Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii niweze kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na Wabunge wenzangu kumshukuru Rais wetu, hasa kwa pesa ambayo imeletwa kwenye majimbo yetu. Wakati unatoa takwimu za wanafunzi ambao wako darasa la nne nikawa naangalia kwenye Wilaya yangu ya Muleba, tunao zaidi ya wanafunzi 19,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwaka huu kabla Mheshimiwa Rais hajasema neno lolote, tulikuwa tunajiuliza Muleba kule hivi tunafanya nini na watoto ambao wamemaliza darasa la saba. Tukawa tumeanza ujenzi wa vyumba vya madarasa. Nashukuru kwa pesa ambayo ametuletea sasa tunao uhakika kwamba vijana wetu wa darasa la saba watapata madarasa wote na tuendelee kumshukuru Rais wetu kwa kazi nzuri anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru Waziri wa Fedha na Mipango kwa hotuba yake. Pamoja na pongezi hizo, zaidi niwapongeze Kamati yetu ya Bajeti. Nimesoma maandiko yao yote na nipende kuwapongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza zaidi kwenye sekta ambazo zinachochea uchumi katika majimbo yetu, hasa sisi tunaotoka vijijini. Mimi naomba nitoe ushauri wangu; kwa vipaumbele ambavyo napendekeza kwenye bajeti ijayo naomba tuangalie sekta ya kilimo, tuangalie sekta ya mifugo, tuangalie sekta ya uvuvi na usafirishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamechangia sekta ya kilimo na wengi wamesema inachukua zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania ambao ni karibia milioni 22 ya Watanzania, wanajihusisha na masuala ya kilimo. Na tumeona mchango wa sekta ya kilimo kwenye uchumi wetu. Lakini ukiangalia bajeti ambayo tunaipatia kilimo, nadhani hatukitendei haki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti imependekeza kwamba bajeti tuliyonayo ya mwaka huu tuiongeze mpaka ifike zaidi ya bilioni 400. Kama tunataka kutoka hapa tulipo, sikubaliani na mapendekezo ya Kamati ya Bajeti, mimi napendekeza twende zaidi ya trilioni moja kwenye sekta ya kilimo ili tuweze kunusuru uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia uzalishaji wa mazao mengi per hector, mazao mengi tunazalisha chini ya kiwango kwa sababu hatujawekeza vya kutosha kwenye sekta ya kilimo. Ukiangalia mpango wa miaka mitano ambao tulijadili hapa mwaka jana tulikubaliana kwamba tunakwenda kuongeza eneo la umwagiliaji kutoka ekari 500,600 kwenda milioni moja na laki mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia tulipo leo, tuna miaka mitatu kufikia mwaka 2025 ambako ndiyo target yetu, bado tunaekari 569,000 lakini lengo letu ni kufikia ekari milioni moja na laki mbili, kwa miaka mitatu iliyobaki tunakwenda kufanya muujiza gani ili tuweze kufikia hilo lengo letu. Tusipoongeza bajeti ya kilimo tutabaki tunaimba wimbo uleule, tutabakia hapohapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia uzalishaji kwa mfano wa mafuta ya kula. Mpaka leo tunapoongea ni aibu kwa nchi hii ambayo tunasema wakulima ni zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wote, bado tunaagiza mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Naomba kwenye mpango huu Waziri wa Fedha atupatie mkakati wa nchi ili kuinusuru nchi hii kutokana na kuagiza mafuta kutoka nje wakati tunalima na wakati nchi hii tunasema ni nchi ya wakulima na ni nchi ya wafanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya mikoa wamekuja na mazao mapya. Kwa mfano Kagera kule tuna mazao mapya ya vanilla, kwa mfano. Wakulima wamejitahidi wanalima lakini hatuna masoko. Na Wabunge wengi hapa wamesema tunapowekeza kwenye kilimo tuhakikishe kwamba tunawekeza kwenye utafiti, tunawekeza kwenye kutafuta masoko tusije tukatumbukia kwenye janga ambalo tulinaswa nalo hapa juzi wakati tunahangaika kutafuta pesa ya kununua mahindi kutoka kwa wakulima. Naomba tunapohamasisha wakulima wetu wazalishe kwa wingi na Serikali ihakikishe kwamba inatafuta masoko kwa ajili ya mazao ya wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya uvuvi; mwaka jana wakati nachangia hapa nilisema nchi yetu imebahatika kuwa na maziwa na bahari, lakini ukiangalia mchango unaotokana na mazao ya uvuvi na yenyewe bado ni aibu. Ni aibu kwa nchi kama Tanzania tunapoagiza samaki kutoka nje ya nchi kwa kutumia pesa ya nje ni aibu kwetu. Naomba atakapokuja Mheshimiwa Waziri kwenye mpango tutakaokwenda kutunga sasa kutengeneza bajeti, atuambie tuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba sekta ya uvuvi na mazao ya uvuvi yanachangia kwenye pato la Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliongea mwaka jana hapa, na ninaomba nirudie niliyoyasema; tumejifunga na kanuni na sheria ambazo zinarudisha uchumi wetu nyuma. Ukiangalia tozo tulizonazo kwenye sekta ya uvuvi, ukilinganisha Tanzania na nchi jirani, hasa zile tatu ambazo tuna-share Ziwa Victoria kwa mfano, kodi zetu hazikubaliki na hazibebeki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache tu, ukiangalia tozo ambazo sisi Tanzania tunatoza na wenzetu, majirani zetu, kwa mfano ukiangalia VAT Tanzania tozo yetu ni shilingi 552 wakati jirani yetu Uganda anatoza 115, mwenzetu Kenya anatoza shilingi 34. Matokeo yake ni nini; mazao mengi ya uvuvi yamekuwa yakielekezwa upande wa pili na sisi tumekuwa tukikosa kazi, na hasa vijana wetu ambao wame- invest kwenye sekta ya uvuvi hawawezi kufanya kazi kwa sababu hawawezi kushindana na wenzao ambao wako nchi jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata viwanda vya kuchakata minofu ya samaki. Miaka ya nyuma Tanzania tulikuwa na viwanda vingi lakini kutokana na hizi sheria tulizojiwekea, tozo, sheria mbalimbali, vibali na nini, viwanda vyote vimehamia nchi za jirani, tumebaki na viwanda vichache hapa. Ni lazima tujiulize tumejikwaa wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunapoongea tumebaki na takribani viwanda nane. Uganda wana viwanda zaidi ya 20, Kenya wana zaidi ya viwanda vitano, na vyote vimehama vimekimbia kutoka hapa kwa sababu ya mfumo tulionao wa biashara, mfumo wa tozo na mfumo wa sheria tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najiuliza kwa nini mpaka leo tunapoongea unapotaka kusafirisha mazao ya uvuvi lazima yasafirishwe kupitia Viwanja vya Ndege vya Entebbe na Viwanja vya Jomo Kenyatta, Kenya, mazao ya uvuvi yanayotokea Tanzania. Tuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba sasa badala ya kusafirisha kwenda Entebbe na Nairobi, kwa nini tusitumie Viwanja vyetu vya Mwanza, Dar es Salaam au KIA? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Mwanza tumejenga facility kwa pesa ya walipa kodi, facility nzuri hata inazidi Jomo Kenyatta International Airport, lakini hatuitumii. Na sote tuko hapa tumekaa hatujishughulishi na hatujiulizi kwa nini hiyo facility ambayo tumeigharamia haitumiki. Na mwaka jana niliongekea hapa lakini tumemaliza tumerudi nyumbani, kila kitu kimeendelea business as usual. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tubadilike, kama tunataka kuingia kwenye soko la ushindani na kwenye mpango tumesema tunakwenda kujenga uchumi shindani na uchumi shirikishi, tunaujengaje kama hatuwezi ku-strain our minds tukafikiri nje ya boksi ile tuweze kunusuru nchi yetu na kuhakikisha kwamba hii sekta ya uvuvi ambayo tumebarikiwa, ni mali ya Watanzania, ili iweze kutusaidia kuchangia uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo kundi la vijana, sijaona kwenye mpango. Ukienda huko vijijini tunakundi la vijana ambao wakiamka asubuhi hawana kazi ya kufanya, mchana hawana kazi ya kufanya, mpaka jioni hawana kazi ya kufanya. Naomba kwenye mpango huu Serikali ije na mkakati hawa vijana tunawafanyaje.Vinginevyo tunatengeneza bomu ambalo miaka kumi, sihirini ijayo, litakuja kutulipukia wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima mpango uangalie kama ni mikopo ambayo tunaitoa kwenye halmashauri zetu ya kuwasaidia hawa vijana, hii asilimia nne ambayo tumejipangia haitoshi. Lazima tuangalie mkakati wa kuwanusuru hawa vijana na kwa kufanya hivyo tuweze kuwashirikisha kwenye uchumi wetu…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)