Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipa. Nami nijumuike na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya. Tulimwona alipokuwa kwenye Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, tumemwona alipokuwa kwenye Mkutano wa Mazingira wa Mabadiliko ya Tabianchi huko Duniani na hotuba alizozitoa ambazo kwa kweli zilikuwa na mvuto mkubwa na msisimko mkubwa. Hakika analitendea haki Taifa lake na aendelee kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii kama ingekuwa tunafika mahali tunaweza tu kuwa kwenye mipango muda wote; na hata yale tunayoyazungumza wakati mwingine yasipate muda wa kufanyiwa kazi; tulizungumza mengi sana wakati tunapitisha bajeti ya mwaka huu. Nami naamini kama yale tuliyoyazungumza wakati huo kama kuishauri Serikali yangezingatiwa kwenye huu Mpango tuliowasilishiwa, leo hii tusingekuwa na maneno mengi hivi ya kusema. Hayo tuliyoyazungumza na ushauri wote tuliousema, hatuyaoni kwenye Mpango, sasa tutashauri mpaka lini ili tuweze kusikilizwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauri mengi sana kuhusu ajira za vijana wetu, zinapatikanaje? Tulishauri mengi sana kuhusu sekta binafsi, kuhusu mapato ya Serikali na kuhusu kuumaliza umasikini Tanzania. Vile vile ukipitia Mpango huoni ni wapi sasa ambapo maoni yetu yamezingatiwa. Nami nianze moja kwa moja na hili eneo la ugharamiaji wa Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Hotuba ya Mapendekezo ya Mpango wa Bajeti uliowasilishwa na Waziri, sehemu kubwa inazungumzia tu matumizi, lakini ni namna gani haya mapato tutayapata kwa ajili ya kugharamia Mpango wenyewe? Huoni wapi yameelezwa. Unaona jitihada tu zilizozungumzwa, tutahamasisha matumizi ya Tehama, tutahamasisha hiki, tutahamasisha hiki. Ni mambo ambayo yamekuwa yakirudiwa kila mwaka na ni ya ku-copy na ku-paste.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo changamoto kubwa sana kwenye ukusanyaji wa mapato ambazo zingeweza kufanyiwa utaratibu na tukatoka hapa tulipo. Kwa mfano, hivi ni utafiti gani tunaoufanya? Kila mwaka huwa tunafanya utafiti kweli? Kwa nini huu Mpango usituambie tunafanya utafiti gani kufikia ukusanyaji wa mapato yetu? Vyanzo vyetu vya mapato tunavifanyia utafiti? Hao TRA wanapofanya ukusanyaji wa mapato, tunawachunguza namna gani uwezo wao wa kuweza kukusanya mapato yetu na tunachukua hatua gani? Sasa unakuta mwisho wa siku mnaingia kwenye bajeti mnasema tu, hili limesamehewa, hiki kimetozwa, hii tozo tumeongeza; na mfano upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mwaka 2020 hapa kwa sababu ya sisi wenyewe kutokuwa na utafiti wa kutosha katika mapato yetu, tumekuwa tukiingia kwenye mgogoro mkubwa sana. Tumeingia kwenye mgogoro mkubwa kwenye tozo za simu. Tumebishana hapa, tukatoka tulivyotoka, tumefika mahali tumerekebisha wenyewe viwango vya tozo vya miamala ya simu vilivyokuwa vikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda na withholding tax tukawaambia watu kwamba tunataka kuweka withholding tax kwenye mazao ya 2%, halafu tukaenda kusamehe wanywa bia kwamba wasilipe kodi ili zao la shayiri liweze kuzaishwa. Wakati huo unamsamehe mnywa bia ili kilimo kiongezeke, halafu unaenda kumtoza anayelima shayiri yenyewe. Sasa unaenda kutoza withholding tax 2% huku ukijua kuna