Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa wasilisho nzuri la mapendekezo haya ya bajeti ya Serikali na kwa pongezi nilivyozisikia huu ni ushahidi kwamba Chama cha Mapinduzi kinalea vizuri sana. Maana Mheshimiwa Naibu Waziri alikua mwenyekiti wa vijana wa CCM kwa hiyo alilelewa vizuri, Mheshimiwa Waziri amekua Mweka hazina wa Chama cha Mapinduzi Taifa na Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi. kwa hiyo, ni ushahidi kwamba Chama chetu kinalea vizuri na matunda yake tunayaona, hongera sana Mheshimiwa Waziri na timu yako nzuri kwa kazi ambayo mmeifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Rais hii ni bajeti yake ya kwanza, Rais wa Awamu ya Sita na ni bajeti nzuri sana sana katika historia bajeti zetu hii ni bajeti nzuri na kama bajeti yake hii ya kwanza imefanyika hivi nadhani mama tukimpa bajeti kama 10 hivi nchi yetu itakwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tumuunge mkono kwa bajeti yake ya kwanza na bajeti zake tano za mwanzo halafu 2025 tumuongeze bajeti zingine tano ili mambo yetu yaende sawa sawa. Kwa tafsiri rahisi kabisa hii ni bajeti ya watu na Mheshimiwa Waziri umetutendea haki maana sisi hapa tumeletwa na watu umetuletea bajeti ya watu umehalalisha kurudi kwetu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya watu kwanini? Kwanza umegusa maeneo ambayo ni ya muhimu sana suala la barabara vijijini, suala la maji, suala la afya, suala la miundombinu ya elimu, haya ni maeneo makubwa yanagusa watu na kumekuwa na kelele ya muda mrefu ya kushughulika na maendeleo ya watu. Sasa umeya-identify jambo la kwanza, lakini la pili umependekeza vyanzo vya fedha ya kwenda kutatua mambo haya hili jambo ni kubwa sana na mimi naunga mkono mapendekezo ya Wabunge wengi kwamba hizi fedha tuziwekee wigo, tuzikusanye ndiyo lakini tuziwekee wigo zikafanye hii kazi uliyokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niwaombe Watanzania tuunge mkono na tulipe kodi ili tujivunie kujitawala ni kujitegemea na haya mapendekezo yanatupeleka kwenye kujitegemea badala ya matatizo haya kuendelea kutegemea fedha kutoka nje. Mheshimiwa Waziri na Serikali hii tunawaungeni mkono kwa mawazo haya mazuri na ninaomba Wabunge wote bila kujali tofauti zetu, mwisho wa siku tupige kura ya ndiyo ili tukajenge barabara tukapeleke afya tukapeleke elimu tukapeleke maji vijijini. Mheshimiwa Waziri hii kazi nzuri hii ni bajeti ya watu, mmetafsiri vizuri ukuwaji wa uchumi wetu kwenye maisha ya watu tunawaungeni mkono kwenye jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, nataka kupongeza uamuzi wa Serikali wa kuamua kuangalia upya finance ya miradi yetu mikubwa. Hili jambo ni kumbwa sana litasaidia kupunguza mzigo mkubwa kwa wananchi wa kawaida financing ya miradi yetu, tumeshaanza wenyewe vizuri hapa tulipo sasa tuangalie financing yake na kwenye hili Mheshimiwa Waziri tuweke nguvu tuhakikishe tunafanya credit rating ya nchi yetu itatusaidia sana kupunguza hali ambayo tunapambana nayo kwenye mikopo mbalimbali ambayo tumekua tukiomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono credit rating ifanyike ni wakati sahihi tuko uchumi wa kati credit rating itatuweka mahali pazuri sana na tutapata fedha ya kuendeleza miradi hii. Kwa haraka sana nilitaka nizungumze eneo moja kubwa la hisa za Serikali kwenye makampuni, hisa za Serikali kwenye makampuni na hapa nazungumzia makampuni mawili TIPER na PUMA na bahati nzuri kuna fedha nyingi za kutosha huku, makampuni yote haya mawili Serikali ina hisa asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TIPER