Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kwanza kuchangia taarifa ya Kamati hii ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Spika, kwanza nitumie nafasi hii kukushukuru sana wewe kwa kuniamini na kuniteua kuwa kwenye Kamati hii ya Sheria Ndogo ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema kwenye utangulizi, kwa mujibu na mifumo ya nchi yetu, sheria ndogo ndio sheria ambazo zinagusa kwa kiasi kikubwa wananchi walio wengi kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, na nitumie nafasi hii kuipongeza sana Kamati ya Sheria Ndogo kwa kufanya kazi kubwa sana katika uchambuzi wa sheria hizi ambazo katika uchambuzi huo imebainika dhahiri kwamba kulikuwa na dosari muhimu za kurekebisha hasa kwenye kulinda tasnia ya sanaa, tasnia ya walimu, tasnia ya watu wa bodaboda na wananchi mbalimbali kwenye kilimo na kadhalika. Kwa hiyo, niwapongeze sana Kamati ya Sheria Ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kamati na ripoti ambayo imetolewa hapa ni dhahiri kwamba ziko changamoto mbalimbali hasa kwenye ushirikishwaji wa wananchi kwenye kutoa maoni kwenye sheria hizi ndogo. Sote tunajua kwamba katika nchi yetu yapo maeneo kadhaa kumekuwa na mvutano na wafanyabishara wadogo pamoja na watu wa bodaboda wakilalamikia baadhi ya sheria ambazo zimekuwa zikitungwa na mamlaka ambazo zinatunga sheria ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali na mamlaka ambazo zinahusika na utungaji wa sheria hizi ndogo ni vizuri sheria hizi kwa sababu walaji na waathirika wa sheria hizi ni wananchi wa kule chini, kabla ya sheria kuanza kutekelezwa ni muhimu sana wadau hawa wakasikilizwa na ndiyo maana kwenye ripoti ya Kamati imeabainika dhahiri kwamba kwenye Sheria ya Bodi ya Walimu kwa mfano walimu walikuwa na maoni yao ya msingi sana ya kuboresha Bodi ya Taaluma ya walimu. Lakini kwa sababu tu ya kutokushirikishwa vizuri na kutoa maoni yao kwa ufasaha kumeleta mvuta usiokuwa wa lazima na kupelekea Kamati ya Sheria Ndogo kutoa mapendekezo ambayo imewatoa ndani ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni muhimu kwenye siku za usoni, mamlaka hizi za kutunga sheria ndogo wafahamu kwamba sheria hizi ni kama huduma kwa wale walaji wasiposhirikishwa wale ambao ndiyo sheria inawagusa inaleta shida nyingi sana kwenye maeneo mbalimbali. Na ndiyo maana Kamati ilibaini mfano; kule Mbeya kulikuwa na sheria ndogo ambayo ilikuwa inaweka faini kwa watu wa bajaji kwenye fedha ambayo ni karibu sawa na mtu anayemiliki basi.

Sasa sheria hizi kama ambavyo kamati imebainisha ni kwamba hazina uhalisia wa mazingira ya wananchi na biashara ambazo wanafanya. Kwa hiyo, ni rai yangu mimi kama Mbunge basi mamlaka za kutunga Sheria ziweke mazingira ya wazi ili sheria zisiwe na malalamiko makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kama ambavyo taarifa ya Kamati imesema, imeonesha ndani ya sheria ambazo zimefika kwenye Kamati kulikuwa na shida ya kiuandishi kwenye sheria karibu 15. Hii tafsiri yake nini? Na nimaoni yangu mimi kama Mbunge pengine mamlaka ambazo zimekasimiwa kutunga hizi sheria ndogo ni vema wakawa na muda wa kutosha wa kupitia sheria inayohusu utungaji wa sheria ndogo kwa ufasaha ili kusudi kuipunguzia mzigo kamati wa kuchambua kazi ambayo ingefanywa na mamlaka husika kwenye utungaji wa sheria yenyewe. (Makofi)

Kwa hiyo, ni vyema basi kwenye siku za usoni ambako tutakwenda baadaye na nimuombe sana Waziri wetu wa Sera Bunge, Kazi na Ajira Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na kazi nzuri ambayo anafanya ya kusimamia utaratibu mzuri wa sheria ndogo basi asaidie pia hizi mamlaka zinazotunga sheria ndogo wajitahidi sana kufuata utaratibu ambao tumejiwekea kama nchi kwa ajili ya ustawi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kulichangia kwa mujibu wa taarifa ambayo imetolewa hapa ni kuhusu hoja mahususi ya hizi sheria zinazohusu watu wa filamu. Kwa mujibu wa taarifa ya Kamati ni dhahiri kwamba sanaa ya muziki nchini ni sanaa inayoajiri vijana wengi sana na vijana hawa wanafanya kazi hizi kwa ubunifu wao wenyewe, ni rai yangu kama Mbunge kwamba sekta ya sanaa nchini inahitaji kupewa ulezi na nafasi ya kukuzwa badala ya kuwekewa mazingira ya kudidimiza.

Kwa hiyo, ushauri ni kwamba Serikali ichukue hatua, inapotunga sheria za kusimamia sekta hii ya sanaa na muziki nchini basi sheria zake ziweke mazingira ya kuhamasisha sekta badala ya kuwavunja moyo wasanii wetu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nimatumaini yetu kwamba kama sekta hii ya muziki na sanaa itakuzwa kwa kiasi kikubwa itachangia sana kwenye pato la Serikali, lakini pia itachangia ajira kwa vijana wengi ambao nchi nzima sasa hivi wanafanya ubunifu katika sanaa na muziki. Kwa hiyo, niipongeze sana kamati kwa kazi nzuri walioyoifanya kwa ajili ya kuboresha kanuni za kusimamia filamu sanaa pamoja na muziki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia niwapongeze upande wa Serikali kwa Mawaziri ambao walienda kwenye Kamati ni dhahiri kwamba walitoa ushirikiano mzuri sana na hii imetoa picha kwamba dhamira ya Serikali imekusudia kuboresha maisha ya Watanzania na kuwapeleka Watanzania katika maisha bora zaidi. Kwa hiyo, hili ni jambo jema na niipongeze sana kwa hiyo kwa sababu ni sura nzuri, kwamba kama Taifa sasa na Serikali inatazama zaidi maslahi ya wananchi walioko kule chini ili kusudi kama Taifa tuweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano Waziri wa Elimu Profesa Ndalichako, kwenye Kamati hii ya Sheria Ndogo ameeleza vizuri sana utayari wake wakushirikisha wadau mbalimbali kwa ajili ya sekta ya elimu na tumeona wiki iliyopita ameanza kutekeleza kwa kuanza kukaa na wadau mbalimbali kwenye hii sekta ya elimu katika kutekeleza maoni ya Kamati ambayo imeanza kuyatoa hii ni sura nzuri na tukiendelea hivi kama Bunge basi mbele ya safari kazi itakuwa nzuri na nyepesi sana.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, baada ya hayo nakushukuru sana naunga mkono ripoti ya Kamati. (Makofi)