Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mpango wa mwaka 2022/2023. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kunifanya siku ya leo tena nipate nafasi hii adimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu waliotangulia wamesema mengi wamesema mazuri na naungana nao. Sasa nichangie Mpango wa Mwongozo wa Taifa. Nimeusoma wote, nimesoma sura ya pili pale inapoelezea kwamba deni la Serikali limekuwa. Jana wakati Waziri anasoma hapa nimepata meseji nyingi sana kwa Watanzania wanahoji ni kwa nini deni limekuwa kutoka bilioni 564 mpaka bilioni 644 ambayo ni sawa na asilimia 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu tuko kwenye kipindi kigumu, wakati huu Watanzania wanatupima, tuko kwenye utekelezaji. Nimpongeze Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia, kiukweli anapambana sana, kweli kabisa yaani bila unafiki mama anapambana, isipokuwa niseme tu wazi maana huwa napenda kusema ukweli, mama anacheza peke yake kwenye uwanja, wasaidizi hawafanyi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu nimeshuhudia hii trilioni 1.3 jinsi ilivyoshuka vijijini kule kwenda kusaidia sekta mbalimbali kama vile afya pamoja na mambo mengine. Mwenzangu Mheshimiwa Tabasamu pale aliweka mfano wake, nami nataka nirudie tu maneno yake yale aliyoyasema, kuna hatari kubwa na hiki ni kipimo chetu cha kwanza sasa Wabunge kwenye maeneo yetu, hizi hela zinaenda kupigwa yaani inavyoonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza imeanza kuonekana mifano mingi mara cement imepanda, nondo zimepanda, yaani kila kitu kumekuwa na migogoro mingi, baada ya pesa kufika kwenye maeneo. Niiombe Serikali sasa iliangalie kwa macho manne, wananchi wanatupima, tukiangalia Ilani yetu yenye kurasa 303, wananchi walituamini kwa moyo mmoja kabisa na tuliahidi mambo mengi katika Ilani hii. Nashauri katika Mpango huu tuchukue vitu vichache tu ambavyo ni muhimu sana kwa wananchi wetu wale wa kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongelea suala la miundombinu za barabara mkoa hadi wilaya, bado hatujafanya lakini kwenye ilani humu wananchi tuliwaahidi. Ukiangalia kwenye mpango humu milolongo ni mingi, kuna ndege, service, mashirika yasiyo na mbele na nyuma, kwangu mimi naweza nikasema hivyo kwa uelewa wangu. Kwa wananchi wetu wale wapigakura waaminifu kuna vitu muhimu kama vitatu tu; miundombinu ya barabara, maji na afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiboresha hayo maeneo tunaweza tukathaminiwa sana na tukaonwa kweli kupitishwa kwetu, hata kuja humu ndani tutaonekana tunaisaidia Serikali kulikoni kuelekeza matrilioni kwenye masuala ya watu wachache, wanufaika wachache, hawa wengi ambao hawana uwezo wa kupanda hizi ndege wakaendelea kuteseka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hivyo kwa sababu nazunguka sana kwenye nchi hii. Majimbo mengi nazunguka, ukiangalia pamoja na kwamba tumezungumza kwamba tumetekeleza, lakini kuna sehemu nyingi ambazo bado hazijafanyiwa marekebisho. Hii inasababishwa na mifumo yetu ya manunuzi, maana pesa kweli mwanzoni tu hapa ilitoka milioni 500, lakini ukiangalia mpaka sasa hivi hizo fedha hazijafanya kazi, bado sijui process za manunuzi, mifumo mara imekataa na sasa hivi mvua zinanyesha, ina maana wananchi wanaona kabisa haya ni maneno tunayaongea ambayo hayatekelezeki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namshauri Mheshimiwa Waziri, yeye kweli ni mpambanaji na nimemwamini kuanzia kwenye tozo, pale alipokusanya bilioni 48 na akazisema hadharani na akazielekeza kwamba ziende zikajenge vituo vya afya nikamwamini kabisa kweli ana mapenzi mema, lakini kwa kuwa na yeye ni binadamu naomba anisikilize ushauri wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu iliyopita nilishauri hapa kwamba, kuna wenzetu Wenyeviti wa Vijiji pamoja na Vitongoji, hawa watu tumefanya nao kampeni kwenye uchaguzi, walikuwa wakitufungulia mikutano, tungewawekea hata kama ni shilingi 50,000 kwenye huu mpango na wao wajisikie vizuri, kuliko kuona deni linakua halafu wenzetu wanalala njaa, hawana hata shilingi 10,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine hapa, nimeona kwenye Mpango huu inazungumziwa kwamba maji yanatoka Ziwa Victoria kuja Dodoma. Nikiri tu wazi kwamba Kanda ya Ziwa bado tuna uhaba sana wa maji. Waziri wa Maji naomba hilo waliingize kwenye Mpango maana ni kelele kubwa ambapo mimi na Mheshimiwa Waziri tumewahi kupita Kanda ya Ziwa na kuwaaminisha watu kwamba litakuwepo hili mwaka 2022 na 2023, lakini kwenye mpango humu halimo na wananchi wanahitaji maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala la umeme, nimezunguka na aliyekuwa Waziri wa Nishati, tukawatangazia Watanzania kwamba