tuna asilimia 50, na ORXY energy wana asilimia 50. Sasa nataka nizungumze namna ambavyo tunaweza tuka maximize hisa zetu zikatuletea vyanzo vingine vya mapato. Sasa hivi hapa TIPER tuna infrastructure ya matenki ya kuhifadhi mafuta. Sasa tusiruhusu wengine ndani ya Serikali humo humo wakatengeneza tena matenki mengine kuna hoja ya bandari kutaka kuingia huko hakuna sababu tutumie yale yale ya TIPER. Kuna hoja ya TPDS kwenda huku, kila mmoja atomize wajibu wake kazi hii ya kupokea haya mafuta na kuyahifadhi waachiwe watu wa TIPER.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hapa Mheshimiwa Waziri kuna jambo very specific, tokea TIPER imeanza MD wa TIPER amekuwa anatoka Ufaransa ambayo ni makubaliano na mimi nakubaliana. Lakini juzi imetokea fursa MD aliyopo anajiuzulu, wametangaza wameingia wazungu tatu, mhindi mmoja na Mtanzania mmoja, mtanzania kashinda kwenye mchakato baada ya kushinda kwa mujibu wa taratibu, wenzetu wanatakiwa kutuandikia Serikali tutoe consent yetu, consent tu tumekaa nalo, tunaangaika nalo na ni kwa roho mbaya tu, kashinda mtanzania, mtanzania akienda kwa faida ya nchi yetu anakwenda kuziangalia hisa zetu lakini tumeng’ang’ana nalo weee! Hivi angeshinda Mfaransa mngefanya vetting? Si mngetoa barua tu akaendelea ameshinda mtanzania roho mbaya mnambania ya nini na mkichelewa kujibu wataweka Mfaransa Watanzania hebu viongozi tuondoke kwenye roho mbaya, Mtanzania mwenzetu tumuunge mkono toweni consent ya Serikali aendelee, wamekaa wazungu wamemkubali sisi tunaweka roho mbaya hili jambo halikubaliki hii ni kwa TIPER. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa PUMA tuna hisa asilimia 50, Mheshimiwa Waziri tunaagiza mafuta hapa ya bulk kupitia PPPA lakini tunatangaza tender, wanaotuletea mafuta ni makampuni ya nje, hapa tuna kampuni yetu ya PUMA asilimia 50 ni Serikali yetu. Hivi ni kwanini tusiwatumie hawa hawa tukaagiza mafuta tukapata fedha lakini pia tukapata income tax kwa sababu hii kampuni iko hapa na sisi wenyewe Serikali tunapata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya sasa hivi tumewaachia makampuni ya nje ndiyo yanayoleta yakituletea tukishawalipa wanaondoka zao lakini na hakuna mtu hatatushangaa kampuni ya PUMA ni ya kwetu tuna hisa asilimia 50 lakini ina uwezo wa kufanya manunuzi ya kimataifa tuondoke kwenye kuangaika na hao twendeni tukaitumie kampuni yetu ya ndani tutapata fedha za ziada, tutapata mapato na mambo yetu yatakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, moja ninaunga mkono bajeti hii asilimia 100, bajeti safi twendeni tukaitekeleze na tumpe nafasi mama na waziri umefanya vizuri na naamini umeanza vizuri na baada ya muda uta-gain uzoefu wa kutosha utatupeleka mbele zaidi. Lakini kwenye financing ya miradi mikubwa twende kwenye credit rating itatutoa hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu twendeni tukaangalie matumizi ya hisa zetu kwenye makampuni yetu, na hizi hisa zetu zitatuongezea wigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza kuongeza wigo wa kodi siyo idadi tu ni pamoja na ubora ukiwaongezea uwezo wale ambao wanakulipa kodi alikuwa anakulipa Shilingi 10 ukimuongezea uwezo anakulipa mia 200, unakuwa umeongeza wigo na hapa ndipo ambapo tunaiomba Serikali yetu ienda, lakini vinginevyo mimi naunga mkono ninampongeza Rais, kwa bajeti hii amelegeza vyuma sana tumuunge mkono aendelee kulegeza ili mambo yetu yaende, style aliyokuja nayo twende nayo tusonge mbele pamoja ninaunga mkono bajeti kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)