Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa nafasi ya kuchangia hoja hii. Nampongeza Rais wetu kwa bajeti hii nzuri, pia nawapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu wake pamoja na Watendaji wote wa Wizara husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita kwenye kushauri. Nilikuwa naangalia hizi sekta zetu za kiuchumi na mchango wake katika pato la Taifa. Ukizipitia zote, kwa kweli bado tunayo kazi kubwa ya kufanya. Ukiangalia kilimo kinachangia asilimia 26.9 kama takwimu zangu ziko sahihi; fedha na bima zinachangia asilimia 3.5; madini asilimia 6.9; viwanda asilimia 8.4; umeme asilimia 0.3; ujenzi asilimia 14.4; uchukuzi asilimia 7.5; na biashara asilimia 8.7. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia jiografia ya nchi yetu, mimi nadhani sekta nyingi kwa kweli tuko chini pasipo sababu yoyote ya msingi. Kwa mfano uchukuzi, kwa jiografia ya nchi yetu, bandari zetu, nchi tunazopakana nazo, napenda kumshauri Mheshimiwa Waziri, tujipe mkakati wa kukatisha baadhi ya sekta mchango wake katika pato la Taifa uende zaidi ya asilimia 10. Tupende tusipende lazima tuwe na mkakati wa namna hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sekta ya uchukuzi tuna viwanja vyetu vya ndege, lakini kanda ya ziwa tuna uwanja wa ndege wa Mwanza. Zamani mazao ya uvuvi yalikuwa yanasafirishwa kwa ndege kutoka uwanja wa ndege wa Mwanza kwenda nchi za nje, lakini hivi sasa tunavyoongea, mazao yote ya uvuvi ili yaende kwenye masoko ya nje, lazima tuyasafirishe kwa malori tuyapeleke Entebe au Nairobi. Ukijiuliza, kwa nini mazao yetu ya uvuvi yaende Entebe au Nairobi? Hatuna sababu yoyote ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani uwanja wetu wa ndege haukuwa na facility ya kuhifadhi hii minofu ya Samaki, lakini hivi tunavyoongea, Serikali yetu kupitia TAA wamejenga facility nzuri sana ambayo ukilinganisha na nchi jirani actually facility tuliyonayo pale Mwanza ni nzuri na bora kuliko facility zote za Afrika Mashariki na Afrika ya Kati. Tatizo tulilonalo, hatujaisajili kupata FOB Mwanza na ndiyo maana mashirika ya ndege kama Air Rwanda walipojaribu kusafirisha minofu yetu ya samaki kutoka Mwanza, wameshindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, kwa kuwa tumeshawekeza pesa yetu pale Mwanza, tumejenga facility, tutafute registration, tupate FOB Mwanza ili mazao yetu ya uvuvi yasafirishwe moja kwa moja kutoka Mwanza kwenda nchi za nje. Hii kwanza itaongeza chachu kubwa ya kuwekeza viwanda hapo Mwanza au Kanda ya Ziwa. Pili, zile pesa ambazo tunazilipa Entebe na Nairobi zitabaki kwenye nchi yetu, tutaongeza pato kwa sekta ya uchukuzi na sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni kuhusu kilimo. Ukiangalia sekta ya kilimo, mchango wake ni mdogo. Wachangiaji wengi wamesema hapa, tuna vijana wengi huko mitaani hawana kazi, lakini hawawezi kwenda kwenye kilimo kwa sababu ukiwaambia wanasema hawana mitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, jeshi letu kitengo cha JKT wanafanya vizuri sana kwenye kilimo. Nashauri tuwaongezee pesa wakajikite kwenye kuzalisha mazao ya kilimo. Kwa sababu wana uwezo, watazalisha, watayaongezea thamani na wanaweza kupata masoko kirahisi kuliko mkulima mmoja mmoja. Hata kilimo ambacho tunakizalisha, hapa tunaongea lakini nadhani hatuna mkakati wa madhubuti kuhakikisha kwamba tunaongeza tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu Kagera