Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia mpango huu. Nianze moja kwa moja kwa kuishukuru sana Serikali, kuanzia Rais wetu, Mheshimiwa Waziri Mkuu na viongozi wote kwa miradi mingi ambayo imeelekezwa kwenye Jimbo la Ludewa. Wananchi wa Ludewa walikuwa wanaliwa sana na mamba Mto Ruhuhu, hawakuwa na daraja, wamelilia kwa miaka sita, nashukuru sana, sasa daraja lile limekamilika na wananchi wanaweza kufanya shughuli zao na hawaliwi tena na mamba. Kwa hiyo, naishukuru sana Serikali, ni jambo ambalo limewafurahisha sana wananchi wa Ludewa na wameahidi kuiunga mkono Serikali kwa nguvu zao zote na uwezo wao wote aliowajaalia Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa daraja lile limekamilika, kwa hiyo, wanaomba pia ile meli ambayo inapita Ziwa Nyasa kuanzia Itungi kwenda Nyasa nayo iweze kuanza safari zake. Kwa sababu kwa muda wa miezi mitano sasa, toka mwezi Mei, ilikuwa matengenezo na wananchi wanatumia usafiri wa mitumbwi na maboti; hivyo, wengi wanazama kwenye maji na kupoteza mali zao. Kwa hiyo, wanaiomba sana Serikali, huu uchumi ambao tumesema umekua kwa asilimia 4.8 na robo hii 4.7 nao wanatamani kufanya shughuli ili uchumi wao uweze kukua. Kwa hiyo wanaiomba sana Serikali meli ile ianze safari zake mara moja, maana katika Ziwa Nyasa, Wilaya ya Ludewa ina kata nane; kuna kata ya Kilondo, Lumbila, Lifuma, Makonde, Lupingu, Iwela, Manda na Ruhuhu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kata zote hizi nane zinategemea sana usafiri wa maji kwa sababu maeneo haya yana changamoto sana za barabara. Kwa hiyo, jambo hili linarudisha nyuma jitihada za wananchi katika kujishughulisha na uchumi ili nao waweze kuongeza kipato chao na kulipa kodi ili uchumi wa nchi yetu uweze kukua zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, upande wa sekta ya kilimo kuna changamoto moja kwamba hizi sheria zetu nyingine zimekuwa kama zinadidimiza wananchi. Kuna Sheria ya Matumizi ya Rasilimali za Maji; Sheria Na. 11 ya Mwaka 2009. Sheria hii imeanzisha utaratibu kuwa, mtu yeyote anayetaka kutumia maji, anatakiwa apate kibali ambalo siyo tatizo; lakini sambamba na kibali hicho, kuna tozo ambazo zimeanzishwa. Sasa wananchi wa Mkoa wa Njombe na hasa Ludewa Kata ile ya Madilu na Madope wanalima sana viazi vya umwagiliaji. Sasa sheria hii inawarudisha wananchi kwenye kilimo cha kutegemea mvua, kwa sababu mwananchi ananunua ma-roll yale ya mabomba, anatafuta maji, anachimba mtaro, anaingia gharama kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inamwanzishia kodi ya shilingi 250,000 na gunia moja la viazi unakuta linauzwa shilingi 12,000. Kwa hiyo, ili upate hizo 250,000 unahitaji siyo chini ya gunia 23. Kwa hiyo, tozo hii naiomba sana Serikali, kwani inakuwa inawarudisha wakulima kwenye kutegemea kilimo cha mvua. Hii iko sana maeneo ambayo yana miradi ile ya umeme wa maji. Hizi jumuiya na haya mabonde yanakwenda kutoa elimu, yanaanzisha jumuiya za watumia maji. Kule kwangu wananchi wanalia sana na hii tozo ya shilingi 250,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kwenye sekta hiyo hiyo ya kilimo, Wabunge wengi wamezungumzia changamoto ya mbolea. Nitatoa mfano wa bei chache ambazo ziko kwa Njombe. Mbolea aina ya DAP ilikuwa inauzwa shilingi 55,000 mwaka 2020, lakini sasa hivi inakwenda kwa shilingi 97,000 mpaka shilingi 106,000; na hii mbolea ni muhimu sana kutokana na virutubisho ambavyo vinahitajika kwenye udongo. Kwa hiyo, kuna mbolea nyingine ambayo ni muhimu ya UREA, nayo imetoka kwenye shilingi 55,000 mpaka shilingi 80,000 au shilingi 90,000. Kwa hiyo, imepanda karibia mara mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mbolea nyingine