umeme sasa unakuja tena tuliahidi mwezi huu ungekuwa umekamilika vijiji vyote, lakini mpaka sasa hivi bado sarakasi za kichina mpaka nazima simu kuonekana kwamba sina majibu ya kuwaeleza wananchi. Kwa hiyo Serikali ione umuhimu wa kupeleka umeme katika kila kijiji ambavyo vimebakia. Hii itaturahisishia sisi wanasiasa kuweza kuendelea kuwaongoza wananchi, maana tutakuwa tunatoa ahadi zile za kweli na zinafanikiwa kuliko kuwa tunapanga mipango elfu moja ambayo hatuiwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, kwa wachimbaji wadogo, niishukuru Wizara ya Madini mwezi wa Nne ilinipa mkoa wa kimadini na nimekusanya mpaka sasa hivi bilioni 6.49 kwenye Mkoa wangu wa Kimadini Mbogwe. Niwaombe tu wananchi wengine, Wabunge nimeona wamo wengi humu wawekezaji karibu kwenye Jimbo lile, tuje tushirikiane, lakini hii sekta inapaswa iangaliwe vizuri, maana kwenye Mpango huu haimo, haijawekewa kipaumbele kwamba Serikali itasaidiwaje kwenye huu mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachimbaji wadogo wanaingiza pesa nyingi na hawajawezeshwa na Serikali. Ukiangalia kuna mashirika Serikali huwa inayapa bajeti na ukiangalia zile hesabu hata ripoti za CAG hayafanyi vizuri, hao wachimbaji ambao wanachimba kwa nguvu yao Serikali ione umuhimu ya kuweza kuwasaidia watu hawa. Kwa mfano mimi hapa kama nimeingiza bilioni sita ni miezi mitatu tu, unaweza ukaona kwamba jinsi gani watu hawa waweze kusaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa wafanyabiashara; Taifa hili, na-declare interest nauza mafuta, ipo changamoto kubwa kwenye mafuta ya petrol na diesel. Mafuta yanapanda bei kila siku, Serikali ione sasa namna gani inaweza ikatenga bajeti ili kusudi mafuta yakishuka bei kila mwananchi atapata unafuu kupitia hii bidhaa ya mafuta. Jana EWURA imetangaza tena kupandisha bei, wananchi wanalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia wakati tunakuja mara ya kwanza Bungeni humu mafuta yalikuwa yanauzwa shilingi 1,900, lakini mpaka sasa hivi mafuta yanaelekea shilingi 2,500, vijijini ambako hakuna vituo mpaka shilingi 4,000, lita moja ya mafuta. Hii inaonekana kabisa kwamba mambo yanaenda vibaya kwenye Taifa letu na sisi Wabunge tunakuwa kama vile hatuyaelewi haya mambo wakati sisi naweza nikasema, ni maprofesa wa mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tuiombe Serikali, ina bandari yetu na Waziri wa Nishati ameteuliwa juzi nimshukuru, nilimwona juzi sijui Norway, sijui wapi, alikuwa na mzungu, naomba apambane usiku na mchana, wananchi tunamtegemea ili tuweze kupata unafuu kwenye bidhaa ya mafuta. Mafuta yakipungua bei nauli zitashuka bei. Mafuta haya haya pia ndio yameshikilia uchumi wa nchi. Ukiangalia kwenye bandari yetu pale tunapoingizia mizigo, nahisi kuna michezo ambayo inafanyika pale ndiyo maana mafuta yanakuwa na bei juu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri akidhibiti vizuri hapo tunaweza tukaishi vizuri sana na itaonekana kwamba tunamsaidia mama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, niwaombe Wabunge wote, unajua sisi ni wasaidizi wa mama na anatusaidia kweli kwenye Majimbo yetu, lakini nashangaa Wabunge hatusemi mazuri yale ambayo mama anayafanya. Alijitokeza mchana kweupe akachanjwa, sisi Wabunge wengine tunachanja kimya kimya kwa kujificha. Mama ametupa pesa za barabara, mama anatupa kila pesa anayoipata na anaitangaza hadharani za shule, zahanati na kadhalika. Tunakuwa na ugumu gani kusema mazuri ya mama pale tunapokuwa kwenye mikutano yetu. Kwa kweli niseme kabisa, kuna Wabunge nawaangalia tu, maana hawajui walitendalo, hawasemi kama mama kawatuma amewapa zile fedha wananyamaza tu.

MBUNGE FULANI: Kweli.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Sijui wanategemea nini mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kuna kila sababu hata tutakapomaliza hili Bunge, Wabunge wenzangu, tukiwa tunaifuatilia hii trilioni 1.3 tukamseme mama, maana hata juzi tumemwona akihutubia mataifa na kiukweli mama ni mpambanaji, siwezi nikalinganisha sijui ni mchezaji nani ambaye nilikuwa namjua, labda Messi, ila kila akipiga pasi hivi, wengine wanazubaa tu. Niwaombe Baraza la Mawaziri, kila Waziri ajitathimini kwamba ni kwa nini umepewa kiti hicho na ufikirie hapa Tanzania unafanya nini? Umepewa nafasi utembelee kwenye V8 au umsikilize Mama au ukamshauri na ulete mawazo mbadala ya kuweza kulibadilisha Taifa. Tofauti na hapo hizi nafasi tutaziomba na sisi, tunaziweza kabisa tena tunaziona ni kazi rahisi tu kuliko hata vitu vingine. (Makofi/ Kicheko)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Maganga, kengele ya pili imegonga.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nakushukuru sana. (Makofi/Kicheko)