Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami nichangie maboresho ya Mpango wetu. Kwanza nianze kabisa kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais na Serikali. Katika hii ripoti, imeonesha kabisa kuwa utekelezaji wa bajeti zilizopita ulikuwa ni mzuri sana. Pia ni hivi juzi tu Mheshimiwa Rais ametupelekea zaidi ya shilingi trilioni 1.3 kwenye Halmashauri zetu. Hizo zimeleta mabadiliko makubwa sana kwa nchi yetu na hayo mabadiliko nafikiri yatakuwa endelevu kwa jinsi ninavyoyaona mambo yanakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hotuba yake ya juzi, alipokuwa kwenye mkutano. Ile hotuba imeniwezesha hata mimi kujaribu kuuangalia huu Mpango vizuri zaidi, na nikagundua kuwa huu Mpango wetu umeacha kipengele ambacho ni muhimu sana. Kilimo hakijawekwa kama ni kipaombele katika huu Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoongelea suala la tabia ya nchi, kilimo kinabeba kwa kiasi kikubwa hayo madhara ya tabia nchi. Dhima ya Mpango wetu tulionao ni kujenga uchumi shindani. Uchumi shindani unashindana na nani? Sasa ukiangalia huu Mpango wetu haujatuonesha kuwa huo ushindani wetu sisi tunashindana na nani? Nina imani ya kwamba sisi kama nchi, kama Tanzania, unapojenga uchumi shindani, unajilinganisha na wengine ambao tupo kwenye ukanda mmoja, kama East Africa, SADC au Afrika kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa sababu, nchi za wenzetu, kilimo wamekipa kipaombele sana. Uzalishaji kwenye kilimo ukiangalia nchi kama wenzetu Zambia, uzalishaji wa mahindi ni magunia 30 mpaka 40 kwa eka, ukilinganisha na sisi ni magunia ambayo hayazidi 10. Sasa unaona ni kiasi gani sisi hatujajijengea kilimo kikawa ushindani kwenye ukanda wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia mapato yanayotokana na zao la kahawa kwa wenzetu Waganda. Kwa mwaka 2020, wenzetu foreign exchange ya kahawa wamepata dola karibu milioni 515 ambayo ni karibu shilingi trilion 1.2; wakati sisi tulichopata hakizidi shilingi milioni 135, ambayo ni asilimia 30 au theluthi tu ya ile ya wenzetu wa Uganda. Sasa ukiangalia ungetegemea wapi tupate mapato mengi ya kigeni yanayotokana na kilimo cha kahawa? Kwa imani yangu, nafikiri sisi tungepata nyingi zaidi inawezekana hata mara mbili ya hizo. Ni kwa nini wenzetu wamepata fedha nyingi hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huhitaji hata elimu kubwa. Wanachokifanya wezetu, kwanza wamejenga ile chain ya uzalishaji. Kwenye production wamehakikisha kuwa wakulima wanapewa ruzuku (subsidy) kwenye mbolea na wakulima wanapewa malengo. Sasa hapa kwetu hiyo haipo. Naangalia hata kwa nchi ya Rwanda, nayo wameweka hivyo hivyo; kwenye kilimo kuna ruzuku kwenye mbolea, na wanzetu ruzuku yao ni zaidi ya nusu; asilimia mpaka 60, lakini sisi ruzuku hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitengeneza hesabu kwenye kilimo cha Watanzania, hakuna mkulima hata mmoja anayeweza kwenda na jembe shambani, kwa sababu hutakuwa na nguvu hiyo, hata kwa bei hizo zilizokuwepo. Mkulima wa kwetu, uwekezaji kwenye eka moja ya mbolea, atakachopata hata akawauzia NFRA, ni nusu tu ya ile gharama ya uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa naomba tunapoiangalia nchi kama Tanzania ambapo tegemeo kubwa ni kilimo, seriously kwenye mipango yetu tuangalie kilimo tutakisaidia namna gani ili tufanye kilimo cha kisasa, na huku ndiyo kutakuwa na mabilionea ambao Mheshimiwa Shangazi alikuwa anawaulizia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na wenzangu, kwa mwaka huu hivi sasa Serikali iagangalie namna gani itawapatia wakulima ruzuku ya mbolea na isisubiri Mpango. Leo hii kilimo kimeanza, lakini hakuna maandalizi yoyote ya kilimo. Pamoja na hali ya hewa kuwa mbaya, lakini wakulima wanaogopa kuandaa mashamba kwa sababu ya bei ya mbolea ambayo hakuna mtu atakayeweza kuimudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ombi langu, kwa hesabu ya haraka haraka, nilikuwa naona Serikali ikitenga (sijui itazipata wapi, nina imani itazipata), kama shilingi bilioni 200 mpaka 250 zinaweza kusaidia zikaiokoa nchi yetu ili janga la njaa litakalotokana na ukame mwakani tuweze kuzalisha kwa tija. Kwa hiyo, naomba pamoja na mwendelezo wa hii ruzuku, lakini tungeanzia sasa hivi na uharaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Spika kwa lile agizo aliloipa Serikali. Nafikiri lile ni agizo muhimu, naiomba Serikali iangalie kwa haraka sana ni namna gani iweze kuwasaidia wakulima. Hilo tamko lisichelewe, kwa sababu kwa ukanda kama ule ninaotoka mimi, sasa hivi watu ndio wanatafuta mbolea ya kupandia, na kwa bahati mbaya hata mbolea za kukuzia leo wanaoagiza mbolea nina imani ni pungufu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipojaribu kuuliza wakasema, wazalishaji wote sasa hivi hawawezi kuzalisha kwa sababu order zilizopo kwenye wazalishaji nje ya nchi, labda mwezi March au April next year, 2022. Sasa hiyo inaweza kutusababishia sisi, kama tulikuwa hatujajiandaa kwa hilo, hata hiyo mbolea ambayo tunaitegemea isiwepo. Hata hizi mbolea za kupandia nazo hazipo. Sasa hii yote inatokana na sababu kwamba katika mipango yetu kilimo hakijawekwa katika kipaumbele. Kwa hiyo, naomba Serikali katika huu Mpango, iweke kipaumbele cha kilimo ikiwezekana namba moja, ili tuweze kusaidia jamii yetu ya Watanzania ambao ni zaidi ya asilimia 60 wanaotegemea kilimo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)