Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Kilumbe Shabani Ng'enda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchukua nafasi hii kwanza, kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi. Pili, kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuamka salama na kuanza kufanya kazi za kutumikia tena Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote nitoe pongezi maalum za sura ya bajeti. Nasema za sura ya bajeti kwa sababu, kwa hakika bajeti hii imetudhihirishia mambo mawili makubwa. Kwanza, imetudhihirishia kwamba, Serikali hii ya CCM ni Serikali sikivu. Pili, imetudhihirishia kwamba, Serikali inayoongozwa na Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu ni Serikali ambayo imekusudia kabisa kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sifa hizi hazipatikani kwa kusema tu, zinapatikana kwa mambo tunayoyaona kwa sababu, Serikali sikivu inazo sifa zifuatazo: Moja ni Serikali inayowasikiliza wananchi; Pili, Serikali inayowasikiliza Wabunge; Tatu, Serikali inayoshaurika; Nne, Serikali ambayo ipo tayari kujikosoa; na Tano, Serikali inayotekeleza mambo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya mambo yakiwepo ndio unasema hii Serikali sikivu na katika bajeti hii unaweza ukayaona haya mambo katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, kitendo cha kupunguza faini za makosa ya barabarani kwa bajaji na bodaboda, kutoka Sh.30,000/= mpaka Sh.10,000/= ni kuwa Serikali hii ni sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kitendo cha kuhakikisha kwamba, katika bajeti hii posho za Waheshimiwa Madiwani, ambao ni wasaidizi wa karibu wa sisi Wabunge, zitakuwa zinalipwa sasa kutoka TAMISEMI badala ya Halmashauri zao. Hiki kitendo kinaonyesha Serikali hii ni sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kitendo cha kuweka posho maalum kwa Watendaji wa Kata na Makatibu Tarafa,


ili waweze kupata uwezo wa kuzifanya kazi zao vizuri, kinaonyesha Serikali hii ni sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, kitendo cha kuyatafutia ufumbuzi matatizo ya barabara zetu zinazosimamiwa na TARURA, maji na kushughulika na maboma ya shule zetu, haya yote yanaonyesha Serikali hii ni sikivu na kwamba, lazima tutoe pongezi maalum kwa Rais wetu na Serikali kwa ujumla, kuonyesha kweli kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, ningependa kuwatoa wasiwasi Wabunge wenzangu, hasa ambao wamekuwa na wasiwasi au wakiwa na maoni tofauti kuhusu kodi ya majengo, kwamba, itozwe wapi na mahali gani? Nataka niipongeze kabisa Serikali wamelenga, wametafuta mahali pazuri ambapo kodi itapatikana na ambapo hapawezi kuwa na maumivu kwa mtu mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri katika hili tukafahamu kwamba, kodi zote na hasa zilizo nyingi, lazima mwisho wake zilipwe na mtumiaji, maana hata ukisikia kodi imewekwa kwenye mafuta, unaweza ukafikiri analipa mwenye gari, si kweli hiyo. Mwenye gari ataenda kununua mafuta tu, lakini baadaye abiria akipanda gari hilo atalipa hiyo kodi ya mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kodi zote hatimaye hulipwa na mtumiaji kwa hiyo, kama nyumba imejengwa na mwenye nyumba yupo, aidha, anakaa kwenye nyumba hiyo ina umeme au hakai kwenye nyumba hiyo kuna mtu mwingine anakaa na huyo ndiye anayelipa kodi hiyo ya majengo, iko sahihi, wala hakuna tatizo lolote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni niliungana na Rais wetu, kushuhudia utiaji saini wa mikataba mitano kule Mwanza ya ujenzi wa meli ambazo zitatoa huduma na kuchochea uchumi katika Taifa letu. