Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Ng'wasi Damas Kamani

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru sana kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika mjadala huu wa Mpango wa Mwaka Mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kuu itakuwa kuwazungumzia wapigakura wetu walio wengi katika nchi hii ambao ni vijana. Changamoto namba moja, ambayo nitaendelea kuipigia kelele ambayo ni ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan kwa sababu, ndani ya muda mfupi ambao ameingia vijana ni kundi ambalo ameendelea kulibeba, ameonekana kutokulisahau na hata katika maamuzi mbalimbali ameendelea kutukumbuka. Kwa hilo tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mambo machache tu ambayo ningependa katika Mpango huu ambao ni wa mwaka mmoja basi tuyazingatie kwa kuangalia vijana hawa. Kama tunazungumzia asilimia zaidi ya 60 ya watanzania wote ambao ni vijana, maana yake tulitegemea discussion kubwa may be asilimia zaidi ya 30 ya Mpango huu uwe unalenga kuliangalia kundi kubwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwenye hili hasa katika suala hili la ajira niongelee mambo machache. La kwanza, tangu Mheshimiwa Rais ameingia madarakani kwa hii miezi sita kuna ajira nyingi sana zimeshatangazwa zaidi ya ajira 5000, katika taasisi mbalimbali kuna TANAPA, TAKUKURU, POLISI, TRA tunashukuru sana. Kwa hilo, tunashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna vigezo ambavyo vimekuwa vinajumuishwa kwenye qualification za watu wanaotakiwa kuomba ajira hizi, ambazo kwetu sisi vijana tunakiri kusema kwamba zinatutatiza kidogo. Kwa mfano; kuna kigezo cha mtu awe amekwenda National Service au JKT. Tukiangalia katika Nchi yetu, kwanza kabisa nafasi za JKT zinazotangazwa huwa ni chache ukilinganisha na idadi kubwa ya vijana tuliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mbili hata wale ambao wana ule mfumo wa kutoka form six kwenda JKT bado Serikali yetu haiwachukui vijana wote. Kuna baadhi ya miaka vijana wamechukuliwa kulingana na division zao kwamba, mwenye division one na division two peke yake ndiyo watakwenda. Lakini kuna baadhi ya miaka wamechukuliwa vijana kwa alphabetical order ya majina yao. Kwamba, kwenye wale wenye walioanzia A labda mpaka J ndiyo watakwenda wanaobaki wanabaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, naona inasikitisha sana kama tukianza kutoa ajira kwa vijana kwa kuwahukumu kulingana na alphabetical order ya majina yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwa vile ninaanziwa na N basi ajira fulani fulani nizisahau au kwa sababu nilipata division three, lakini qualification zote ninazo basi ajira fulani fulani nizisahau. Kigezo hiki si sawa na kama Serikali yetu ilikuwa inaona kwamba ni muhimu kutangaza ajira kwa vigezo vya namna hii, basi ingeanza kwanza kutengeneza mazingira ya vigezo hivi ndiyo twende kwenye ajira kulingana na vigezo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadiriki kusema kwamba tukiendelea na vigezo kama hivi tunavunja Katiba yetu hasa Ibara ya 13(4), ambayo inakataza Kitengo chochote cha Serikali au Mamlaka kutoa maamuzi yoyote ambayo yataleta ubaguzi kwa watanzania kwa namna yoyote ile. Kwa hiyo, nashauri kuanzia sasa Serikali yetu iangalie, tunapokuwa tunatoa ajira au fursa kwa vijana wetu, ili wote tuweze kuzi- access kwa usawa basi tuangalie vigezo ambavyo vina maana na ambavyo vina maslahi katika utekelezaji wa ajira hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili ni suala zima la mitandao. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu miezi kadhaa iliyopita, hali ya hewa ilichafuka kidogo baada ya gharama ya mitandao kupanda na akatoa maelekezo kwamba gharama hizo zirekebishwe lakini suala hili lisijitokeze tena. Sisi vijana tunatumia sana mitandao siku hizi kujiajiri, na hii imeipunguzia sana Serikali mzigo wa kutuajiri sisi vijana. Lakini si kujiajiri tu, tunatumia pia mitandao hii kusoma kwa hiyo inachukua nafasi kubwa sana katika maisha yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa changamoto iliyokuja ni kwamba baada ya Mheshimiwa Rais kutoa maelekezo kwamba hali hiyo irekebishwe na isijirudie tena, imeanza kurudishwa kidogo kidogo, kidogo kidogo, mpaka sasa tunavyozungumza imerudi hali ile ile aliyoikanya Mheshimiwa Rais. Nitoe tu mfano kidogo kwamba katika takwimu zilizotolewa na TCRA kwa mfano mdogo tu wa mtandao wa Airtel. Gharama ya MB 1 kwa takwimu za robo mwaka kwa Disemba, 2020 ilikuwa ni shilingi 5/= kwa MB 1 kwa mtandao wa Airtel. Robo iliyofuata ambayo ni Machi, 2021 ilibaki hivyo hivyo shilingi 5/=.