Service Levy 3%. Huyo mkulima atalimaje? Matokeo yake najua, watakuja kufanya marekebisho hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwenda kwenye mafuta, nako hivyo hivyo, tulisema yanaweza kua-attract inflation, hata kama tuna nia hiyo njema, Serikali imefanya marekebisho katikati ya safari. Hii yote ni uthibitisho kwamba tunaibuka na mabadiliko ya kodi bila ya kufanya utafiri wowote. Kwa nini hatufanyi utafiti? Kwa nini hatuwekezi? Kwa nini suala hili la mapato limekuwa la siri siri tu, halafu linakuja kuibuka hivi, hakuna mafanikio ambayo tunaweza kufika nayo popote? Hata hivyo Mpango hauzungumzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema hapa Wabunge, tunazo shilingi trilioni 360 zimeshikiliwa na Mahakama, uamuzi haujatoka. Nilitegemea kwenye Mpango hapa isemwe kwamba hizo shilingi trilioni zetu 360 ziko wapi? Leo hapa Bunge zima linapiga makofi kwa shilingi trilioni 1.3 tulizopewa na IMF. Fedha ndogo shilingi trilioni 1.3 tunapiga makofi mpaka mikono inauma; na kwa kweli tunashukuru kwa hilo, lakini tuna shilingi bilioni 360 za kwetu, hata kama ni asilimia 10 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 10 ya shilingi trilioni 360 ni shilingi trilioni 3.6. Bado hilo kwetu halijatuuma, Bunge halijaumia, Serikali haijaumia. Fedha zimeshikiliwa tu kwa maamuzi tu ya Mahakama. Kama tatizo ni hizo bodi zetu za rufaa za kodi zina shida na wataalamu, si tuajiri wataalamu hata wa kutoka mpaka nje kama ni wataalamu? Ni nini kinachosababisha? Mpango haujazungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la transfer pricing nalo tulilisema. Tunayo makampuni 504 yenye miamala zaidi ya shilingi trilioni 105 kwa mwaka. Uwezo wa TRA kuyakagua makampuni haya ni asilimia moja. Hawana wataalamu, hawana fedha na hawawezi kukagua na hivyo hatuwezi kupata kodi katika maeneo hayo. Fedha nyingi za Watanzania zinapotea, matrilioni ya fedha. Makampuni 504 unakagua asilimia moja kwa mwaka, unapata nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yote kwetu sisi, mipango yetu hatuoni kama ni shida, lakini tukiletewa hata shilingi bilioni tano hapa tunafurahi kweli kweli, lakini fedha zetu zimeshikiliwa na watu, hatupati hasira katika hili. Nilitegemea hata mikataba mibovu ya akina SICPA na TRA ingezungumzwa humu kwamba tunaenda kuifuta mara moja. Mikataba ya kinyonyaji ambayo inanyonya fedha za Watanzania tungeweza kuifuta tukapata mapato mengi tu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaye TR, anasimamia Mashirika ya Umma 237, makampuni haya yamekuwa mzigo mkubwa kwa Serikali, yanategemea ruzuku kutoka kwa Serikalini. Tumeshindwa kuyawezesha kuyapa fedha, hayana mtaji, yapo tu, hayatekelezi majukumu yake sawa sawa. Kwa nini Mpango hauzungumzi juu ya Mashirika yetu ya Umma, kuyapatia mtaji yaweze kufanya biashara tuweze kupata gawio kubwa la Serikali na hela tunazozipeleka kwa ajili ya ruzuku zifanye mambo mengine? Ila kwetu sisi tunaona hii ni sawa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu TR leo, Msajili wetu wa Hazina ana uwezo wa kuyasimamia makampuni haya kwa asilimia 13 tu. Hana fedha, hana wataalamu, lakini kwetu sisi tunaona kukaa na kupanga tu ni sawa, lakini upembuzi wa matatizo haya yanayotukabili hatuyafanyii kazi. Tatizo letu lipo wapi?

