Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia napenda tu kutoa taarifa kwamba, leo alfajiri nilipokea taarifa ya kusikitisha ya kuondokewa na mzee wetu, aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM kati ya mwaka 2012 hadi 2017 katika Wilaya ya Kilwa. Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu Mwenyekiti wetu, Yusuf Bakari Kopakopa mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa taarifa hiyo, naomba niendelee kuchangia sasa. Kwanza naishukuru Serikali yetu ya Awamu ya Sita ikiongozwa na mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikifanya kwa Watanzania katika kuwaletea maendeleo na kuondoa kero mbalimbali ambazo zimekuwa zikitokea kupitia miradi ya maendeleo ambayo imekuwa ikifanikishwa na Serikali yetu.

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, siyo kwamba namkatiza Mheshimiwa Ndulane, lakini yuko vizuri kabisa, mnamuona yuko na karatasi zake vizuri kabisa bila wasiwasi wowote ule. (Kicheko)

Mheshimiwa Ndulane, endelea bwana na tunakupa pole kwa msiba wa Mheshimiwa Mwenyekiti wetu, poleni sana.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kwa kweli Serikali yetu imefanya kazi kwa ufanisi mkubwa ndani ya kipindi kifupi na kwa kweli mambo mengi yameonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu unafahamu vizuri sana ramani ya jimbo langu, kuna mambo yamefanyika, haya kwa mfano ya madarasa, kwenda shule za sekondari na shule shikizi mpaka katika maeneo ambayo yalikuwa hayatarajiwi. Hii imeleta hamasa kubwa kwa wananchi wangu kuweza kui-support Serikali yetu. Vilevile maji, madawati na huduma nyingine. Kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kutuongoza vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, isipokuwa nina angalizo tu; taratibu nyingi zimetolewa za ufuatiliaji na usimamizi wa miradi hii. Naomba katika kipindi hiki cha utekelezaji wa miradi sisi Wabunge wote tutakapotoka hapa Bungeni twende tukafuatilie na kuisimamia vizuri hiyo miradi ili tija iweze kupatikana. Vilevile kitengo cha ukaguzi wa ndani katika kila halmashauri kiweze kuimarishwa vizuri na kitumike kufuatilia vizuri miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nyongeza napenda katika Mpango sasa ambao tunauendea wa 2022/2023 tuweze kuona changamoto nyingine za miundombinu, hasa hii ya elimu na afya ziweze kutekelezwa vizuri. Kwa mfano, kuna eneo la mabweni; mpaka sasa hivi kuna baadhi ya shule zetu za kata ziko mbali sana na kule wanapotoka wanafunzi. Nafikiri kwamba kunahitajika ujenzi wa mabweni ya wavulana na wasichana katika kuboresha huduma ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo katika jimbo langu ninakotoka, shule za kata ziko umbali wa kilometa mpaka 43, kilometa15, sehemu nyingine 17 toka shule iliko. Kwa hiyo naiomba Serikali yetu katika Mpango wa 2022/2023, basi tuone namna ambavyo huduma ya mabweni, lakini pia huduma ya matundu ya vyoo, vifaa vya maabara na maabara zenyewe, iweze kuimarishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujikita katika eneo la kilimo. Tumekuwa na Benki hii ya Maendeleo ya Kilimo, kwa kweli imefanya kazi nzuri, lakini kuna changamoto katika utekelezaji wa majukumu yake. Benki hii imetoa pesa nyingi, zaidi ya bilioni 100, tangu ilipoanzishwa mwaka 2014, lakini kumekuwa na shida katika kuwafikia wakulima wadogo wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya yangu ya Kilwa nina kaya zisizopungua 42,000 ambazo napenda kukuthibitishia mpaka kufikia wakati huu hakuna kaya hata moja ambayo imefikiwa na benki hii. Kwa hiyo naomba hii benki iongezewe mtaji ili iweze kuhudumia wananchi mpaka wale wa vijijini kabisa badala ya kuhudumia wananchi ambao wako katika zile skimu maalum za kilimo kama umwagiliaji na nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, alternative ya pili kwenye hili inawezekana mtaji ukawa mdogo katika ku-support hii TADB, basi naomba vilevile ikiwezekana tuanzishe Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo ambao uta-operate kutokea kwenye halmashauri zetu na utashirikiana na AMCOS zetu, utashirikiana na SACCOS zetu zilizopo katika maeneo ambayo wakulima wanatoka hasa hawa wadogowadoo wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kwamba upatikanaji wa pesa za mikopo za TADB unahusisha kujaza fomu nyingi ambazo wanavijiji wetu hawawezi kupata huo mkopo kiharaka, hasa ukizingatia kwamba Ofisi za TADB ziko mbali sana na maeneo ya vijijini. Hapa karibuni nilikuwa nauliza kwa mfano watu wa Singida wanapata wapi huduma za TADB, nikaambiwa wanapata Dodoma. Sasa yule mwananchi wa kule ndanindani kabisa Singida atafikaje Dodoma kirahisi, inakuwa ni ngumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Kilwa tunapata huduma kutokea Mtwara. Kwa hiyo nafikiri wakiongozewa mtaji, basi wanaweza wakatusaidia, lakini vilevile tukiunda Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo ambapo mikopo itatolewa bila riba, hii itasaidia sana wakulima wetu wa vijijini kuweza kuinuka kiuchumi na kuweza kuendelea mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kabisa ni suala la michezo. Msimu uliopita tulikuwa na performance nzuri sana hasa kwenye mashindano ya vilabu ya kimataifa, lakini mwaka huu mambo yamekwenda ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata michezo mingine pia, tuliona Simba na Namungo ambavyo zilifanya vizuri msimu uliopita na kutuweka katika ramani ya juu kabisa Barani Afrika na duniani kwa ujumla, lakini mwaka huu haikuwa hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia Timu yetu ya Biashara United ikishindwa kusafiri kwenda kucheza mechi ya marudiano Nchini Libya. Pia hata katika mchezo wa volleyball tumeshuhudia timu yetu ya Taifa ambayo ilitakiwa kwenda kushiriki mashindano kule Nchini Burundi ikishindwa kufika kwenye mashindano na hatimaye kufungiwa kama ambavyo Biashara United pia ilifungiwa.

Kwa hiyo niiombe Wizara ya Fedha ikishirikiana na Wizara ya Michezo kwa pamoja zishirikiane katika kuona namna ambavyo tutaweza kuzilea timu zetu za Taifa pamoja na timu hizi za vilabu ambazo zinapata nafasi ya kucheza katika mashindano haya ya kimataifa ili ziweze kutuwakilisha vizuri, zisipate huo upungufu ambao ulijitokeza, hasa wa kifedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja. (Makofi)