Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. SILLO D. BARAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kidogo kwenye mapendekezo ya Mpango huu wa Taifa wa mwaka 2022/2023. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu, Mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanyia Taifa letu ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya ugonjwa huu wa Uviko ambao tumepata mkopo wa masharti nafuu wa shilingi trilioni 1.3 ambao umesaidia sana katika maendeleo yetu mbalimbali katika nchi yetu. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti pamoja na timu nzima ya Kamati ya Bajeti kwa kazi nzuri na ushauri ambao imetoa katika Mapendekezo ya Mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nakupongeze wewe Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Spika kwa kutuongoza vizuri sana katika Bunge letu Tukufu. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na timu nzima ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa ushirikiano mkubwa sana kwenye Kamati ya Bajeti pamoja na kuleta mapendekezo ya mwongozo huu wa Mpango wa Taifa wa mwaka 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia maeneo machache, moja ni upande wa kilimo. Amesema Mheshimiwa Ali King kwamba ukitemewa mate na wengi, utalowa. Kilimo chetu kinachangia asilimia 26.9 katika pato la Taifa. Pia kilimo kinaajiri Watanzania zaidi ya asilimia 66. Vile vile malighafi za viwandani zaidi ya asilimia 60 zinatoka kwenye sekta ya kilimo. Kama tunasema kilimo kinachangia asilimia 26.9 ya pato la Taifa, maana yake Watanzania zaidi ya asilimia 66 wanachangia asilimia 26 tu kwenye pato la Taifa. Kwa hiyo, maana yake, kwa kuwa kilimo kinaajiri Watanzania wengi zaidi, tulitarajia basi na mchango wa kwenye pato la Taifa ungekuwa mkubwa, siyo asilimia hii ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna haja kubwa sana ya Serikali kuwekeza kwenye sekta ya kilimo ili kuhakikisha kwamba inachangia vizuri kwenye pato la Taifa ambako pia itakuza uchumi, itakuza ajira na itaongeza wigo wa walipa kodi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, katika mapendekezo haya, namwomba sana Mheshimiwa Waziri katika Mapendekezo haya ya Mpango huu tunaouandaa, Serikali iwekeze vyema kabisa kwenye sekta ya kilimo. Ninaamini kabisa tutakwenda kuondoa Watanzania kwenye umasikini na pia na kufikia dira ya nchi yetu ya mwaka 2025. Kwa hiyo, naomba sana kwenye Mpango wazingatie sana sekta hii ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ni sekta ya afya. Naipongeza sana Serikali imewekeza kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, tumejenga vituo vya kutosha, kuna hospitali za Halmashauri pamoja na zahanati katika maeneo yetu, lakini kuna upungufu wa rasilimali watu watumishi wa afya zaidi ya asilimia 53. Tumejenga majengo najua Serikali italeta dawa lakini hatuna wataalam wa kutosha, upungufu wa asilimia zaidi 53 ni kubwa sana. Kwa hiyo niombe kwenye mpango huu tunaouandaa sasa Serikali iwekeze vizuri kwenye kuajiri wataalam wa afya katika maeneo haya ambayo tumejenga vituo vya afya pamoja na zahanati na hospitali za Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya maeneo ukienda unakuta zahanati ina nesi mmoja tu akiugua na huduma haitoki, kwa hiyo niiombe sana Serikali kwenye mapendekezo ya mpango huu sasa, iweke mkakati kabisa wa kuchambua na kuajiri hawa watoa huduma za afya katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ni sekta ndogo ya fedha. Unakumbuka mwaka 2018 Bunge lako Tukufu lilipitisha sheria pamoja na kanuni zake mwaka 2018 kuhusu sekta ndogo ya fedha, Kifungu cha 14 cha sheria hiyo kiliipa mamlaka Benki Kuu kukaimisha usimamzi wa mikopo kwenye maeneo yetu kwa Serikali za Mitaa na Kifungu cha 54 cha Sheria hiyo kinamlinda mkopaji, waheshimiwa Wabunge wenzangu mtakuwa mashahidi watu huko vijijini wanakopeshana, wafanyabiashara walio rasmi na wasio rasmi wanawakopesha walimu na wananchi wetu na kuwatoza riba kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki Kuu haijafanya vizuri kwenye eneo hili, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha isimamieni Benki Kuu sheria hii isimamiwe, sheria zinazotungwa na Bunge lako Tukufu zisimamiwe kama tunaona sheria haina manufaa kwa wakati huu tuifute, wananchi wanateseka hasa walimu na wakulima wetu kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuserma hayo nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha wazingatie maoni na ushauri wa Kamati, jana nilisema humu ndani kuna madini ya kutosha wasome wazingatie naamini kwamba watakuja na mpango mzuri sana na bajeti inayokuja ya mwaka 2022/2023 itakuwa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushkuru kwa nafasi hii naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)