Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia Wizara hii ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wanaendelea kufanya na kwa presentation nzuri waliyofanya asubuhi ya leo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie mambo mawili au matatu kama muda utatosha. La kwanza, ni majengo ya zahanati na vituo vya afya. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imesema tunajenga Zahanati kila Kijiji na tunajenga Vituo vya Afya kwenye kila Kata. Maana yake, haya ni majengo ili huduma za afya ziweze kutolewa kwenye majengo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa najaribu kuangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri sikuona kiuwazi sana mpango mahsusi juu ya jambo hili la Vituo vya Afya kwenye Kata na Zahanati kwenye Vijiji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma pia hotuba ya Waziri wa TAMISEMI, lakini na kwenyewe sikuona kwa uwazi sana. Jambo hili linazungumzwa vizuri na mkakati mahsusi umewekwa ili kuhakikisha kweli tuna zahanati kwenye kila kijiji na tuna vituo vya afya kwenye kila kata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma hizi za afya zinatolewa kwenye majengo yenye viwango maalum; siyo kila jengo tu linaweza kuwa zahanati au kituo cha afya. Sasa kama hatujazungumza kwa uwazi hapa; na kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi jambo hili tulilizungumza sana kwa wapiga kura wetu na wengine tumehamasisha, wameanzisha maboma na mengine yamekwisha, yaliyofikia kwenye lenta, yapo mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najiuliza, nikirudi naenda kuwaambia nini wananchi wangu sasa ambao tayari wana maboma yamekwisha, bado kuezekwa? Yapo maboma mengi kwenye Jimbo langu la Maswa Magharibi yamekwisha bado kuezekwa tu, lakini kwenye mpango wa Mheshimiwa Waziri wa Afya na hata kwenye mpango wa Waziri wa TAMISEMI sijaona. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwamba wakati Mheshimiwa Waziri anakuja kuhitimisha, atuambie angalau mpango mkakati ni upi kuhusu zahanati kwa kila Kijiji na kituo cha afya kwa kila kata, vinginevyo, watu wetu tutawakatisha tamaa. Nina maboma mengi kwenye Jimbo langu na nilichokuwa nawaambia wapiga kura wangu ni kwamba Serikali watatusaidia kuyamaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko boma kwenye Kijiji cha Bukangilija, liko boma Kijiji cha Nyabubinza, liko boma Kijiji cha Mwanubi, liko boma Kijiji cha Mwang‟anda; yako maboma mengi! Sasa kama hayapo kwenye mpango huu, kwa kweli nasikia baridi kwamba nitakapokutana na watu wangu itakuwaje? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa akijumuisha hotuba yake, basi atuambie mpango mahsusi hasa kwa ajili ya kila kijiji kuwa na zahanati yake, kila kata kuwa na kituo cha afya, ni upi hasa ili tuweze na sisi kuwa na matumaini kwa wapiga kura wetu pia? Kwa hiyo, hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni suala la ubora wa huduma za afya kwenye maeneo yetu. Nashukuru kwamba wamefanya uhakiki Wizara, kwenye hotuba ya Waziri ameelezea; wamefanya uhakiki na kutathmini na walikuwa wanavipa vituo vya afya au zahanati, zile zinazotoa huduma za afya alama za nyota ya kwanza mpaka ya tano. Sasa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukijaribu kuangalia, vituo hivi vinavyotoa huduma ya afya karibu asilimia 87 vilipata nyota kati ya sifuri (0) na moja (1).
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kuonesha kwamba huduma zinazotolewa kwenye vituo vya afya na kwenye zahanati bado ni duni sana. Ukweli tunaufahamu kwa sababu tunatoka kwenye maeneo hayo. Sasa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri sikuona pia mpango mkakati ni upi kuhakikisha kwamba hizi huduma zinakuwa bora kwenye hivyo vituo ambavyo wao wamevihakiki. Sijaona mpango mkakati ni upi ili kufanya huduma hizi ziwe bora kwenye maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake, huduma zinazopatikana kwenye zahanati au vituo vya afya, maana maeneo haya ndiyo yanayotoa huduma za msingi za afya kwenye maeneo yetu, siyo nzuri. Nina Kituo changu cha Afya cha Mwasai kinahudumia Kata tatu; Kata ya Masela, Kata ya Seng‟wa na Kata ya Isanga. Kituo hiki cha Afya kina Nurse mmoja na Clinical Officer mmoja; watu wawili ndio wanaofanya kazi pale, vifaa tiba pale havitoshelezi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata mfadhili kwenye hicho Kituo cha Afya akatuletea vifaa vya upasuaji, viko kwenye container mpaka leo. Tukiuliza kwa nini havifanyiwi kazi, wataalam wanatuambia hakuna Daktari pale. Hii inaonekana kwamba watumishi kwenye zahanati na kwenye vituo vya afya ni pungufu sana. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri watutazame kwa jicho la pekee wa maeneo hasa ya vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu nina vituo vya afya viwili; Kituo kingine kinaitwa Malampaka na chenyewe ni hivyo hivyo, kina container la upasuaji lakini limekaa tu, halifanyiwi kazi, vifaa vipo vimekaa tu. Tatizo ni kwamba hakuna mtaalam. Pia pale kuna tatizo la ziada kwamba hakuna jengo la upasuaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu Serikali wakiwa wazi na kutuambia tunatatuaje haya matatizo ili huduma za afya kwenye maeneo yetu ziwe angalau bora? Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema, maeneo mengi yanayoonekana ni mazuri ni kuanzia kwenye wilaya, mkoa na kuendelea juu, lakini ukishuka chini huduma za afya siyo nzuri sana. Kwa hiyo, tunaomba Serikali itoe kipaumbele kwenye maeneo haya ili watu wetu pia ambao ndio wengi wapate huduma zinazotosheleza kwa ajili ya afya zao ili waweze kufanya na kujitafutia maendeleo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ni huduma za ugonjwa wa saratani. Saratani imekuwa tatizo kwenye nchi yetu sasa hivi. Nilikuwa najaribu kuangalia takwimu sikuzipata vizuri, lakini inavyoelekea tatizo la saratani linaongezeka, maana watu wanaotoka kwenye maeneo yetu ni wengi; wanapochunguzwa wanakutwa na saratani, lakini huduma za matibabu au huduma za kupunguza ukali wa tatizo hili zipo tu Ocean Road, Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba Serikali ifikirie ni kwa namna gani inaweza ikawa na huduma za matibabu kwenye Kanda au Mikoa ili kutuletea huduma hii ya matibabu kwa ugonjwa huu karibu na wananchi wetu? Vinginevyo ni ghali mtu wa kutoka kule Kijiji changu cha mwisho Jija atafute usafiri aende Maswa Shinyanga, baadaye apande basi mpaka Dar es Salaam akatafute matibabu, ni ghali sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba Serikali inapojibu itueleze mpango wake ni upi hasa ili kuwapunguzia wananchi wake adha za kupata matibabu hasa kwa ugonjwa huu ambao sasa unakuja juu kwenye maeneo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni hayo kwa siku ya leo, lakini nimalizie kwa kuwapongeza hawa…
MWENYEKITI: Ahsante, muda wetu ndiyo huo.
MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.