ambayo inahitajika zaidi aina ya CAN, nayo kwa sasa inauzwa kati ya shilingi 60,000 mpaka shilingi 72,000 kwa Mkoa wa Njombe. Kwa hiyo, kwa hali hii, niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba Serikali ina kila sababu ya kutoa ruzuku kwenye mbolea ili bei iweze kushuka irejee kwenye hali yake ya mwaka 2020 au pungufu zaidi ili wakulima waweze kulima mazao yao kama kawaida, kwa sababu imekuwa ni kilio kikubwa sana. Kwa hiyo, naomba Serikali ichukulie katika uzito wa pekee ili tuweze kumnusuru huyu mkulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwenye sekta hii ya kilimo, naishukuru sana Serikali ilitoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa mahindi. Bahati mbaya sana mfumo uliotumika mwaka huu wa kutumia vikundi vya ushirika umewaumiza sana wale wakulima wenye gunia tano, sita saba au 15, wengi hawajauza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda Kijiji kimoja cha Mkongobaki kufanya mkutano, nikajaribu kuuliza pale wakulima mmoja mmoja ambao waliweza kuuza mahindi. Kwa kweli katika Kata ile ya Mkongobaki nilipata mwananchi mmoja tu. Kwa hiyo, zile tani nyingi hazieleweki zilikwenda wapi? Wakulima wanalia mahindi yanaoza, sasa hivi watoto wanaripoti Vyuo Vikuu, masomo ya mahindi hakuna. Kwa hiyo naomba hapa napo paangaliwe mfumo ule, ama tungeweza kuwaandaa wananchi kwa kuwapa elimu ya kutosha au tungetumia mfumo wa soko la miaka yote, tusingepitia kwenye hivi vikundi. Kwa Ludewa, wananchi; mkulima mmoja mmoja wameumia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niishukuru Serikali kwenye miradi ya umeme. Miradi ya umeme kwa kweli vijana wa kileo wanasema Serikali imeupiga mwingi sana. Kule kwangu Ludewa kuna vijiji ambavyo havina umeme kabisa ambavyo ni vitatu. Naomba Serikali iweze kuviingiza kwa wakandarasi hawa REA. Kuna Kijiji cha Ndoa, Kijiji cha Kimata na Kijiji cha Kitewele. Vijiji hivi havijaingia kwenye Mpango ili wananchi hawa nao waweze kuona wananufaika na uchumi huu ambao uko chini ya Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan ambaye ameelekeza fedha nyingi kwenye Mpango huu kwa ajili ya miradi ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halikadhalika, kuna hii miradi ambayo ya umeme ya wazalishaji binafsi. Kuna Kampuni ya Madope, inazalisha umeme kwa ajili ya vijiji 20. Kwa hiyo, umeme huu umekuwa na changamoto ya mgao wa masaa zaidi ya 12 kwa muda wa miaka miwili sasa. Naishukuru Serikali na Waziri wa Nishati, Bodi ya REA imekwenda kule na wameona changamoto hizi.

Kwa hiyo, tulikuwa tunaomba ile tathmini waliyoifanya ya kutatua hizi changamoto ziende haraka ili Kata ya Mlangali, Lubonde, Madilu, Madope, Lupanga na Lugarawa waweze kupata umeme wa uhakika na wa bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye kipengele cha uchumi shindani na hii miradi vielelezo, kuna huu mradi wa Mchuchuma na Liganga, nashukuru sana Mheshimiwa Rais alishatolea maelekezo kwamba miradi hii ianze, amechoka sana kuisikia; na ninafikiri ametambua kwamba miradi hii itatoa ajira nyingi sana. Ajira za moja kwa moja zaidi ya milioni nane pale zitapatikana. Wale wote watalipa kodi Serikalini, Serikali itaongeza mapato nao watapata kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hoja unayoizungumza ya mabilionea, sisi pale tuna makaa ya mawe ambapo leseni zake zote zimeshikiliwa na NDC halafu uchimbaji haufanyiki. Kwa hiyo, wangepewa wachimbaji wadogo, nina imani (namwona Mheshimiwa Biteko ananisikiliza vizuri) na sisi Ludewa tungezalisha mabilionea. Naomba wananchi wale waweze kulipwa fidia wakati Serikali inaendelea na majadiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, nakushukuru sana. (Makofi)