Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi nichangie katika bajeti ya Serikali, kama ilivyowasilishwa juzi hapa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Nipende kupongeza sana bajeti hii nzuri, ambayo Serikali imeiwasilisha hapa kwetu. Nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa bajeti nzuri ya kwanza. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa bajeti nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya bajeti hii ni mazuri sana na hasa hasa ambaye imenigusa sana ni ile ya TARURA. Kuongeza fedha kwenye mamlaka hii au Wakala huu wa barabara vijijini, ili iweze kupata uwezo mkubwa wa kuboresha barabara za vijijini. Tunafahamu wote kwamba, vijijini ndio kuna uchumi, ndio kuna kilimo, kunapelekwa pembejeo, kuna huduma za afya kwenda kwenye zahanati na vituo vya afya, bila barabara huwezi kuzifikia huduma hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule kwa hiyo, kwa kuwa na fedha zaidi kwenye mfuko wa TARURA, ina maana huduma hizi zinakwenda kuboreshwa na kuonekana na kufikiwa na wananchi kirahisi zaidi. Lakini na mambo mengine mengi sio tu TARURA peke yake, ambayo bajeti imeyagusia na kuyazingatia. Nnaipongeza sana Serikali ya CCM kwa kuwa sikivu na kwa kuwa inaboresha maendeleo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo napenda nizungumzie suala la elimu kwa sababu, tunapoongelea bajeti hapa tunaongelea uchumi na huwezi kupanga uchumi kama huna elimu nzuri. Elimu ndio ufunguo wa maisha na ndio ufunguo. Sasa, kwa hiyo bila elimu nzuri huwezi kuwa na uchumi mzuri na elimu yetu bado ni ya mitihani. Mtoto akitaka asonge mbele ni lazima afanye mitihani, afaulu, aende hatua nyingine, hatua nyingine, mpaka vyuoni huko aweze kuhitimu, akifeli mitihani hawezi kwenda huko. Nchi nyingine hawatumii utaratibu huo, kama Ujerumani na nchi nyingine wana system tofauti ya vitendo sisi ni ya mitihani kwa hiyo, lazima mtoto afaulu mitihani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wiki iliyopita nilikwenda Jimboni, najitahidi mara kwa mara nakwenda jimboni, natembelea wapiga kura na safari hii nilitembelea shule. Na nawashauri Wabunge wenzangu mnapokwenda Majimboni, msisahau shule, mtembelee shule, shule za sekondari na za msingi. Kwa sababu, kama shule ina wanafunzi 500 ukaenda pale kusalimia wanafunzi 500, umesalimia jimbo zima karibu kwa sababu, ni kama watu 5,000. Kwa hiyo, nilifika pale nikaona shule zinavyoendelea, nikakuta shule zimefungwa kama ilivyo kawaida sasa hivi ni wakati wa likizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baadhi ya shule nilizozitembelea nikakuta vijana wa Form Four wamebaki. Shule za Kata wamebaki kwa mpango maalum wa kusoma ili waweze kufaulu mitihani. Nilitembelea shule ya Butura ni Sekondari, Shule ya Kaja Sekondari, Katoro Sekondari, Bujuko Sekondari na nyingine nyingi. Hizi zilikuwa na wanafunzi wapo wa Kidato cha Nne wanajisomea, kwa mpango wa kujaribu kufaulu mitihani ya Taifa ya mwezi wa kumi na moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na wanafunzi hawa wana shida nyingi sana. Mtoto anaweza akawa anaumwa hajahudhuria shule au amechelewa kwa sababu mbali mbali, hana uniform hajaenda shule, uwezo wa wazazi ni mdogo. Kwa hiyo, wanaamua kubaki ili waongeze muda wa kujisomea au walimu hawatoshi, kama tulivyosikia humu ndani kila siku walimu wa sayansi na wewe umesema kule kwako walimu wa sayansi ni pungufu. Kwa hiyo, walimu wanaamua kujitolea muda wa ziada, waweze kutoa elimu hii ambayo wanafunzi wameikosa huko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, ikatokea mtu mmoja Wizarani pale amezuia utaratibu huu. Kaandika waraka kwamba, shule zikifungwa zifungwe hakuna kubaki shule, nikashangaa sana! Hawa vijana wanaobaki shuleni, wanabaki ili wajiandae na mitihani na hawana uwezo wa kufaulu bila kubaki. Na sio kwamba, wana fedha nyingi wanabaki pale wanajitolea na wanakaa mabweni shule za kutwa zile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanaingia kwenye madarasa mle, hawana magodoro, wanaweka nyasi chini wanalala, ili wasome waweze kuongeza ufaulu. Walimu wanajitolea kufundisha bure bila malipo, wazazi wanachangia mihogo, ndizi, maharage, ili watoto wale usiku na mchana, wasome waendelee waweze kufaulu. Huyu mtu mmoja Kamishina wa Elimu amezuia utaratibu huo lengo lake silifahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachelea kusema ana lengo la kuharibu elimu ya nchi hii na hivyo ana lengo la kuua uchumi wa nchi hii. Watoto wanajitolea, wazazi wanajitolea, walimu wanajitolea. Mtu mmoja anakaa pale Wizarani anaandika waraka anasema hii hairuhusiwi, Serikali, haichangii. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kamishina wa Elimu hachangii. Sasa inashangaza kweli kwa nini anazuia, inamuhusu nini yeye. Kuna mtu mmoja aliwahi kusema kwamba ukitaka kuua Taifa wala usipeleke sumu kwenye wananchi wale au kuharibu madaraja na barabara wewe ua elimu tu. (Makofi)