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Amos Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwa mchango wake mzuri kwamba, ni kweli Serikali mbali ya kutoa ruzuku, inashindwa kutoa mtaji kwa mashirika yake ili yaweze kufanya vizuri. Mfano Shirika la TTCL, linahitaji mtaji wa shilingi bilion 300 ili liweze ku-compete na Voda na Airtel, lakini mpaka sasa hivi wameshindwa na shirika haliko kwenye hali nzuri kama ilivyo mwanzo.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, unapokea taarifa hiyo?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea sana taarifa ya dada yangu na ninamkubali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna maeneo mengi, kuna utoroshaji mkubwa tu wa fedha, utoroshaji mkubwa sana. Ukienda mipakani mle madini yetu bado yanatoroshwa, mazao yetu ya uvuvi bado yanatoroshwa, mifugo yetu bado inatoroshwa, misitu na hata wanyamapori bado wanatoroshwa. Mpango unatueleza nini? Unaenda kudhibiti namna gani maeneo haya ili tuweze kupata mapato? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukuangalia hapa sasa hivi, tunazungumza kwenye Mpango huu, kwa mwaka unaokuja wa fedha, mapato yetu tunayotegemea kuongezeka ni shilingi trilioni 1.16 peke yake. Ila ukiangalia hiyo shilingi trilioni 1.1 wanaipata wapi? Hilo ongezeko wanalipata wapi? Wanaserma mapato yataongezeka kwa asilimia 7.6, lakini 7.6 wameipataje wakati uchumi utakua kwa 5.2%, mfumuko wa bei utaifikia kwenye 4%, tayari ni 9.2%, bado kuna kuongezeka kwa tozo, tunakuja na kodi mpya ambayo ni walau 1%, tunapata 10.2%, bado kuna uthibiti wa upotevu wa mapato kama huu atunaouzungumza. Kukishaweka mikakati kama hiyo, nayo kuna asilimia kama moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, unaweza ukakuta mapato yetu yakaweza kukua hata kwa 12%, kama tungekuwa tunafanya utafiti wa kutosha kuhusu mapato yetu; lakini hapa tunafika tu tunasema mapato yataongezeka kwa shilingi trilioni 1.2, halafu yanatokana na nini? Kwa hiyo, wakusanyaji nao wanaenda kiuzembe kukusanya, wanashindwa hata kushughulikia fedha hizi ambazo zipo, ni za kuchukua tu kwa sababu sisi Bunge tumewaidhinishia makadirio madogo. Sasa tutabaki hapa mpaka lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kuhusu ushiriki wa sekta binafsi. Hatuwezi kukua kama ushiriki wa sekta binafsi tunaenda nao namna hii na kama sekta binafsi itaendelea kudhulumiwa namna hii. Sekta binafasi, kwa mfano taarifa zetu za madeni, watu wa sekta binafasi walikuwa wanatudai shilingi trilioni 3.8 tulipoanza uhakiki mwaka 2015/2016, lakini ikaja kugundulika kwamba shilingi trilioni 1.16 ni malipo ambayo siyo halali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kuhusu ushiriki wa sekta binafsi. Hatuwezi kukua kama ushiriki wa sekta binafsi tunaenda nao namna hii, kama sekta binafsi itaendelea kudhulumiwa namna hii. Sekta binafsi ambapo kwa mfano taarifa zetu za madeni, watu wa sekta binafsi walikuwa wanatudai trilioni 3.8 tulipoanza uhakiki mwaka 2015/2016, ikaja kugundulika kwamba trilioni 1.16 ni malipo ambayo siyo halali. Kwa hiyo, karibia asilimia 30 ya malipo hayo siyo halali. Inayosema siyo halali ni Serikali siyo wananchi waliokopwa. Hii ni dhuluma kwa sababu wewe unakuja kuhakiki huku deni langu nilishakupa service, ukapata service hiyo halafu unakuja kusema hili deni asilimia 30 walioingia madeni hao ni akina nani, waliruhusiwa na nani na wamechukuliwa hatua gani waliodanganya hilo? Mnaenda kuwaadhibu hawa wananchi ambao ni haki yao, kumdhulumu mtu kwa fedha au kwa mali ulioichukua ni sawasawa na ujambazi mwingine tu. Kwanini, Serikali ijihusishe kwenye ujambazi wa namna hiyo? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mpina.