumbusha Serikali yapo mambo ya msingi ambayo ni lazima yaendelee kuangaliwa katika utunzi wa Sheria Ndogo hizi na katika mambo hayo ya msingi zaidi ni kuendelea kukumbuka wapi mamlaka imetolewa, lakini pia zile principles za drafting za sheria zetu pia kuangalia kwamba sheria zenyewe zinaendana na hali halisi ya maisha ya Watanzania ambao wanakwenda kuathirika kwa namna moja au nyingine na sheria hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi naunga mkono hoja ya Kamati. Ahsante sana. (Makofi)