tunazalisha kahawa. Tumepiga kelele sana hapa, tumesema hebu ruhusuni wafanyabiashara wakanunue hizi kahawa. Kuna watu wamewekeza kwenye viwanda pale, lakini tunawawekea figisufigisu hatuwapatii vibali. Msimu wa kahawa ulianza mwezi wa Nne, lakini tunavyoongea leo, vyama vyetu vya msingi havijafungua masoko, hata wafanyabiashara binafsi ambao wangenunua kahawa, hawajapewa vibali. Ukijiuliza wakati mwingine, tunadhamiria nini? Tunalenga kufanya nini? Ndiyo maana sekta nyingi kama hizi kutokana na kanuni zetu tulizojiwekea, hatufanyi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwamba hizi posho ambazo walikuwa wanalipwa Madiwani sasa Serikali inazibeba. Hata hivyo nikiangalia hizi posho zao hawa Madiwani wenzetu, pamoja na kwamba naishukuru Serikali kwamba imezibeba, itazilipa kwa wakati, lakini tuziangalie hizo posho, bado ni kidogo mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Madiwani wenzetu ndio tunawaachia majimbo yetu, ndio wanafanya kazi kwenye kata zetu, ndio wanafanya kazi ya kuhamasisha kukusanya mapato ya Halmashauri zetu. Napendekeza kwamba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja yake, tuiangalie hii posho ya Madiwani, tuwaongezee angalau kidogo nao wakajisikie na wakafurahie kazi wanayoifanya huko kwenye Halmashauri zetu na waweze kutulindia majimbo yetu ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa posho zilizopendekezwa kwa ajili ya Watendaji wa Kata na Maafisa Tarafa. Nawashukuru sana. Hata hivyo, kuna kundi ambalo tumelisahau; kundi la wazee. Nimefurahi kule upande wa pili wa nchi yetu, Zanzibar wanawalipa wazee posho ya shilingi 25,000/= kila mwezi; wanafanya vizuri. Ila kwa upande wa Tanzania Bara tuna makundi ya watu wenye mahitaji maalum; tunaongelea watoto, wanawake na vijana ambao wanapewa mikopo, lakini tumesahau hili kundi muhimu la wazee na ambalo katika maisha yao wamelitumikia Taifa hili na kwa kweli wanaishi kwa kusononeka, baada ya kuingia kwenye hili kundi la wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yetu na tujuwe kila mmoja wetu tunaelekea kwenye uzee, tuwatengee na wenyewe posho kidogo ambayo itawapatia furaha katika maisha yao. Hii inawezekana. Baadhi ya taasisi kwa mfano ninakotoka kwenye jimbo langu, kuna NGO tu; kuna mzee mmoja Mswisi, ameishi pale zaidi ya miaka 10. Aliamua yeye kwa pesa yake kuwaletea raha wazee wenzake, kila mwezi anatumia zaidi ya shilingi milioni 16 kuwapa posho hawa wazee. Anawalipa posho zaidi ya wazee 1,000; na kwa mwaka anatumia zaidi ya shilingi milioni 195 kwa pesa yake na pesa ambayo anaitafuta nje. Huyu mzee amekaa hapa muda mrefu sana, lakini alijaribu hata kuomba na uraia tukamnyima. Naona Waziri wa Mambo ya Ndani yuko hapa. Huyu mzee amefanya mambo mengi mazuri na anawasaidia wazee na anawapa raha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaposema kuwalipa posho wazee siyo suala la pesa unawalipa kiasi gani? Kinachofanyika ni kwamba, wanajiona wamethaminika, wanajiona wanapendwa, wanajiona wana thamani katika nchi yao, hata tukiamua tuwepe shilingi 10,000/= tu, watafurahi, wataishi maisha marefu zaidi na watafurahia nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili tuliangalie, tulitafakari na tulitathmini. Sasa hivi wazee tunasema ni wachache lakini tuendako zaidi ya miaka 10 ijayo, wazee tutakuwa wengi, tunazidi kuongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga hoja mkono, nakushukuru sana. (Makofi)