Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimwia Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa na mimi kuingia katika taarifa ya nchi hii ya kuchangia bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Waziri wa Fedha Kaka yangu Mwigulu kwa hotuba nzuri sana yenye kuleta matumaini makubwa. Naomba nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mama yetu mpendwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa anazozifanya na kuona umuhimu wa vijana na kufanya kikao kikubwa na vijana Jijini Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe pongezi zangu kwa Serikali kwa kuhusu suala zima hili la bodaboda, kwa kweli kitendo cha kutoa faini ya bodaboda kutoka shilingi 30,000 mpaka kufika shilingi 10,000 vijana tumefarijika sana. Lakini tutakuwa hatujafanya vizuri kama tutaishia tu kupunguza faini hii kutoka shilingi 30,000 kwenda shilingi 10,000 bado kwenye bodaboda changamoto ni kubwa tunafahamu wazi kwamba dhamira ya Serikali ni nzuri sana ya kuwatengenezea mazingira vijana ili waweze kufanya kazi vizuri lakini bado changamoto ni kubwa. Mbali ya kuwa na hii shilingi 10,000 kama faini na tusipoitumia vizuri hii shilingi 10,000 kama faini tutatengeneza tatizo lingine. Nasema hivi kwa sababu moja, matatizo mengi ya bodaboda yanahusiana na suala zima la kuwa hawana leseni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu leo kijana wa bodaboda ili aweze kupata leseni lazima awe na shilingi 70,000. Kwa hiyo, matatizo mengi na faini nyingi hizi wanapigwa kwa sababu hawana leseni. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali na nimuombe Waziri pamoja na kupunguza hii faini basi tuangalie pia utaratibu huu wa leseni. Kama itampendeza Mheshimiwa Waziri angalau hata iwe shilingi 20,000 kwa mtu mmoja. Kwa sababu, leo haiwezekani kijana wa bodaboda atoe shilingi 70,000 pia na watu wenye magari watoe shilingi 70,000 haiwezekani Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri, Rais wetu mpendwa, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, wakati anaongea na vijana wa Taifa hili kupitia vijana wa Mwanza aliongea na vijana wa bodaboda na katika hotuba yake ya vijana wa bodaboda alisema anatamani kuona vijana wa Taifa hili wanamiliki bodaboda zao wenyewe. Nasema hivi kwa sababu, mwanzoni bodaboda ilifikiriwa kuwa ni ajira kwa watu ambao hawajasoma lakini naomba nikupe taarifa hii, leo hii asilimia kubwa ya vijana waliomaliza vyuo vikuu leo wanafanya kazi ya kuendesha bodaboda, yote hii ni kwa sababu kuna changamoto kubwa ya ajira, vijana wameamua kujipatia ajira kupitia bodaboda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ili uingize bodaboda hapa nchini, kumekuwa na kodi nyingi na hizi kodi zinawanyima fursa vijana kumiliki bodaboda zao wenyewe ndiyo maana wanatumia bodaboda za watu na kuwaingizia utajiri watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nikitaka kuingiza bodaboda kwanza lazima nilipe import duty ambayo ni 20 percent pia lazima nitalipa excise duty asilimia tano, nitalipa VAT asilimia 18. Ukiangalia tozo zote hizi anayezilipa mtu wa mwisho ni yule mnunuzi, kwa hiyo hii inawafanya vijana wengi wanashindwa kumiliki bodaboda zao wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mheshimiwa Waziri, tunasema kabisa kwamba, maagizo ya viongozi wakubwa tunasema ni maagizo. Sasa Rais amesema natamani kuona vijana wanamiliki bodaboda zao wenyewe. Nilitarajia kuona mkakati wa Wizara ni namna gani vijana wataenda kumiliki bodaboda zao wenyewe. Hapa naomba nitoe ushauri kidogo tu kwa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na uhamasishaji wa vijana wengi kwamba wajiunge kwenye vikundi na vikundi hivi tumekuwa tukivielekeza kwenye Halmashauri zetu bado tuna Mifuko ya uwezeshaji wa vijana na akina mama chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, niombe Mheshimiwa Waziri kwamba tunaweza tukaratibu vikundi hivi ama kupitia Halmashauri zao au kupitia usajili wao wa vikundi angalau tukaona tukapunguza hizi kodi hasa VAT.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe Mheshimiwa Waziri tunaweza tukaratibu vikundi hivi either kupitia halamashauri zao au kupitia usajili wao wa vikundi. Angalau tukaona tukapunguza hizi kodi hasa VAT. Tukisema kama tutatoa hii asilimia 18 tutakuwa tumewafanyia ahueni vijana wengi, na vijana wataweza kumiliki bodaboda zao wenyewe. Lakini leo ukisema vijana waende benki, tunajua zipo benki zinazotoa mikopo ya bodaboda, wanasema ni riba nafuu lakini Riba hizo sio nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni kijana, nafahamu benki si rafiki kwa vijana wengi kwa sababu hawana hati za nyumba, viwanja wala mitaji kwa hiyo wakifika watakosa vigezo hivyo. Kwa hiyo nilikuwa napenda sana kuishauri Wizara, kwamba either wawape mamlaka halmashauri zetu hizi, kama itawezekana waondolewe hii VAT watakapokuwa wanaagiza bodaboda kwa vikundi ambavyo vimesajiliwa vipo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, muda ni mchache lakini naunga mkono hoja, ahsante kwa kunipa fursa ya kuingia kwenye record ya Taifa hili kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali. Ahsante sana. (Makofi)