Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuibadilisha historia ya Tanzania kwa kuwa Rais wa kwanza Mwanamke katika nchi yetu, pia nimpongeze Mama yetu kwa kutuletea bajeti ya kihistoria, bajeti ya mwanamke katika Taifa letu la Tanzania. Kule Kilimanjaro wanasema bajeti hii ina mshiko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Mawaziri, nimpongeze Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na Watendaji wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi nianze kuchangia katika Sekta ya Nishati. Nimpongeze Rais wetu kwa kusikiliza kilio cha Watanzania wengi ambao Wawakilishi wao ambao ni Wabunge wakaja kulia kilio hiki katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu suala la zima la umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa kutoa tozo la nguzo la umeme kuanzia shilingi 327,000 hadi 27,000, Tanzania bila giza inawezekana. Wote tunaelewa kwamba umeme ndiyo chachu ya maendeleo, Tanzania bila umeme hakuna Tanzania ya Viwanda, vijana wetu wengi wamefanya kazi nyingi sana katika nchi hii lakini mara nyingi sana wamekuwa wakikimbilia mijini kwenda kutafuta ajira. Baada ya Sera ya umeme vijijini vijana wengi wamepata ajira katika vijiji, wamejiajiri na hata wengine wameajiri wenzao tuipongeze Serikali katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tunao wanawake wengi ambao wanajishirikisha katika biashara za mama lishe, wanawake hawa nao wamefaidi umeme vijijini kwa kuwa wameweza kutengeneza mazingira ya kuboresha biashara zao kama vile kutengeneza juisi na hata kuwa na friji kwa ajili ya kuhifadhi vyakula vyao. Niipongeze sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuipongeza Serikali kupitia nishati nije suala zima la Madiwani. Wote tunatambua kwamba Madiwani wana kazi nyingi sana katika Kata zao nani wawakilishi wetu ambao wanafanya kazi nyingi sana katika maeneo yao. Niipongeze Serikali kupitia Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kusikiliza kilio cha Madiwani ambao sasa fedha zao zitakuwa zinatoka Serikali Kuu badala ya Halmashauri zao. Hii itawaletea nguvu sana kwa kuwa watakuwa wanapata fedha zao kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi niiombe Serikali yangu sikivu tunatambua kazi nyingi wanazozifanya Madiwani katika maeneo yao ikitokea misiba wataombwa majeneza, ikitokea shughuli wataombwa hiki na kile, kukiwa na wagonjwa wataombwa usafiri ni hela hizi hizi, posho hii hii ambayo ndiyo wanayoitumia. Niiombe Serikali yako sikivu iwaongezee posho Madiwani hawa, naungana na wenzangu wote waliochangia hili kwamba ni vizuri Serikali ikawatazama sasa na wao waweze kuongezewa posho ili angalau waweze kuendesha shughuli zao vizuri na kwa amani katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije suala la TARURA, niipongeze Serikali Wabunge wengi sana hasa wa Majimbo wamekuwa wakilia kilio cha TARURA humu ndani tukiwepo na sisi wanawake wa Viti Maalum. Wengi wameongea mengi kuhusu suala la barabara, bila barabara hakuna maendeleo, wakulima kilimo kinahitaji barabara, wananchi wenyewe tunahitaji barabara, wameongea wengi wakasema kwamba hata akina mama wengine wakati wakijifungua wanajifungulia njiani kwa sababu ya barabara zetu kuwa mbovu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uongozi wa mwanamke siku zote mwanamke huwa anaangalia mtoto analia nini, mama ameweza kuangalia nini watanzania wanacholilia akajaribu kuleta bajeti hii katika Bunge hili ambalo kila Mbunge amefurahia bajeti hii na kwa kupitia Bunge hili Watanzania wengi kila mtu amefarijika na bajeti hii. Niseme kwamba tozo kwa ajili ya barabara ya TARURA ambayo zaidi ya shilingi milioni 222 zikipatikana nakutekeleza malengo kama ilivyokusudiwa naamini kwamba 2021/2022 ifikapo mwishoni tutakuwa barabara zetu zote zinapitika kipindi chote cha mwaka. Niiombe Serikali ipeleke pesa hizi zikafanye kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo mimi niunge mkono hoja. Nasema ahsante sana kwa bajeti hii nzuri. (Makofi)