Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Salum Mohammed Shaafi

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Chonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. SALUM MOHAMMED SHAAFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi kuchangia bajeti hii muhimu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nichukue fursa hii nimshukuru Mwenyezi Mungu kutujaalia kuweza kukutana hapa na kujadili jambo muhimu ambalo ndiyo msingi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuri Wizara kwa namna walivyoweza kutuwasilishia bajeti hii nasi kuweza kuichambua na kuijadili na kuitolea maoni yetu na kama hatuna la kushauri basi tumepata nafasi hiyo. Mimi leo sina mengi ya kusema lakini naomba niseme machache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza binafsi nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza kwa kipekee kabisa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwenye macho haambiwi tazama. Sote tunaona namna Mama yetu anavyoongoza Taifa hili na niseme Mheshimiwa Rais wetu Mwenyezi Mungu kamjaalia kipaji cha hekima na busara. Namuomba Mwenyezi Mungu ampe afya njema, ampe umri mrefu wa kuzidi kutuongoza Watanzania kusimamia haki na kujali utu wa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii kuna mambo mengi yamezungumzwa. Mimi leo naomba nitoe rai na kuishauri Serikali. Mara baada ya kupitisha bajeti hii siku ikifika tunaenda kuwapa fedha Wizara au mamlaka husika. Naomba niishauri Serikali iende ikazisimamie fedha hizi katika yale maeneo yote ambayo yamepangiwa kupewa hizi fedha. Wawasimamie ili tuondokane na ile kadhia ya watu kuhujumu uchumi, watu kuiba fedha za Serikali, watu kuiba fedha za walipakodi wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haya tukifanya haya tutakuwa tumedumisha nidhamu Serikalini lakini tutakapoziacha tu hizi fedha ziende ile nidhamu ya fedha Serikalini itakuwa haipo, lakini mara baada ya kuwapa fedha hizi naishauri Serikali sasa iwakumbushe watumishi hawa wajibu na majukumu yao katika kazi zao. Jeshi la Polisi likumbushwe wajibu wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona mengi yanatokezea wananchi wanalalamika juu ya kadhia ya baadhi ya Wanajeshi la Polisi, yapo mitaani! Leo tukiangalia tu Taifa letu linapita katika hali ya usalama na amani ya kutosha kabisa ni kwa sababu wanasiasa ndiyo walioleta amani hii. Ni wanasiasa ndiyo walioleta amani hii katika nchi hii. Nani anasema haya? Mengi yalipita, kule kwangu Zanzibar mengi yalifanyika kupitia Jeshi hili la Polisi pamoja na vikosi vya SMZ, watu walipigwa, watu walinyanyaswa, walipigwa risasi, yale makovu Wazanzibari wameyafunika, wanaamini sasa tumekuwa kitu kimoja tunasonga mbele, tumesahau yaliyopita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa yaliyopita yasije yakarejea tena. Ili yasijirudie lazima Serikali muende mkawakumbushe sasa hawa watumishi wajibu wao katika utekelezaji wa kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba niwasemee wenzetu wastaafu. Hawa wastaafu wamelitumikia Taifa kwa muda mrefu sana, wamejitoa kwa hali na mali, wamejitoa kwa kila hali kuhakikisha kwamba wanatumikia nchi yao. Naomba bajeti hii iwe ni sababu ya kwenda kumaliza kero za wastaafu hawa, isiwe kila mwaka wa bajeti katika Bunge hili tunawajadili hawa wastaafu kwamba bado posho zao hawajazipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wastaafu wengi na wana miaka mingi bado hawajapata posho zao. Naomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kijana mwenzangu, muonekano wa sura yako inaonekana ni msikivu na mtiifu, nenda kalisimamie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tu niendelee kusema Serikali hebu nendeni TFF. Wizara husika nendeni TFF mkaangalie kuna nini TFF? Kuna shida gani TFF? Manung’uniko haya yaweze kuisha, niishauri Serikali nendeni huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kikubwa tu na cha mwisho ambacho naomba nikiseme ni kudumisha Muungano wetu na ninachukia sana wanapojitokea baadhi ya watu kuunyoshea vidole upande wa pili kwamba hawaupendi Muungano, sio kweli, wao wanaonyosha ndio ambao hawaupendi Muungano. Hakuna aliyesema hataki Muungano. Sote tunataka Muungano, lakini tunataka Muungano wa haki na usawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya nikiamini hapa Wabunge wengi wamesimama, wamesema na ninaishukuru Serikali kwamba wameingiza hizo shilingi milioni 500 ili kuweza kusaidia maendeleo katika majimbo yao, lakini leo, jana na juzi, baadhi ya Wabunge wanahoji fedha hizi je, na kule Zanzibar zitapatikana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwa muono wangu mimi naamini sisi sote ni Watanzania. Kama tutabaguliwa Wazanzibari katika fedha hizi sasa hapa ndio tutaanza kuhoji kuhusu suala la Muungano, kwa sababu Serikali yangu ni sikivu, Serikali yangu nawaelewa ni wasikivu, sidhani kwamba ikifika Jumatatu jambo hili litajadiliwa tena humu kwa sababu mimi nafahamu Serikali yangu ni sikivu na jambo hili italisikia na Wazanzibari nao ni sehemu ya Muungano. Hapa Bara Wazanzibari wapo wanafanya biashara, wanalipa kodi, sasa leo iweje eti Wazanzibari wasipewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siamini; mimi siamini, mimi naamini tutapewa, zitatumika Zanzibar na ile fedha ambayo inajenga shule ya sekondari kila kata na Zanzibar kila jimbo tutajengewa shule ya sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nimalizie kwa kusema naishukuru Serikali. Waziri Mheshimiwa Mwigulu unanisikia sana rafiki yangu, shilingi milioni 500 hii ni haki ya Watanzania, hatuna Mbunge wa Bara wala hatuna Mbunge wa Zanzibar; ni Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sote tuliomo humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nashukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)