Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niungane na wenzangu katika kuchangia hoja hii iliyopo mezani ya Azimio lililoletwa katika Bunge lako Tukufu la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu Afya ya Mimea, Afya ya Mifugo na Usalama wa Chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuzipongeza Wizara zote mbili ambazo zimetupa ushirikiano mkubwa katika kuchambua Azimio hili nikimaanisha Wizara ya Kilimo pamoja na Wizara ya Mifugo na Wizara nyingine ambazo wataalam wake walikuja tulipokuwa tunafanya uchambuzi wa Azimio hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wameshasema yote kuhusiana na faida za kuridhia Azimio hili, lakini pia nipende kusema kwamba kuna hasara tusiporidhia kwa sababu ni makubaliano ya Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Moja ya hasara ambayo tungepata tungeweza kutengwa, tungetengwa katika baadhi ya vipengele vya hii Itifaki kwamba kuna wakati tunataka kutetea maslahi ya mazao yetu haya, afya ya mimea, mifugo yetu, usalama wa chakula lakini wanaweza wakasema ninyi hamna haki ya kusema kwa sababu hamkuridhia hili Azimio. Hivyo ili twende pamoja kama tulivyokubali kuwa wanachama ni muhimu wote kama Bunge lako Tukufu turidhie leo Azimio hili ambalo tumeshalitafakari, tumeshalidadavua na tumejiridhisha kwamba kuna faida kubwa katika kuliunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na kutoa wito kwamba turidhie Azimio hili, napenda tu kutoa maoni na ushauri kwa Serikali, kwa sababu tumegundua katika kuchambua utekelezaji wa Azimio kwamba kuna maeneo ambayo tuna upungufu mkubwa. Moja ya maeneo ambayo kuna upungufu mkubwa katika kusimamia afya na usafi wa mazao yanayohusika ikiwemo kilimo au mazao ya mimea na mifugo na usalama wa chakula ni kwenye hii sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna vitendea kazi vingi vimeshatengenezwa nikimaanisha instrument za kusimamia utekelezaji wa Azimio hili lakini pia bado tumegundua kwamba mifumo ya kusimamia na uwezo wa Taasisi za Serikali husika zina upungufu. Hivyo napenda kuisihi Serikali iwekeze kwa dhati katika kujengea uwezo hizo taasisi ili tusije tukasaini ili Azimio tukadhani tumeshafaidika maana yake tutapigika kweli kweli kwani wenzetu walisaini siku nyingi na ina maana wamejipanga. Kwa hiyo, nasi tunatakiwa tujipange, tuwe na sera, tuwe na sheria, tuwe na kanuni, ambazo zitatuongoza katika kuhakikisha kwamba tunafaidika ipasavyo tunapokuwa katika Itifaki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende basi kujielekeza kwenye maoni na ushauri ambao ningependa niongezee pale ambapo Kamati imeishia kwa upande wa afya na usafi wa mifugo. Kwa kweli hii sekta ya mifugo ni moja ya sekta ambayo ukiachia kazi iliyoanza kufanywa na Serikali ya Awamu ya Tano na hii ya Sita ilikuwa ni kama imesahaulika. Ili basi tufaidike katika kuingia kwenye hii Itifaki ni vizuri na napendekeza kiundwe chombo mahsusi kama ilivyo katika Wizara ya Maliasili, wana chombo mahsusi, Mamlaka ya Hifadhi za Taifa, tuanzishe Mamlaka ya Uendelezaji wa Miundombinu ya Mifugo Tanzania au kwa Kiingereza tungeweza kusema Tanzania Livestock Infrastructure Development Agency ambayo itakwenda kusimamia mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ingeweza kusimamia masuala ya masoko ya ndani ya nje maana hatuuzi bidhaa yetu ipasavyo katika masoko ya nje kwa sababu havikidhi viwango. Ingesimamia masuala ya usafirishaji, masuala ya minada kuelekea sehemu za kupakia na kupakua mifugo, ingesimamia machinjio, ingesimamia suala la ngozi kwa sababu kuna ngozi nyingi zinatumwa siku hizi hakuna masoko, ingesimamia masuala ya magonjwa, masuala ya chanjo ya mifugo, ingesimamia masuala mbalimbali pamoja na usimamiaji wa nyanda za malisho, ingekaa na kutengeneza kanuni za kutenga maeneo mahsusi kwa ajili ya wafugaji. Nyanda za mifugo zingeweza kupimwa zingeweza kuwekewa miundombinu ya maji zingeweza kabisa kuwa gazetted kama National Park zilivyokuwa gazetted na tukawa na maeneo ambayo tungeita kwa lugha ya kigeni disease free zone.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Wilaya yangu ya Longido asilimia 95 ni wafugaji, ni mapori yasiyofaa kwa kilimo, ni maeneo ya wafugaji ambayo yangeweza hata kuchukuliwa yakafanywa model ya maeneo mahsusi ya kufuga mifugo na kunenepesha kwa ajili ya soko la Afrika Mashariki na nchi za nje. Kwa bahati nzuri tuna kiwanda kikubwa kile ambacho wawekezaji wamejenga, moja ya viwanda vikubwa sana hapa nchini vya kuchakata bidhaa za mifugo, lakini mpaka sasa hivi kina-operate under capacity kwa sababu hatujajipanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Itifaki itakapokuwa imeridhiwa na tukawa bado hatujaweza kuimarisha afya ya mifugo yetu tutaendelea kukosa masoko kwa sababu mifugo itakayopita ni ile ambayo imevuka vile viwango. Hii Itifaki ni ya viwango, the whole thing is about standards ya mazao ya mimea, mazao ya mifugo na usalama wa chakula chote tutakachokuwa tunazalisha Tanzania kitakuwa kinapitishwa kwenye hiyo mizania na tusipopita hakuna mahali tutakwenda kama Taifa hata baada ya kusaini Itifaki hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ningeshauri Taifa letu baada ya kuridhia hili Azimio, basi sasa tujifunge mikanda tufuatilie kwa makini dhana ya utekelezaji. Kila sekta, kila taasisi husika ikajengewe uwezo, tukawasomeshe wataalam wetu katika kila fani; mambo ya maabara, afya ya mimea, udongo, mambo haya ya magonjwa ya sumu kuvu yanayoshambulia mazao na kutukosesha soko na kuelimisha wananchi wetu jinsi ya kuzalisha, jinsi ya kuhakiki afya na kutafutia masoko ya ndani na ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, napenda kusema naunga mkono hoja hii iliyo mezani na nalisihi Bunge lako Tukufu liridhie ili tuweze kusonga mbele. Ahsante sana. (Makofi)