Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ili nichangie bajeti iliyopo mbele yetu. Nikushukuru wewe na pia nielekeze shukrani zangu za dhati au pongezi zangu kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote waliomo kwenye Wizara hii, kwa kweli kazi wanayofanya mwaka huu imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pongezi za dhati ziende kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan, kwa namna ya aliyoweza kujibu hoja za wananchi mbalimbali kupitia kwa Wabunge wetu kwenye bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini watu wanaisifia hii bajeti, kwamba kama kumbukumbu zetu zipo vizuri huko nyuma bajeti kuu ilianza kusomwa kabla ya bajeti za kisekta, lakini Serikali ya Chama Mapinduzi ilikuja kubadilisha ule utaratibu, ili kukidhi matakwa haya ambayo yamekuja na bajeti hii, kwamba bajeti za kisekta yale tuliyoyachangia yote ndio yamekusanywa, yameingizwa kwenye bajeti hii. Tunawapongeza sana, tunawapongeza kwamba bajeti imekwenda kujibu hoja za Wabunge na kujibu hoja za Wabunge maana yake ni kwenda kujibu hoja za wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa zaidi kwenye bajeti hii tunakwenda kujibu masuala ya afya, elimu, maji, umeme na mambo kama hayo. Kuna jambo moja naomba niliongeze kwenye bajeti hii limesahaulika. Tunalo jambo linalozungumzwa kwa jumla ya uhifadhi wa wanyamapori, lakini hapa tumesahau jambo moja kwamba wananchi wale wanaozungukwa na hifadhi za wanyamapori, wanayaonaje matunda ya moja kwa moja kwa kuwepo kwao kwenye hifadhi. Maana leo tunaweza kuzungumza kwamba hifadhi ina faida kwa inaongeza watalii, na mambo mengine kama hayo ya kuinua uchumi, lakini hayo ni mambo ya mbali sana ambayo yanahitaji elimu kubwa kuyaelewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali waende waimarishe WMAs, hapo ndipo wamesahau kwa sababu zile WMAs, wananchi wanahifadhi kwa WMAs ni kwamba wanapopata mapato yao wanajenga shule, madarasa, vyoo. Kwa hiyo wananchi wale wanaozungukwa na hifadhi wanapata ile pinch ya moja kwa moja kwamba kumbe kutokana na hawa wanyama tunapata faida hizi, kuliko hizo ambazo tunatakiwa Wabunge twende tukajieleza, Waziri aje aeleze. Hivyo, kama Serikali wangeimarisha WMAs kwenye maeneo yetu, wananchi wangeweza kupata faida ya moja kwa moja kwa wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo kwenye WMAs naiomba sana Serikali, kumekuwa na kigugumizi kikubwa sana hata pale ambapo vitalu vya WMAs wakapata wawekezaji, bado yale mafao yao yanakuja kwa kuchelewa sana. Kwa hiyo sasa tunapokwenda kuzunguka kule, wananchi wetu wanapohama mashambani kurudi baada ya kukosa mazao yao, kuliwa na tembo na wanyama wengine wanakosa nini cha kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba sana sana, naiomba Serikali, iimarishe WMAs, na kuimarisha WMAs maana yake nini? Kuwasaidia hata kuwatafuta wawekezaji kwenye vile vitalu, vile vile kuvitangaza, unawaachia WMAs watangaze vile vitalu vyao, uwezo wao wa kutangaza ni mdogo sana. Naiomba Serikali kupitia Maliasili waendelee na wao kuitangaza vile vivutio, ambavyo kwenye vile vitalu vinanyomilikiwa na WMAs.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ambalo naweza kuishauri Serikali katika kuboresha hii bajeti yetu. Jana nimeuliza swali hapa kuhusiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuendelea kufanya upembuzi yakinifu wa barabara mbalimbali nchini. Zipo barabara zimefanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2012, mpaka leo tunatafuta fedha kwa ajili ya kwenda kujenga. Mfano mmojawapo, kuna barabara yetu ya Nachingwea-Masasi, barabara ya Nachingwea – Liwale, barabara ambazo zimefanyiwa upembuzi yakinifu kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini basi Serikali isifikirie sasa isitishe kwanza kuendelea kufanya upembuzi yakinifu ili barabara zile ambazo tayari zimeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, iweze kupata fedha kwa ajili ya kuzijenga. Jambo hili Serikali imelifanya, mwaka huu imepunguza kujenga vituo vya afya, imepunguza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya kwa sababu gani, wapate fedha za kupata vifaa za kumalizia zile hospitali. Naomba na huku kwenye upembuzi yakinifu wafanyeni hivyo, kwamba wajiridhishe barabara ngapi tumeshazifanyia upembuzi yakinifu, zinahitaji fedha ngapi kuzijenga, basi wakasitisha, wakaacha kufanya upembuzi yakinifu kwa barabara zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ndio mambo niliona kwamba nije kuwashauri kwa maana kwamba, niwashauri ili waone kwamba wanaweza kupoteza fedha