Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye haya mapendekezo yaliyoletwa ya Mpango wa Serikali wa Miradi itakayotekelezwa mwaka unaokuwa wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, naomba nitoe shukrani za pekee kwa niaba ya wananchi wa Longido, kwa ile ziara ya Rais aliyokuja Longido. Imeongeza hamasa kubwa sana, wananchi wamejenga imani kubwa na kiongozi wao na pia kauli alizoziacha pale zimeacha hamasa kubwa na kuwafanya wananchi wa Longido wajue kwamba Rais wao anawapenda, anawajali; na hasa alipokuja kuwakabidhi ile miradi miwili; mradi wa majisafi na salama kutoka Kilimanjaro shilingi bilioni 15 za Serikali zimeleta maji kwenye Tarafa ya Longido karibu yote inakwenda kufikiwa. Ukisikia naongea habari ya shida ya maji, ni kwa sababu wilaya ni kubwa na Tarafa tatu zilizosalia bado zina shida kubwa ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye kile Kiwanda cha Nyama, alipotambua kwamba kuna kero ya tozo, ameacha maagizo kwamba zifanyiwe kazi ili viwanda vyetu viweze kuzalisha kwa tija na wafugaji nao waweze kupata mapato mazuri. Namshukuru sana Rais, nampongeza na Waziri wa Fedha na timu yake yote kwa kazi nzuri waliyoileta mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujikita zaidi katika eneo moja tu katika mchango wangu; eneo la sekta ya mifugo. Kabla sijaingia katika hiyo hoja, naomba nitoe angalizo katika moja ya maeneo ya vipaumbele vya huu mpango kwenye miradi yetu ya kimkakati. Nimekuwa nikifuatilia huu Mkutano wa Mabadiliko ya Tabia Nchi unaoendelea kule Scotland, gazeti la The Times la Marekani nadhani kama siku mbili zilizopita, liliandika article iliyosema kwamba, kuna Mataifa 18 na baadhi ya Mabenki na Taasisi wanakwenda kutengeneza deal la kufanya mchakato wa kusitisha matumizi ya nishati inayotokana na makaa ya mawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ikanifanya nifikirie kuhusu moja ya miradi yetu ya kimkakati hapa nchini ambao ni Mradi wa Mchuchuma na Liganga. Nikasema kwamba basi nitashauri katika kuratibu hii miradi ya kimkakati, basi tuangalie namna ya kuwekeza katika miradi ambayo itakuwa na uendelevu mkubwa na sina shida kama huu mradi wa makaa ya mawe utakuwa viable kwa muda gani, lakini ni vizuri kutathmini. Tusije tukawekeza fedha nyingi katika mradi ambao labda miaka mitatu au minne ijayo dunia itasema makaa ya mawe hayatakiwi tena kwa sababu yanachafua hali ya hewa ,ni moja ya polluter kubwa ambayo inayoleta shida ya mabadiliko ya tabia nchi kwa maana inatoa sumu nyingi inayoingia angani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema kwamba basi nishauri tu kwamba katika tu kwamba katika kupanga, mwangalie hilo suala kwa makini, tujue jinsi ya kuiendea hiyo miradi ya kimkakati kwa upande wa makaa ya mawe na ninafahamu pia pale kuna madini ya chuma. Kwa hiyo, pengine tunaweza kuongeza mtaji mkubwa katika kuvuna chuma badala ya kuhangaikia makaa ya mawe.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kiruswa pale nchi jirani Kenya, nadhani Lamu, hivi sasa wanajenga kiwanda kikubwa kitakachotumia Makaa ya Mawe ambacho kitazalisha karibu nusu ya umeme unaohitajika Kenya. Hivi sasa, they are doing it. Hata hivyo, point yako noted. Haya mambo ya dunia wanasema tu, lakini sisi tupo sahihi.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nilitoa tu concern ya kitu nilicho-observe kwamba isije ikatokea ikafika mahali…

MWENYEKITI: Wala, hiyo itawafuata wao, lakini sisi tusonge mbele.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hii Sekta ya Mifugo, pia nimeangalia kutokana na uzoefu ambao sasa tunao nikaona kwamba sekta ya mifugo haikui kwa kasi inayostahili na nikaona pengine kuna jambo ambalo lingeweza kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu Mpango uzingatie katika hilo ili na yenyewe iweze kunyanyuka ichangie katika uchumi wa Taifa kwa zaidi ya hii asilimia saba ambayo tunayo sasa hivi, iwepo na kilimo ni asilimia 26, nikasema basi ungeanzishwa Wakala wa Uendelezaji wa Miundombinu ya Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakala huu hautakuwa tofauti na Mawakala wengine ambao tayari tunao. Kwa mfano, tuna REA na mnajua mapinduzi ambayo wimeleta katika nchi yetu katika kusambaza umeme. Tuna Wakala mwingine wa TARURA, mnajua pia kwa kiasi gani imefungua barabara katika nchi yetu. Tunayo RUWASA, tunao umwagiliaji; wameleta mapinduzi makubwa katika sekta ambazo wamesimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na Wakala wa Mifugo ambayo itaenda kusimamima, kutengeneza mifuko kama ilivyo katika haya Mawakala mengine, mifuko ambayo itatusaidia sasa kunyanyua Sekta ya Mifugo na kusimamia miundombinu mingi. Naomba nikutajie baadhi ya miundombinu ambayo huu Wakala ungeweze kusimamia kama utaanzishwa. Kuna majosho ya kuogesha mifugo, kuna mengine yamekufa tangu zamani, kumbe wakala ukiwekwa in place itatusaidia sana. Kuna mabwawa na visima vya kunyweshea mifugo, tuna masoko ya mifugo ya awali, ya upili na ile masoko ya mipakani; kuna machinjio, kuna vituo vya kukusanyia maziwa, kuna miundombinu ya usafirishaji wa mifugo na bidhaa zake. Kama kwenye minada, utakuta minada mingi haina ramp ile ya kupakilia na kupakua mifugo. Nyingine, tunahitaji hata kwenda zaidi katika mazao yanayouzwa nje. Kwa hiyo, kuna code chain inayoangalia mazao ya mifugo kule bandarini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengine ambayo sasa hivi nchi ina-focus katika kuanzisha industrial packs. Tungekuwa pia na eneo la industrial packs kwa ajili ya mazao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Hiyo ni kengele ya pili Mheshimiwa Kiruswa.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi wakala huo uanzishwe, nami naungana na wenzangu katika kusema kwamba Sekta ya Uzalishaji Kilimo na Mifugo ipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)