Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Janeth Elias Mahawanga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia bajeti hii. Kwanza naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa bajeti hii nzuri kwa Serikali ya Awamu ya Sita maana ni bajeti ya kwanza. Vile vile, nampongeza Waziri wa Fedha na Mipango na Naibu wake pamoja na timu nzima kwa bajeti hii nzuri. (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, bajeti hii inatia matumaini na faraja kwa Watanzania kwani ni bajeti ambayo imekidhi changamoto zote za jamii yetu kwa kuweka vipaumbele ambavyo Wabunge wengi walichangia katika Wizara mbalimbali. Vile vile, bajeti hii inakwenda kukamilisha mahitaji yote hususan kwenye masuala ya afya na miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napongeza kuhusiana na kipengele cha kodi ya line za simu. Tija ya kodi hii ni nzuri, kama ambavyo bajeti imeonyesha Shilingi za Kitanzania bilioni 360 zinakwenda kupatikana ambapo zitakwenda kujenga zahanati na mahospitali. Naiomba Serikali, fedha hizi kama zitakwenda kutekeleza haya, basi kiu kubwa na changamato ya masuala ya afya katika jamii yetu itakwenda kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naipongeza bajeti hii kwenye kodi ya shilingi mia katika kila lita ya mafuta. Fedha hii itakapopatikana itapelekwa TARURA kama ambavyo imeonyeshwa, ni kitu kizuri sababu fedha hizi zitakapokwenda kutoa changamoto ya miundombinu, uchumi wetu utakwenda kuimarika hususan kwenye jamii yetu hasa vijijini, kwani uchumi wa nchi unategemea sana suala la miundombinu. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali kwa kuliona hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile bajeti hii imekwenda kugusa masuala ya vikundi vya akina mama na vijana, hasa katika kutoa mikopo. Ukiangalia hata Mheshimiwa Rais alipoongea na akina mama ali-insist sana suala la vikundi vya akina mama kujiunga ili wapate mikopo ambayo itasaidia kutoa ajira na kufanya biashara zenye tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kupitia bajeti hii, wakaangalie katika suala la Sheria ya Fedha Mwaka 2018, kwani limekuwa ni mzigo hasa kwenye vikundi vya akina mama. Naiomba Wizara ikatumie wataalamu wa BoT katika kutoa elimu, maana vikundi vingi vimeshahamasishwa kujiunga, lakini kupitia sheria hii wengine wanafunga, hawaelewi sheria ile inataka nini hususan kwenye kutumia teknolojia ya TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Wizara itumie wataalamu wao wa BoT ambao wanaweza kufafanua sheria hizi wapite kwenye Wilaya wakutane na Madiwani na Bibi Maendeleo, watoe miongozo ya sheria hii hasa katika vikundi vya akina mama na vijana ili nao watakaposhuka chini kwenye makato wakikutana na akina mama waweze kufafanua sheria hizi ili vikundi viende kuwa imara vikatumie fursa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kupitia bajeti hii ikaangalie masuala ya sheria za fedha, lakini zaidi sana ikaangalie kwenye kipengele cha mabenki, kwani mabenki yatakaposhirikiana na Serikali katika kuongeza tija kwenye mikopo ya wafanyabiashara, itasaidia sana, maana mikopo ya asilimia 10 bado haitoshelezi. Kwa mfano, Mkoa wa Dar es Salaam, kazi za usafi wa barabara ambazo zilikuwa zikifanywa na akina mama wengi sasa hivi zile kazi zimeamishwa kwa SUMA JKT. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna kundi kubwa la akina mama ambalo limepoteza ajira na kupitia ajira zile walikuwa wakilea familia, wakisomesha watoto na kujikimu kwa mahitaji yao ya kila siku. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie sana taasisi za kifedha hususan mabenki, kuangalia ni jinsi gani ambavyo mabenki haya yataweza kuongeza mikopo kwa akina mama na vijana lakini mikopo hiyo itoke kwa riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naishauri Serikali iwekeze kwenye mfumo thabiti ulioungana (complete and consolidated system) ambayo watakuwa na utambulisho utakaokuwa na kanzidata ya taarifa za wafanyabiashara. Taarifa hizo zikiwa zinahusisha biashara zao, mali zao anuani za makazi ambazo zitaweza kusaidia mabenki kuwatambua hawa watu na kutoa mikopo kwa gharama nafuu, lakini kwa kutumia mfumo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Serikali iangalie kwa jicho la pili kuwekeza katika mabenki yote kuhakikisha kwamba gharama za uendeshaji wa mabenki, zisizidi asilimia 55 ya mapato. Ni kwamba inasema ikizidi benki hairuhusiwi kupata dividend ambayo ni kutoa faida. Kanuni hii imefanya mazingira ya uwekezaji wa mabenki kuwa ngumu. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie sana katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, kwa kupitia bajeti hii, naiomba Serikali ijikite zaidi katika mapato na mwenendo wa uchumi hususan kwenye ukuaji wa pato la Taifa, kwenye mapato na matumizi ya Serikali, kwenye deni la Taifa, Serikali ijikite sana kuangalia ukopaji na ulipaji wa madeni ili Taifa letu lisije likaingia kwenye adha ya kutokopesheka. Zaidi Serikali iboreshe tena kwenye sekta ya fedha; Serikali irejeshe mifumo iliyokuwa inasaidia benki kutoa mikopo kwa wingi (Guarantee Credit Schemes). Benki hizi zilikua kwa kutumia mifuko hii; mifuko ilikuwa inachochea sana utoaji wa mikopo. Kwa hiyo, Serikali ijitahidi kurudisha hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile uendeshaji wa sekta binafsi. Kama tulivyoona Serikali imeweka mazingira mazuri hususan kwenye Mfumo wa Sera na sheria za kodi ambazo zimekuwa ni kivutio kwa wawekezaji wetu. Mwisho, ijizatiti katika tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naipongeza Serikali kwa bajeti hii nzuri na ninaunga mkono hoja. (Makofi)