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi katika Ziwa Tanganyika ni wanufaika, maana kuna meli mbili; moja ya abiria ambayo itabeba abiria 600 na mizigo 400 ipo katika mkataba huu ambayo itaanza kujengwa; na nyingine ni ya mizigo. Hapa narudia kuipongeza Serikali, maana nimesema hapa Bungeni katika Mpango na hata katika Wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, nilisema kuhusu suala la kuhakikisha tunachangamkia fursa ya soko kubwa la DRC Congo. Kwa hiyo, meli hizi zitakuwa kichocheo kikubwa cha uchumi cha kufungua mlango na kuongeza wigo mkubwa wa biashara baina ya sisi na DRC Congo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mniruhusu vile vile baada ya kusema Serikali hii Sikivu, niwakumbushe mambo ambayo hamjayasikia vizuri. Maana ingekuwa ni binadamu ungeweza ukasema, kama mtu ana masikio mawili labda ungesemea sikio la kushoto, la kulia labda liliingia maji hakusikia vizuri. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia haya mambo, nimeshayasema na sasa nataka niyarudie. Uchumi wa nchi yetu unategemea sana uimara wa sekta binafsi. Sekta binafsi sasa hivi imebeba mizigo mikubwa miwili; tukiitua mizigo hii sekta binafsi itatusaidia sana katika kukuza uchumi. Mzigo wa kwanza ni riba za mabenki. Maana ilisababisha hapa mpaka nijiteue mwenyewe kuwa balozi wa kutetea riba za mabenki. Riba za mabenki endeleeni kulitazama jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mzigo wa pili ni ulipaji wa madeni ya Serikali kwa wakandarasi wa ndani. Nataka nikwambie, hali ni mbaya. Kuna watu sasa hivi hapa wakipiga simu napata shida kupokea. Mmojawapo ni mpiga kura wangu mmoja anaitwa Raymond Dabiegese, yupo kule Kigoma, anaidai TBA (Tanzania Building Agency). Amewa- supply vifaa, duka lenye thamani ya mtaji kama wa shilingi milioni 100, unakwenda kuchukua vifaa vya shilingi milioni 40, halafu unafika mahali miaka miwili hujalipa. Unamuua huyu mtu. (Makofi)


Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa kupitia nafasi hii niseme, tumesaini mikataba na hawa wakandarasi kwa ajili kutengeneza meli hizi. Naiomba Serikali ichukue tahadari sana katika kuwasimamia hao wakandarasi kufanya kazi zetu. Najua Serikali kabla ya kutoa kazi, inafanya kitu kinaitwa due diligence, kuangalia uwezo wa kitaaluma na kifedha wa haya makampuni kufanya kazi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa tunalo tatizo, kampuni iliyopewa kandarasi ya reli yetu ya kisasa, inakabiliwa na madeni makubwa ya wazabuni wa ndani wadogo iliyowapa kazi. Sijui hili kama mnalijua! Serikali inawalipa wao kwa wakati, lakini wao wale watu waliowa- sub-contract kazi ndogo ndogo hawawalipi. Sasa hivi wanadaiwa zaidi ya shilingi bilioni 14. Baadhi ya wadeni walikuwa hapa niliwaunganisha na Naibu Waziri wa Ujenzi ili waone jinsi ya kuwasiaidia. Ndugu zangu imetokea baadhi ya makampuni haya yamefanya kazi kwenye nchi nyingine yakamaliza mikataba yake, yakamaliza miradi, yakawaacha watu wa nchi hizo, Wakandarasi wadogo wadogo wa nchi hiyo, wazabuni wadogo wadogo wanadai madeni; nchi mojawapo ni Ethiopia. Wametekeleza miradi lakini wameacha makovu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali na hasa Hazina mnapotoa fedha, ikiwezekana hata katika mikataba yenu, hawa wakandarasi wa kutoka nje mnapowapa kazi, waoneshe wao wanaingia mikataba na wazabuni wadogo wadogo wa ndani ya nchi; mikataba ile mwenayo na mjue kama wale wazabuni wanaowapa, wanalipwa kwa wakati. Vinginevyo ninyi mnawalipa lakini wao hawawalipi. Hilo jambo litafika mahali litasaidia miradi kutekelezwa lakini litarudi tena kuwabebesha mizigo watu wa sekta binafsi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla nataka niseme kwamba sisi Wabunge naamini kama nilivyowasikia wenzangu wengi wanasema, tumeridhishwa sana na bajeti hii na kwa kweli napenda kutamka rasmi kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)