nyingi sana za Serikali. Kwa mfano, nafahamu barabara ambayo imefanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 2012, tutakapokwenda kuijenga mwaka 2025 hatutaijenga kwa data zile za mwaka 2012. Kitakachofanyika ni building and design, tunapoteza nyingi. Kwa hiyo nashauri jambo hilo dogo sana walifanye kama ambavyo wamefanya katika sekta zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naisifu sana Serikali, tulichangia hapa kutafuta fedha za TARURA, kutafuta fedha za maji vijijini, jambo hili wamekuja nalo vizuri sana, wamekuja kutwambia wameongeza Sh.100 kwenye mafuta; wameongeza tozo kwenye miamala ya simu, jambo zuri, lakini vile vile kwenye line ya simu ni jambo zuri. Hizo fedha mpaka leo tunamwomba Mheshimiwa Waziri, hebu ziwe ring fenced tuzione, kwa sababu zile zilivyo wazi wazi hivi, hazieleweki, haiwezi kuwa sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu zile Sh.100 tuzione moja kwa moja kwamba zile fedha zinakwenda TARURA na hata pale unapoweka mafuta zinaonekana kabisa kwamba imekatwa shilingi kadhaa zimekwenda TARURA kama zilivyo kwenye REA. Leo ukinunua mafuta kwenye REA unaona kabisa kama kuna shilingi kadhaa imeenda REA. Unapofanya muamala kwa simu unaona kabisa kuna shilingi kadhaa zimeenda kwenye REA, tunataka tuone fedha ya mafuta inakwenda moja kwa moja TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile na zile za kwenye miamala ya simu, tunapofanya miamala ya simu, tuone kwamba hii shilingi kumi imekwenda moja kwa moja kwenye maji vijijini (RUWASA)….

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Hapo ndiyo tutakuwa tumeona vizuri, hiyo ndiyo ring fence ambayo nashauri iwekwe, kwa sababu inaweza kutokea….

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Baba yangu anachangia vizuri sana yaani pesa zikifanyiwa vizuri hesabu za mafuta pamoja na kwenye simu zikaenda mahali husika, Taifa hili tutakuwa hatuna shida tena ya barabara. Ahsante sana, nilikuwa nataka nimpe taarifa hiyo tu.(Makofi/Kicheko)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kama nilivyosema, nilianza kwenye miamala ya simu iende RUWASA na hii ya laini iende maji vijijini, hapo tutakuwa tumefanikiwa, kwa maana kwamba hela ya mafuta inaenda TARURA, hela ya miamala inaenda RUWASA, na hela ya laini inakwenda maji mijini. Huo ndio mchango wangu kwenye bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, mimi ni miongoni mwa Kanda ya Kusini, kwa hiyo kukaa bila ya kuizungumzia korosho nitakuwa sijafanya sawasawa. Nataka niambie Serikali, mazao yote hakuna zao lenye export levy isipokuwa korosho. Lazima tujiulize imetokana na nini hii export levy kwenye korosho. Hii imetokana na kikao cha wadau wa korosho. Walipokaa wadau wa korosho wakasema sisi hili zao za korosho lisiendelee kudumaa tufanye nini? Tukaweka fedha kwenye export levy ili ziweze kurejea kwenye korosho, lakini Serikali baada ya kuona zile fedha ni nyingi na ni tamu wakazihamisha zote wamebebea.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo kwenye kikao cha wadau wa korosho cha mwaka 2020 tumetoa kwa mkulima shilingi 25/= kwenye kila kilo kwa ajili ya kupeleka Naliendele kwenye Chuo cha Utafiti. Tumetoa shilingi 25/= kwenye kila kilo, tumepeleka kwenye Bodi ya Korosho ili Bodi ya Korosho iweze kusimamia zao la korosho. Sasa Muone hii mizigo yote inarudi kwa mkulima. Tunaomba Export Levy irudi kwenye zao la korosho, hata kama siyo hundred percent, lakini mhakikishe angalau hata 50 au 60 zirudi kwenye korosho, vinginevyo zao hili linakwenda kupotea. Nawaomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho siyo kwa umuhimu, naomba kuishauri Serikali, tujiondoe kwenye kufanya biashara; tusimamie, tuimarishe Sekta Binafsi. Hatuwezi kuimarisha Sekta Binafsi kama na Serikali nayo itakuwa na taasisi zake zinatamani kufanya biashara. Taasisi zile ambazo zimepewa kusimamia sekta mbalimbali, zenyewe ziwe kama regulator. Siziwe na zenyewe zinafanya biashara, tunakwenda kuharibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mfano, kuna taasisi moja ya TASAC, kazi yao ilikuwa ni ku-regulate biashara pale bandari, lakini nao pamoja na kwamba tuliwaambia wapitishe zile nyaraka za Serikali tu, leo hata ngano pale kwa Bakhresa wanachukua TASAC. Tunawashauri, tunaomba Serikali, kama tunataka kuimarisha uchumi wa nchi yetu, lazima watu binafsi tuwabebe. Sekta binafsi lazima tuibebe. Tutafute namna yoyote tunavyoweza, Sekta Binafsi ipate nafasi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nakushukuru sana. Huo ndiyo ulikuwa mchango wangu kwa leo. (Makofi)