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Juni, 2021 imepanda mpaka shilingi 9/= almost twice na kwa vile tu TCRA hawaja upload taarifa ya robo iliyofuata ambayo inakwisha mwezi Septemba, 2021. Maana yake tunategemea itakuwa imepanda zaidi, ni ngumu sana kwa kijana wa Kitanzania ambaye anategemea mitandao hii kujiajiri. Kutumia gharama kubwa namna hii ambayo haistahimiliki kuweza kufanya shughuli zake na kimsingi, Serikali inakuwa imeshindwa kabisa kumsaidia Mtanzania kijana wa kitanzania kutengeneza mazingira bora ya kujiajiri mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha zaidi ni kwamba Serikali yetu pia ni shareholders kwenye mitandao hii ya simu. Kwa hiyo, ina nafasi kubwa sana pia ya kutusemea na kutusaidia kutengeneza mazingira bora ili vijana tuweze kuendelea kujiajiri kupitia mitandao hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nizidi kumshukuru sana Mheshimiwa Rais na ama kweli ni haki kusema kwamba tumepata mama mtafutaji kweli kweli. Mama atakwenda akirudi anawaambia nimerudi na kijisenti hiki kidogo tutagawana hivi tena kwa uwazi kabisa. Hilo tunamshukuru sana na kwa kweli sisi kama vijana, anazidi kutupa imani ya kwamba miaka hii minne inayofuata itakuwa ni miaka ya neema kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia hayo nilitegemea basi, kulingana na fedha hizi za Covid ambazo tumepata, tumepata madarasa 15,000 ya Sekondari, tumepata Shule Shikizi madarasa kama 3000, tumepata ambulance 395. Lakini pia, kwa fedha za tozo hizi hizi kwa maarifa ya Mheshimiwa Rais tunapata pia madarasa mengi sana katika shule zetu za Misingi na Zahanati. Basi nilitegemea katika Mpango huu wa mwaka mmoja wa bajeti unaofuata tungeona basi Serikali yetu kwa kuangalia pia tuliwaahidi wapiga kura, tuliwaahidi vijana hawa ajira milioni 8 tuone ajira ambazo zitapatikana. Hasa za walimu, madereva na wauguzi au watendaji katika Sekta ya Afya zinakuwa reflected katika Mpango huu, hasa kwa mwaka unaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo nita-subscribe kwa alichokisema Mheshimiwa Kingu jana kwamba, tutatibu kitu kimoja lakini tutazalisha changamoto nyingine ya kutokuwa na ubora. Either katika elimu au katika Afya kwa sababu tutakuwa na madarasa mengi, wanafunzi wengi bila kuwa na watumishi wa kutosha. Ninaomba tukuze imani ya vijana hasa kwa Serikali yetu kwa kuakisi hizi juhudi za Mheshimiwa Rais. Katika Mpango huu tuoneshe namna gani Serikali imejipanga kutangaza ajira za kutosha kwa walimu, kutangaza ajira za kutosha kwa wauguzi na madereva. Ili tuzidi kuiamini Serikali yetu na vijana tujiandae kuweza kukidhi matakwa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine nimalizie, wakati Wabunge wengi wanazungumza, wamezungumza juu ya vipaumbele na mimi nikinukuu mchango wangu katika Mpango uliopita wa Bajeti iliyopita, niliomba kwamba ni muhimu Serikali yetu ikaja na vipaumbele ambavyo vitatuongoza katika mipango yote tunayotengeneza. Wabunge wengi wamekwishazungumza kwamba ni matakwa yetu kama wawakilishi wa wananchi tulitaka kipaumbele kiwe Kilimo. Sasa katika kilimo mwaka huu, mwaka 2021 Mpango wa Taifa wa kuwashirikisha Vijana katika Kilimo ndiyo unamalizika na umekwisha malizika Oktoba, 2021. Mpango huu ulikuwa unaanza 2016 – 2021 na kuna observation fulani zimeonekana katika Mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya observation hizo ni kwamba kilimo it is not attractive kwa vijana kushiriki katika Sekta ya Kilimo katika Nchi yetu. Sasa nilitegemea kwa vile Mpango huu umekwisha, basi huu Mpango unaofuata wa mwaka huu ungetuonyesha kwamba, sasa tu-test mafanikio ya huu Mpango wa miaka minne uliofanyika wa kuwashirikisha vijana katika Kilimo. Lakini pia una Mpango gani mpya sasa baada ya kuangalia mafanikio ya Mpango huu, wa kuhakikisha kwamba basi kilimo kinaanza kuwa- attract vijana ili wote tuweze kushiriki. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwasi.

MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)