Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa fursa hii, kuchangia kwenye bajeti hii ya Serikali ambayo imeongezeka kutoka trilioni 34.88 hadi trilioni 36.33, ikiwa ni ongezeko la asilimia nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Waziri na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti, kwa kuwasilisha vizuri sana hii bajeti yao na ninaomba kabisa nikiri kwamba, bajeti hii imeandaliwa vizuri sana kimkakati. Na inaleta matumaini makubwa sana kwa watanzania kwenye makundi mbalimbali ambao niseme, wafanyakazi, wafanyabiashara, wakulima, wakinamama, vijana, walemavu, watu wa viwanda, bodaboda na hata wastaafu wameipokea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti iliyoletwa ni nzuri na kusema ukweli inategemea kwenda kulegeza vyuma. Kule mitaani watu walikuwa wanasema kwamba, vyuma vimekaza. Bajeti hii nategemea kwamba, itakwenda kulegeza vyuma na itatupeleka mbele kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii inategemea kuongeza pato la Taifa kutoka asilimia 4.8 hadi asilimia 5.6, inategemea kudhibiti mfumko wa bei ibakie kati ya asilimia
3 na asilimia 5. Inategemea mapato ya ndani yatafikia asilimia 15.9 ya pato la Taifa na makusanyo ya kodi yanategemea kuongezeka kutoka asilimia 12.9 hadi asilimia 13.5 ya pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii pia, inategemea kama tutaipitisha Waheshimiwa Wabunge, naomba wote tuiunge mkono inategemea kuwa na akiba ya fedha za kigeni za kutusaidia kuagiza bidhaa za nje kwa miezi minne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina kila sababu ya kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri wanayofanya. Nianze kwa zile shilingi milioni 500 ambazo mama yetu ametupatia/Rais wetu, kwangu ni fursa kubwa sana. Kwamba, barabara zinakwenda kurekebishwa nchi nzima na niwapi tumeshaona tu Rais anaingia tu na kutupa zawadi kubwa kama hii? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo langu, hii fedha inakwenda kusaidia sana kwenye ujenzi wa barabara ya TPC, Mabogini mpaka Chekereni. Na kuna fedha ya ujenzi wa shule za Sekondari za Kata nina hakika wananchi wangu kule Moshi, Kata ya Kindi, Kijiji cha Chekereni, Weruweru tunakwenda kujenga shule pale kwa hiyo, ni jambo lenye heri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii pia, inakwenda kupunguza mzigo kwa mfanyakazi, ambapo kodi ya ajira inakwenda kupungua kutoka asilimia 9 mpaka asilimia 8 na hii itaongeza maslahi ya wafanyakazi na pia, kwa wafanyakazi pia kuna bilioni 449 inayokwenda kupandisha watu karibu 92,000 madaraja. Pia niipongeze Serikali kwa kupunguza faini kwa watu wa bodaboda, kutoka shilingi 30,000 hadi shilingi 10,000 ni kitu kizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na pia Serikali inakwenda kubadilisha mabadiliko ya Kanuni ya Sheria ya Bajeti, ambapo kama tutapitisha hakuna tena kurudisha fedha Hazina zitakuwa zinabakia kule na hii ni kitu kizuri. Kuna mambo mengi sana ambayo kutokana na muda sitaweza kuyasema nitawasilisha kwa maandishi. Lakini Serikali vilevile imepania kikamilifu kulinda viwanda vya ndani kwa kuondoa tozo za ushuru wa forodha, katika malighafi za aina mbalimbali ambazo zitaingizwa na zitasaidia kuboresha viwanda vya ndani. Kwa mfano, kwenye kilimo vile vifungashio vya maziwa, mbegu, kahawa, korosho, pamba wameondoa ushuru wa forodha na hii itachochea watu kufungua viwanda na kufanya biashara hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nina ushauri kwa Serikali. Ushauri wangu wa kwanza ni kwamba, katika bajeti ya Taifa ya trilioni 36.3 asilimia 29.3, ambayo ni sawa na shilingi trilioni 10.66 zitatumika kulipa deni la Taifa. Hizi ni fedha nyingi karibia one third itatumika kulipa deni la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali ikiwezekana tutafute vyanzo vingine vya fedha, ili tukusanye fedha nyingi na zitumike kwenye kudhamini miradi mbalimbali. Vile vile ninaishauri Serikali ibuni mbinu mbalimbali za kukusanya kodi kwenye biashara ndogo ndogo. Hizi biashara ndogo ndogo zimepanuka sana ni wengi lakini wengi wao hawalipi kodi. Kwa hiyo, mjipange muangalie namna ya kuwakata kodi hawa wafanyabiashara wadogo wadogo, ambao wanaweza wakachangia sana katika pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninaishauri Serikali iendelee kuboresha mazingira ya uwekezaji kwa wawekezaji wa ndani na wawekezaji wa nje. Ii tupanue wigo wa kuwaajiri watu wengi zaidi na tukishapanua wigo wa kuajiri watu wengi vile vile tutapata kodi na tutaongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inategemea kukopa ili ku-support miradi ya maendeleo na inategemea kukopa shilingi trilioni 7.34 ili kugharamia miradi ya maendeleo. Katika hizi shilingi trilioni 4.99, zitatoka kwenye Taasisi za ndani kwenye Mabenki ya ndani au Taasisi nyingine za ndani na shilingi trilioni 2.35 zitatoka nje.

Nilifikiri ilitakiwa iwe the opposite kwamba, nyingi tukope kutoka nje na kidogo tukope ndani, Ili tuwaachie wafanyabiashara wa ndani waweze kukopa kutoka kwenye Mabenki yetu. Kwa sababu tunawaminya wafanyabiashara wa ndani hawana mahali pa kukopa na hiyo inasababisha wasiweze kuwekeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu wa pili, ni kuhusu ushirikishaji wa sekta binafsi katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo. Kwenye ule Mpango wa Pili, ni ukweli usiopingika kwamba, Serikali haikuishirikisha sekta binafsi sana kwenye Mpango wa Pili wa Maendeleo. Kazi nyingi zilikuwa zinafanywa na Serikali, Taasisi za Serikali kwa mfano, mikutano ya Kiserikali tulikuwa tunaambiwa twende VETA tusiende kwenye hoteli nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya aina mbalimbali walikuwa wanafanya Taasisi za Serikali. Kwa hiyo, sekta binafsi ilipwaya sana walikuwa hawaajiri. Kwa hiyo, ninaishauri Serikali kwenye Mpango wa Tatu huu, sekta binafsi wameshajifunza kwamba, kama kuna kitu walifanya makosa sasa hivi watarekebisha na tuwashirikishe ili waweze nao kushiriki kwenye ujenzi wa Taifa lao na kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa mwisho na ushauri wangu wa mwisho kwa Serikali ni kwenye sekta ya kilimo. Wabunge wengi hapa walilia sana kwamba, kilimo hakijatendewa haki. Lakini mawazo mengi yalichukuliwa ila la kilimo pamoja na kwamba, karibu kila Mbunge alisema bajeti ya kilimo ni ndogo halikubebwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri, ikiwezekana kwenye ile bajeti ijayo tunajua hili hatuwezi kulifanyia kitu kikubwa lakini kwenye ile bajeti ijayo tujitahidi kilimo, mifugo, wapate fedha za kutosha kwa sababu sehemu kubwa ya watanzania ni wakulima na wanahitaji kusaidiwa. Tukishapanua kilimo tunauhakika kabisa kwamba tuta-improve productivity na watu watapata kipato cha kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)