Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kidogo kwenye haya mapendekezo. Nianze kwa kuipongeza sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa kazi nzuri waliyoifanya, kwa kweli wamefanya kazi nzuri na mimi ni matumaini yangu kwamba Serikali watazingatia ushauri waliopewa na Kamati hii ya Bunge wamefanya kazi nzuri sana, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kushauri maeneo mawili makubwa, eneo la kwanza ni eneo la Deni la Taifa. Kwa taarifa zilizopo ukiangalia taarifa za Benki Kuu, hotuba ya Waziri na hata Kamati Kudumu ya Bunge ya Bajeti inaonekana Deni la Taifa limefikia trilioni 64, pamoja na kwamba taarifa zote zinasema kwamba deni hili bado ni himilivu lakiniā€¦

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa kidogo tu.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Halima.

T A A R I F A

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sikuwa na nia ya kumuingilia Mheshimiwa Mbunge, lakini ninataka nirekebishe kidogo Deni la Taifa kwa mujibu wa taarifa ya BOT iliyotolewa mwezi Septemba ni Trilioni 78, Deni la Serikali ndiyo Shilingi Trilioni 64 na tukiongeza na Trilioni 1.3 tuliyochukua mwezi Septemba maana yake Deni la Serikali sasa hivi ni Trilioni 65.7 huko. Kwa hiyo, Mheshimiwa naomba uendelee na mchango wako mzuri. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Taarifa hiyo Mheshimiwa Nape endelea na mchango.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea, amefanya ufafanuzi ambao pengine nilidhani sikuwa na haja ya kwenda huko, lakini hoja yangu ni nini, kasi ya ukuaji wa deni hili pamoja na kwamba tunaambiwa deni bado ni himilivu kasi yake siyo kasi nzuri, kwa sababu linatupeleka mbele ya safari siku tutakapoanza kusema siyo himilivu utakuwa ni mzigo mkubwa usiobebeka na itakuwa ni shida kwa uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipitie takwimu kidogo na hapa kwa kuwa Serikali inakopa kwa niaba ya wananchi na maana yake ni kwamba watakaokuja kulipa ni wananchi na Bunge tupo kwa niaba ya hao watakaokuja kulipa, nadhani ni vizuri tukafumbua macho tuangalie hii kasi inakotupeleka halafu tuwe wakweli tuambiane ukweli tuchukue hatua mapema kabla ya mambo hayajaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtakumbuka Awamu ya Tatu tulihangaika na hili suala la Deni la Taifa na Awamu ile walichukua hatua ya kuzungumza mpaka tukafikia mahali pa kusamehewa baadhi ya madeni. Wakati ule awamu ile kwa miaka kumi zilikopwa dola Bilioni Tisa. Awamu ya Nne zikakopwa Dola Bilioni Saba kwa miaka 10, Awamu ya Tano kwa miaka Mitano mpaka Sita zimekopwa Dola Bilioni Tisa kwa miaka mitano mpaka sita. Bahati mbaya mkopo huu ambao nautathmini wa miaka mitano, sita asilimia 40 ni mikopo ya kibiashara ambayo moja ya sifa yake ina riba kubwa, lakini inalipwa kwa muda mfupi, kwamba inaiva mapema mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii imepelekea hali ilivyo kwa sasa kama hizi takwimu ni za kweli, katika mapato yetu kwa mwezi tunatumia zaidi ya bilioni 800 kulipa deni ambayo ni asilimia 44 ya makusanyo kwa mwezi. Sasa kama kasi itaendelea hivi maana yake ni kwamba kuna uwezekano mkubwa asilimia ya makusanyo kwa mwezi yakawa yanatumika ku-service madeni na matokeo yake yakaathiri shughuli zingine za utoaji huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili pamoja na kwamba inawezekana namba zilizowekwa kufikia kutostahimilika bado zinaturuhusu, lakini siyo vizuri kupuuza kwamba fedha tunazotumia kulipa madeni kwa mwezi ni hela nyingi ambazo zinaathiri shughuli zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninayo mapendekezo yafuatayo: Pendekezo la kwanza ni kwamba Awamu ya Sita wameanza vizuri sana kwa kuweka uwazi wa pesa walizokopa zinakwenda kufanya nini kwenye shughuli zetu na mfano mzuri ni hii 1.3 trilioni imewekwa mezani kila mmoja anajua mpaka muuza mchina anajua imekwenda wapi. Sasa pendekezo langu kwanza utaratibu huu uendelee, upongezwe, uigwe uendelee tuweke wazi yale tunayoyakopa tunapeleka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hizi za nyuma ambazo zimekopwa na hakuna uwazi mkubwa sasa tuende kufanya ukaguzi kwenye account ya Deni la Taifa tujue kilikopwa nini, kimeenda wapi, thamani yake nini, uhalisi wa miradi inayotekelezwa na thamani tuliyoambiwa iwekwe mezani ili tuige mfano mzuri uliofanywa na Rais Samia. 1.3 Trilioni imewekwa mezani kila mtu anajua, hizi zingine za kibiashara tuende tukague na sisi ndiyo walipaji kwa sababu sisi ni wawakilishi wa wale waliotutuma hapa, hili la kwanza la Deni la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kilimo. Tunasema huu mpango unatupeleka kwenda kujenga uchumi wa ushindani na shirikishi. Sasa nilitegemea kama kweli tunasema shirikishi nguvu kubwa ingepelekwa kwenye sekta ambayo inakusanya watu wengi haya maneno yangekuwa na uhalisia, hali ilivyo haya maneno hayana uhalisia na mimi ni maombi yangu kwa Serikali mtakapoleta mpango na Bunge hili wengi wameletwa humu na wakulima tukipitisha mpango ambao hauna nguvu kubwa kwenye kilimo tutakuwa tunawasaliti waliotuleta hapa na hili jambo siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kinachangia asilimia 26 ya GDP yetu, lakini zaidi ya asilimia 70 au 80 ya Watanzania wameajiriwa kwenye Kilimo. Asilimia 100 chakula nchi, tunategemea kilimo; viwanda na maeneo mengine yote yanategemea kilimo. Sasa kama hali ni hii; ukiangalia miradi yote ya kielelezo, nitajieni mradi mmoja wa kielelezo ambao unashughulika moja kwa moja na kilimo, hakuna. Sasa kama hatushughuliki na kilimo, tunashughulika na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013/2014 mlishafikia mahali tulikuwa tunatenga mpaka shilingi bilioni 200 kupeleka kwenye kilimo kama fedha za maendeleo. Leo bajeti hii tunayomaliza, tumetenga shilingi bilioni 80. Sasa badala ya kwenda juu, tunarudi chini, hii siyo sawa. Sasa mapendekezo; najua muda wangu unakimbia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba Serikali ilete mpango na bajeti inayojiungamanisha na walio wengi kwenye sekta yao. Tuanzie mahali rahisi sana; Ilani ya Uchaguzi inasema tunatakiwa mpaka 2025 tuwe na hekta 1,200,000 za umwagiliaji. Tuna 600,000. Mimi nilitegemea kwenye Mpango walau hata hekta 150,000 au 200,000 ingeonekana kama ndiyo mradi wa kielelezo wa kugusa walio wengi. Sasa ninyi hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siipingi miradi hiyo, lakini ni kweli inagusa walio wengi masikini katika nchi hii? Hapana. Inawezekana inasaidia kwa pembeni, lakini hebu tubadilishe mwelekeo. Mwalimu Nyerere alituambia maendeleo ni ya watu, hata kama tutabishana. Kwa hiyo, pendekezo langu la kwanza, mtakapoleta Mpango, njooni na namna ya kupata fedha za kuweka walau hekta 200,000 au 150,000 ili tuanze hatua ya kufikia hiyo 1,200,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, tumezungumza sana hapa suala la kuwa na mfuko wa kusaidia, au mfuko wa ruzuku kwenye mazao. Dunia ikitikisika sisi wote tunayumba, kwa nini? Hatuna fedha ya kusaidia ruzuku kwenye mazao. Nilitegemea Mpango huu ungekuja na suala la Mfuko wa Ruzuku kwa mazoa yetu kama moja ya miradi elekezi ili tutoke hapa tulipo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)