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ua elimu na utakuwa umefanikiwa kuua Taifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Rweikiza kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Ndalichako.

T A A R I F A

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba, Wizara jukumu lake pia ni kuwalinda watoto. Kwa hiyo, Serikali haiwezi ikaruhusu mtu sehemu ambayo sio bweni tena amesema watoto wanaweka nyasi, wanalala mazingira yanakuwa ni hatarishi, miundombinu haiko salama kwenda pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpe taarifa tu kwamba, shule ambazo sisi tumezuia ni zile ambazo wanalazimisha wazazi kuchanga fedha. Kwa hiyo, suala la kwamba watu wanajitolea sio kweli, wanalazimisha na ni kinyume na maelekezo ya Serikali ya elimu bila malipo. Kwa hiyo, nilikuwa nataka tu nimpe taarifa hiyo, ili labda anapochangia aweze kutupatia maeneo mahususi ambayo anayalalamikia, ili Serikali iweze kufanyia kazi vizuri.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Jasson Rweikiza, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza ulinde muda wangu. Lakini ninachosema ni kwamba, nchi hii inatumia utaratibu wa mitihani, mtu akifeli, amefeli, ameishia hapo ndio mwisho. Kwa hiyo, wazazi na watoto na walimu wanajitolea kusoma wala hakuna anayelazimisha michango. Niko kwenye sekta ya elimu yaani elimu ndio system yangu nafahamu utaratibu wa elimu. Sikutangaza maslahi kwa sababu haina masilahi yangu kifedha, lakini niko kwenye sekta ya elimu na ninaelewa vizuri ninachokisema. Serikali inaharibu elimu, Wizara ya Elimu inaharibu elimu kwa hiyo, taarifa hiyo siikubali, naikataa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nasema kwamba, kuna mtu aliwahi kusema, mtaalam wa elimu, mtaalam wa uchumi, mtaalam wa utawala kwamba, ukitaka kuua Taifa, ua elimu. Usihangaike na mambo mengine ua elimu. Huyu Kamishina wa Elimu amekusudia kuua elimu ya nchi hii, haiwezekani uzuie watu kusoma, watafauluje bila kusoma? Watashindwa mitihani, watapotea, wataishia darasa la saba, wataishia Form Four na ndio mwisho wao na watakuwa wanapata zero.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajitahidi watoto wasome, waende mbele, wafike vyuo vikuu na vyuo vingine, wapate stadi mbalimbali vyuo vya ufundi. Lakini hawawezi kufika huko bila kufaulu mitihani yao ya ngazi mbalimbali, ambayo lengo la kufanya hizo kambi na halikuanza leo, tangu enzi hizo. Yeye mwenyewe Waziri ni Profesa asingefikia U-Profesa kama asingefanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, amesoma kwa bidii za wazazi, za walimu, za shule mbalimbali, za vyuo mbalimbali. Sasa kwa nini anazuia utaratibu huu ambao ni mzuri, nasema ni mzuri. Kule vijijini hawalipi fedha kwa sababu ya kulazimishwa, wanalipa fedha hizo ndogondogo mihogo hiyo, kwa sababu ya kupenda wenyewe na ndio walioomba. Ni Mbunge wa Jimbo nashiriki kwenye mikutano hiyo, watoto wanaomba, wazazi wanaomba. Wanazuiwa kufanya huu utaratibu ambao nafikiri ni kuua elimu. Kwa hiyo, tujitahidi na yeye akiwa ndio Waziri wa Elimu, azuie utaratibu huo wa kuua elimu asimamie, ili elimu iwe bora na tuweze kufanikiwa katika mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naomba kuishia hapo. (Makofi)