Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Kabla ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya na uzima wa kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuweza kuichangia hotuba ya Wizara ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kumpongeza sana Waziri wa Afya pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Ndani ya muda mfupi wameweza kutembelea mikoa mbalimbali na kuweza kutoa maelekezo mbalimbali, hali ambayo pia inawatia moyo hata watendaji wanaofanya kazi katika Sekta hii ya Afya. Hongereni sana na mwendelee kuchapa kazi hivyo hivyo na msimwangushe Mheshimiwa Rais. Nyie ni vijana na tunawategemea, mna nguvu pia mnao uwezo mkubwa sana, endeleeni kuchapa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia katika maeneo makuu matatu. Kwanza, namwomba Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, maeneo makuu matatu ambayo ni changamoto sana katika Sekta ya Afya; kwanza ni upatikanaji wa madawa na vifaa tiba; pili, ni suala la miundombinu ya kutolea huduma; na tatu, ni uchache wa watumishi katika Sekta ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la upatikanaji wa madawa na vifaa tiba ni imani yangu kwamba Wizara ikidhamiria, ikiweka fedha za kutosha, ni suala ambalo linaweza likatatuliwa hata ndani ya miezi sita. Ni suala la dhamira tu, Serikali ikiamua inaweza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija katika suala la miundombinu, sasa hivi pamoja na juhudi zote zinazofanyika, lakini katika baadhi ya maeneo, miundombinu iliyopo kwa kweli imechoka na pia imeelemewa kutokana na idadi ya watu inayoongezeka kila siku, mfano mzuri ni Muhimbili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni miongoni mwa wanaoiamini hospitali ile kuliko hospitali nyingine zote katika nchi yetu. Ukienda pale, idadi ya wagonjwa ukilinganisha na idadi ya wodi pamoja na vitanda kwa kweli inatia huruma. Unawahurumia hata Wauguzi na Madaktari. Wagonjwa wanalala chini kwa sababu wodi ni chache, hata ukiongeza vitanda hakuna eneo ambalo unaweza ukaweka. Ifike wakati sasa suala la ujenzi wa hospitali ya Mlonganzila kwa kweli lipewe kipaumbele kikubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunazo hospitali zetu za Kanda zipewe uwezo kwa maana ya Watendaji na vifaa ili ziweze kusaidia Muhimbili kupunguza mlundikano. Kwa upande wa kusini, Mikoa ya Mtwara na Lindi, tunayo Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini ambayo inajengwa pale Mikindani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia katika Bajeti yako Mheshimiwa Waziri, sijaona eneo lolote. Nimeangalia kwenye bajeti ya maendeleo, nimeona Hospitali ya Rufaa Mtwara shilingi bilioni mbili. Sasa sijui zile shilingi bilioni zinakwenda Ligula au zinakwenda Mikindani! Kwa sababu kama ni Mikindani, Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini, shilingi bilioni mbili kwa kweli hazitoshi, kwa sababu mpaka sasa hivi kilichojengwa pale ni majengo ya wagonjwa wa nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kweli tuisaidie Muhimbili ni lazima tuhakikishe zile Hospitali za Rufaa za Kanda zinajengwa na zinawezeshwa. Sasa hivi mgonjwa yeyote pale Ligula akishindikana, inabidi asafirishwe kwenda Muhimbili. Wakati mwingine Mheshimiwa unalazimika kama Mbunge kununua viti sita kwenye ndege ili mgonjwa mmoja tu aweze kusafirishwa. Afadhali ikiwa ATC, shilingi milioni unaweza ukasafirisha mgonjwa, lakini ukija kwenye Precision, mpaka shilingi milioni 15 kusafirisha mgonjwa mmoja. Kwa kweli kwa wale ambao hawana uwezo hawawezi; na wakati mwingine hata Mbunge huwezi kutoa shilingi milioni 15 kusafirisha mgonjwa mmoja. Tunaomba hospitali ile ijengwe na iweze kukamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwa upande wa watumishi, tuna vituo vya kutolea huduma zaidi ya 7,249 ukichanganya na sekta binafsi, lakini na mahitaji ya watumishi kwa upande wa Wauguzi ni zaidi ya 46,000 na waliopo ni kama 24,000. Tuna upungufu wa zaidi ya asilimia 49 ya watumishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika udahili wa watumishi wetu; nilikuwa naangalia, unakuta Madaktari kwa mwaka wanadahiliwa 1,670 wakati tuna upungufu wa Madaktari zaidi ya 4,000. Kwa upande wa Wauguzi, tuna upungufu wa Wauguzi zaidi ya 22,000, lakini wanaodahiliwa kwa mwaka ni kama 3,499. Hivi kweli tunaweza tukaondoa tatizo hili? Tulikuwa na tatizo la Wahasibu na tatizo la Walimu, Wizara mama zilikuwa zinatenga kiasi cha kutosha ili kuweza kuondoa matatizo haya. Sasa hivi tatizo la Walimu na Wahasibu ni kama limekwisha lakini kwa upande wa Sekta ya Afya, nawaomba wadogo zangu, Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Kigwangalla ni lazima tuje na mpango mahsusi, tupanue vyuo vyetu vya Wauguzi, Madaktari na kada zote za Sekta ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni lazima tuwalipie. Serikali itenge pesa kama ambavyo Wizara ya Fedha ilikuwa inatenga pesa kwa ajili ya Wahasibu; kama ambavyo Wizara ya Elimu na Wizara ya Kilimo zilikuwa zinatenga pesa kwa ajili ya kusomesha watumishi wao. Ni lazima Wizara ya Afya tufanye kama operation. Tunasema anayekwenda kuchukua degree ya Uuguzi atachukua mkopo, lakini wanaokwenda kuchukua Cheti, Diploma tunasema ajitegemee mwenyewe. Karo yenyewe ni zaidi ya shilingi milioni moja. Chakula kinazidi hata hiyo shilingi milioni moja. Kwa kweli kama tunataka kuondokana na upungufu huo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, ni lazima tuwe na mpango mahsusi na tuwekee kipaumbele, tutenge pesa za kutosha kuhakikisha tunadahili vijana wa kutosha hasa wale ambao tunawahitaji kule vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani kwa sisi tunaoishi vijijini, unakuta zahanati moja ina mtumishi mmoja, kule Muuguzi anafanya kazi masaa 24, hana Jumamosi, hana Jumapili; kukiwa na mgonjwa saa 5.00 za usiku anakwenda kuamshwa na sidhani kama kuna chochote wanachokipata. Ndiyo maana unakuta Wauguzi wetu wakati mwingine wanakuwa na lugha zisizostahili. Siyo kwamba wanapenda, ni uchovu wa kazi. Mzigo ni mkubwa wanaoufanya. Kwa hiyo, mtu mmoja halali, usiku kucha anaitwa kazini, asubuhi yuko kazini, Jumamosi yuko kazini, hivi unategemea awe na lugha nzuri? Wakati mwingine ni stress tu kutokana na uzito wa kazi ndiyo unaowafikisha wanakuwa na lugha wengine zisizostahili.
Kwa hiyo, kwa kweli lazima tuongeze udahili, hizi tunazosema kila kijiji kiwe na zahanati, kila kata iwe na kituo cha afya; bila kwenda sambamba na udahili, hizo zahanati na vituo vya afya zitakuwa ni nyumba tu za popo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nichangie, nirudi katika Mkoa wangu. Tunacho Kituo cha Afya cha Nanguruwe ambacho tulikiombea kuwa Hospitali ya Wilaya. Tumekamilisha karibu mahitaji yote yanayotakiwa. Tunayo majengo ya upasuaji, tunavyo vitanda vya kutosha, wodi za kutosha pamoja na Kituo cha Afya cha Nanyumbu; lakini mpaka sasa hivi bado tunasubiri kibali kutoka Wizarani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ummy alikwenda kutembelea Kituo cha Afya cha Nanguruwe, nina imani kabisa kwamba yeye mwenyewe amejiridhisha kwamba vipo vifaa vya kutosha na majengo ya kutosha. Tunaomba watoe kibali ili ianze kufanya kazi kama Hospitali ya Wilaya, tupunguzie mzigo hospitali ya Mkoa ya Ligula. Hii ikienda sambamba na hospitali au Kituo cha Afya cha Nanyumbu ambacho nacho kwa muda mrefu kimeshafikia mahitaji ambayo yanatakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Mtwara Vijijini tunavyo vituo vya afya