Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara hii ya Afya. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na mazingira magumu ya ufinyu wa bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na Wilaya yangu ya Mpwapwa. Wilaya ya Mpwapwa ina Hospitali ya Wilaya, lakini kuna upungufu mkubwa sana wa Madaktari na wafanyakazi wa kada nyingine. Mpwapwa kuna upungufu wa wafanyakazi 285 wa kada mbalimbali, ina Vituo vya Afya viwili, Rudi pamoja na Kibakwe. Kwa utaratibu wa Wizara ya Afya Kituo cha Afya lazima kuwe na Assistant Medical Officer kwa ajili ya kufanya minor surgeries, kama kuna complicated cases pale, lakini pale kuna Clinical Officer na Kibakwe kuna Clinical Officer. Kwa hiyo, naomba watupelekee Assistant Medical Officers katika Vituo hivi vya Afya Kibakwe pamoja na Rudi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mpwapwa ina Zahanati 50. Nusu ya Zahanati hizo zinahudumiwa na Medical Attendant. Nawapongeza Medical Attendants, wanafanya kazi vizuri, lakini ni kazi kubwa sana, kwa sababu mpango wa Wizara ya Afya ulikuwa ni ku-train Clinical Assistants wengi ili kuwasambaza kwenye zahanati, lakini huu mpango umeishia wapi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba anieleze mpango huo umeishia wapi ili zahanati nyingi ziwe na Clinical Assistant au Clinical Officers.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa madawa. Nimewahi kuwa Mjumbe wa Bodi ya MSD, tatizo siyo MSD, tatizo MSD haina fedha. Kwa hiyo, upungufu wa fedha, uhaba wa fedha MSD ndiyo maana wanakosa madawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali itenge fedha za kutosha. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, tumeona kwamba hapa mmetenga shilingi bilioni 65, lakini umetoa taarifa kwamba kuna shilingi bilioni 251 kwa ajili ya kulipa deni la MSD na vile vile kununua madawa. Naomba fedha zote zipelekwa MSD, zisipelekwe shilingi bilioni moja mwezi huu, mwezi ujao shilingi bilioni mbili, hapana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, MSD, Bodi yetu imewahi kutembelea Sudan Medical Store pamoja na Uganda Medical Store. Medical stores zao zinakuwa full funded na Serikali na wana Vote kabisa. Pesa inatoka Hazina, wanapelekewa Medical Store, lakini hapa imekua ni tatizo. Tumezungukia hospitali nyingi, hakuna madawa na tatizo la madawa wanasema labda MSD ndiyo hawasambazi madawa, lakini tatizo ni fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Waziri, Wabunge wengi wamechangia suala hili, nadhani sasa MSD itapata fedha za kutosha ili wanunue madawa na kusambaza hospitali zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nizungumzie ugonjwa wa kipindupindu. Limekuwa ni tatizo katika nchi yetu. Kipindupindu ni ugonjwa mbaya, unaua watu wengi, lakini ni ugonjwa wa kujitakia, wala siyo ugonjwa wa bahati mbaya. Kwa sababu nakumbuka zamani kulikuwa hakuna ugonjwa wa kipindupindu. Nimewahi kuwa Bwana Afya; ilikuwa ikitokea kesi moja ya ugonjwa wa kipindupindu au mgojwa mmoja, lazima iwe reported World Health Organization kwamba Tanzania kuna ugonjwa wa kipindupindu. Sasa imekuwa cholera is endemic in Tanzania, why?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze, zamani kulikuwa na Mabwana Afya. Kazi ya Bwana Afya ni kukagua usafi, unakwenda vijijini unakagua usafi; kila kaya iwe na choo, iwe na shimo la taka, iwe na kibanda cha kuweka vyombo ambavyo vimesafishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siku hizi Wizara ya Afya ni mfumo. Bwana Afya hafanyi kazi alizosomea, Bwana Afya anakuwa mratibu wa UKIMWI, Mratibu wa Malaria, Mratibu wa Chanjo. Mabwana Afya wafanye kazi walizosomea. Naomba sana Mheshimiwa Waziri; na zamani kulikuwa na utaratibu wa kupeleka kila Zahanati Health Assistant, mkafuta utaratibu huo, mkasema hapana, kuna upungufu mkubwa sana, labda uhaba wa fedha. Najiuliza, mbona Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wameweza? Kila Kijiji kina Bwana Shamba, kila Kijiji kina Bwana Mifugo. Kwa nini Wizara ya Afya ninyi mnashindwa kupeleka Mabwana Afya Wasaidizi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa kazi yao kubwa ni kukagua usafi kila Kijiji. Kila kijiji unakwenda unakagua usafi, haya magonjwa ya milipuko tungeyapunguza. Kinga ni bora kuliko tiba. Pale Muhimbili tulikuwa na Kitengo cha Elimu ya Afya kwa Umma (Health Education Unit), kazi yake ilikuwa ni ku-train Mabwana Afya wengi Wasaidizi na wanasambazwa wilaya zote kwa ajili ya kukagua usafi katika vijiji. Siku hizi sijui kama kitengo kipo; kama kipo labda Mheshimiwa Waziri anielimishe, kimeimarishwaje kitengo hicho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya afya kwa umma inasaidia sana. Lazima kwanza pale hospitalini wagonjwa wapewe elimu ya afya kabla ya kutibiwa. Outpatient health education. Tulikuwa na outpatient health education, individual health education na public health education. Kwa mfano Daktari anapomtibu mtu anayeharisha, Daktari anamwuliza kabisa kwa nini unaharisha? Anasema mimi naharisha kwa sababu labda sijui sikuchemsha maji au sina choo. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, public health education, lazima Mabwana Afya wasambae vijijini kutoa elimu ya afya, la sivyo kipindupindu kitatumaliza ndugu zangu. Naomba sana Wizara ya Afya itekeleze haya. Bwana Afya afanye kazi iliyokusudiwa na tu-train hawa Medical Attendant hao, au Clinical Assistants wengi kama ninavyosema. Upungufu wanao kama nilivyosema, MSD ni uhaba, kwa hiyo, ni vizuri MSD ikatengewa fedha za kutosha ili iweze kununua madawa mengi na kusambaza katika hospitali. Wananchi wengi wanapoteza maisha kwa sababu ya ukosefu wa madawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono kwa asilimia mia moja kwa mia moja.