Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametupa afya na nguvu. Jambo la pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kwa bajeti hii ambayo ni nzuri kwa kweli, inatia moyo. Kipekee nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu, kwa kasi aliyoanza nayo kwanza ya kuibua miradi mipya, lakini pia kuendeleza miradi ile ambayo iliachwa na mtangulizi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa ambalo linaelekea kujitegemea, lazima tuhakikishe tunawekeza kwenye mapato ya ndani, hasa hasa upande wa kukusanya kodi. Ukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Waziri, mapato ambayo yanakusanywa kutokana na kodi ni asilimia 4.5 ambayo inatoka kwa watu milioni 2.7. Kwa kweli bado tunayo kazi kubwa ya kuhamasisha Watanzania kulipa kodi. Hili jambo Waheshimiwa Wabunge, tusiiachie Serikali, tunahitaji kuwa mstari wa mbele. Tunakuja hapa tunahitaji maendeleo, tunahitaji barabara, tunahitaji maji na huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya yote hayo, lakini tusipohamasisha Watanzania kukusanya kodi, siku moja mara mbili hivi, nimeenda kule Kariakoo. Ukinunua vitu vya milioni mbili, unashangaa wanakwambia tuandike shilingi 300,000, sasa ni wangapi ambao wanafanya hivi? Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, lazima tuwe mstari wa mbele kuhakikisha tunawahamasisha Watanzania kukusanya kodi, ndio tutaweza kufika kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Serikali imekuwa ikiweka nguvu sana kwenye viwanda. Hapa niishauri Serikali, viwanda hivi viendane na kilimo, ili viwanda vyetu viweze kupata malighafi ambazo zinatoka ndani. Kwa sababu, tutakapopata malighafi zinazotoka ndani nina uhakika uzalishaji utapungua. Kwa hiyo, hili lazima Serikali iliangalie, tuwekeze sana kwenye kilimo. Tumekuwa tukiimba, Mungu ametujalia Taifa lina ardhi nzuri, tuna vipindi virefu vya mvua, hebu tutumie fursa hii au nafasi hii, ambayo Mungu ametujaalia kuweza kuwekeza kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo hiki ili kiwe na faida, lazima tuhakikishe tuna soko la uhakika, wataalam watoke waende kutafuta masoko. Tusiishie kukaa ndani, tukaishia kukaa maofisini bila kutafuta masoko na ili tutakapotafuta masoko, nina uhakika uzalishaji utaongezeka, kwa sababu, mkulima atakuwa na uhakika ni wapi anaenda kuuza mazao yake. Kwa hiyo, hili nalo tulipe kipaumbele tuliangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilisemee, niipongeze Serikali kwa upande wa vijana wetu hawa wa bodaboda. Hii ni ajira, niiombe sana Serikali pamoja na kupunguza hii kodi, bado niiombe Serikali upande wa Polisi tusijikite kutoza faini. Tutoe elimu kwa vijana hawa na hili naamini litawasaidia kwa sababu, hii ni ofisi kama zilivyo ofisi nyingine. Vijana hawa wanafanya kazi kwenye mazingira magumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilisemee, niipongeze Serikali kwa upande Madiwani. Tumefanya kazi nzuri, lakini Madiwani hawa wamechaguliwa kama sisi. Pamoja na malipo yao kulipwa na Serikali kuu, lakini niiombe sana Serikali, iangalie namna gani ya kuboresha posho ya hawa Madiwani ili iweze kuendana na kazi wanazozifanya. Waheshimiwa Wabunge leo hii sisi tupo hapa, lakini wanaofanya kazi kubwa ni Waheshimiwa Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni kwamba, tunao hawa watu wetu Wenyeviti wa Vijiji. Kwa kweli niseme Serikali hili jambo lazima iliangalie, inaitwa Serikali ya Vijiji, ni Serikali gani ambayo Mwenyekiti wa Kijiji halipwi, hakuna chochote anachokipata. Kwa hiyo, niombe, tumeboresha kwa Watendaji, tumeboresha kwa Madiwani, hebu twende kuangalia, Wenyeviti wetu wanafanya kazi kwenye mazingira magumu. Mwenyekiti yuko ofisini lakini hakuna anachopata. Mwisho wa siku ndio maana hawa Wenyeviti wa Vijiji wanaanza kuwaibia wananchi. Kwa sababu, hana kipato mwananchi akija kupata huduma, anachomwambia lazima uache Sh.20,000/=. Kwa hiyo, niombe sana Serikali hili iliangalie na lenyewe ilipe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niipongeze Serikali, leo hii tumepata chanzo cha mapato kwenye barabara zetu. Niombe na niishauri Serikali, tunataka tuone hizi fedha zinaenda kufanya kazi kwa wananchi. Nina uhakika wananchi wetu hawana shida kwa sababu, hizi fedha zitakapokatwa kwenye simu, zinaenda kutoa huduma kwa wananchi wetu. Zinaenda kujenga barabara, zinaenda kuboresha miradi ya maji na afya na tunaenda kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wamefanya kazi kubwa, kama wameweza kujenga maboma ya mamilioni, leo hii ukiwaambia Watanzania wachangie miradi ya maji, wachangie umeme, wachangie barabara, sidhani kama lina shida. Kinachotakiwa, hizi fedha lazima ziwekwe kwenye Mfuko Maalum, ziende kufanya kazi iliyokusudia, watu waone huduma za maji, watu waone umeme, watu waone barabara. Kwa hiyo, niombe sana Serikali hili nalo iliangalie sio mnaweka tu, maana kuna fedha nyingine inaweza ikakusanywa, lakini mwisho wa siku ikatumika tofauti na ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie jambo lingine la Corona, niipongeze Serikali kwa juhudi ambazo zimekuwa zikifanyika. Hata hivyo, niwaambie ndugu zangu, Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, Taifa hili ni Taifa la Mungu na ninyi mtakuwa mashahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majirani zetu wanaotuzunguka sio kusema hawachukui hatua kama sisi, lakini Mungu analo kusudi na Taifa la Tanzania. Kama italazimika kutumia barakoa, tutazitumia, kama italazimika kupata chanjo tutazipata, lakini nataka niwaambie Watanzania, kama tusipoendelea kumpa nafasi Mungu, ambaye amelilinda Taifa hili, wenzetu wanakufa, lakini Taifa hili lipo salama. Hatua zote tuchukue, lakini lazima tutambue, Mungu ndiye namba moja. Tusipompa Mungu nafasi namba moja, tutachoma hizo chanjo, tutavaa barakoa hizo na tutakufa. Taifa hili liko salama kwa sababu, Mungu analo kusudi na Taifa la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)