vya Mahurunga na Kitere. Tumeshajenga vyumba vya upasuaji; vifaa vyote vipo kwa zaidi ya miaka miwili, lakini hakuna huduma inayotolewa pale, tatizo ni lile lile la uchache wa Madaktari. Nakuomba Mheshimiwa Waziri utuletee Madaktari wa kutosha ili vituo vile vianze kutoa huduma ya upasuaji na tuweze kupunguza vifo vya akinamama na watoto hasa wakati wa kujifungua. Pia Mheshimiwa Waziri, wakati unaoandaa hao Madaktari, tunao Madaktari pale Hospitali ya Mkoa ya Ligula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunalo tatizo katika Wilaya yetu na hata kwa mkoa wetu suala la Mabusha. Kwa vile katika vituo vile huduma zote zipo, vifaa vyote vipo, kwa nini hao Madaktari wasiwe wanapanga siku angalau kwa wiki au kwa mwezi wanakwenda katika Vituo vya Afya vile ambavyo vina huduma za upasuaji, wakawa wanatoa huduma ile kwa wale ambao wanahitaji kufanyiwa operation za mabusha? Kwa sababu sasa hivi wanalazimika kuja katika Hospitali ya Mkoa, tunawagharamia, anafika pale anakaa zaidi ya wiki mbili anasubiri zamu. Mara leo sijui tunafanyia wawili, kesho tunawafanyia watatu; kwa nini wale Madaktari walioko katika mkoa wasiwe wanazunguka na wanakwenda katika maeneo hayo kutoa huduma? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napendekeza kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake ni suala la uzazi wa mpango. Nimeangalia katika kitabu cha hotuba haraka haraka, sikuona eneo lolote lililozungumzia suala la uzazi wa mpango. Suala la idadi ya watu na uchumi wa nchi yetu ni muhimu sana. Maeneo mengine kama Wabunge tukienda kule wanatuambia bwana hizi huduma hatuzipati na wanazihitaji. Unakuta kule akinamama wengine tayari ana watoto 10 na uzazi wake ni wa matatizo, ni lazima ajifungulie katika hospitali ya Mkoa. Kwanini wasishauriwe uzazi wa mpango sahihi kwa ajili ya kuwawezesha na wenyewe kuboresha afya zao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wanapoteza maisha kwasababu tu kila baada ya mwaka mmoja ana mtoto au unakuta mtu tayari ameshajifungua kwa zaidi ya mara nane hali ambayo ni kihatarishi cha maisha yake kwa sababu kwa kweli baada ya kuzaa kwa zaidi ya mara nane, nadhani Mheshimiwa Kigwangalla, Naibu Waziri wa Afya ananielewa, ni kwamba kila kizazi kinachoongezeka pale ni hatari kwa maisha ya mama yule anayejifungua na hata mtoto anayejifungua. Ukiangalia vifo vingi vinavyotokana na uzazi ni aidha ni vya wale waliojifungua katika umri mdogo au kwenye umri uliopitiliza umri ule ambao kwa kweli mtu anaweza akajifungua salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusisitiza suala la Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini. Mheshimiwa Waziri akapokuja tungependa kusikia bajeti yake imetengwa wapi. Kama tunataka kupunguza vifo vya akinamama na watoto, tuangalie suala zima la magari ya wagonjwa. Siku za nyuma tulikuwa na magari ya wagonjwa, yana radio call ndani yake, kukiwa na tatizo wanaweza kuwasiliana kwa radio call na gari lolote lililoko karibu na eneo ambalo mgonjwa yupo linaweza likaenda kumchukua kwa haraka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza kwa Mheshimiwa Waziri kwamba sasa hivi tuwe na magari ya wagonjwa ambayo pia ni surgical. Mgonjwa anapofuatwa, basi afuatwe na Daktari na akifika siyo kwenda kumchukua na kumkimbiza zaidi ya kilometa mia moja Makao Makuu ya Wilaya au ya Mkoa kwa ajili ya upasuaji. Gari ikifika, aweze kufanyiwa upasuaji kule kule inakomkuta badala ya kuanza kukimbizana naye. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kujua hilo, kama tunao mpango wa kuwa na magari ya wagonjwa ambapo huduma za upasuaji zinaweza kupatikana humo humo ndani ya magari kama ambavyo nchi nyingine zinafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana.