Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nitumie nafasi hii awali ya yote kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Phillip Isdor Mpango, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu ya usikivu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwani bajeti hii kwa sehemu kubwa imechukua mawazo yetu sisi Wabunge wakati tunachangia Mpango wa Taifa wa 2021/2022 - 2025/2026. Yote ambayo yameletwa mbele yetu ni yale ambayo sisi tumeyaweka Mezani. Bajeti hii ni ya kwetu sisi Wabunge wa Bunge hili la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri, mtani wangu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Naibu wake na wataalam wote kwa jinsi walivyochakata yale mawazo yetu tuliyoyaweka kitaalam na kuakisi mahitaji halisi ya Watanzania kwa wakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulilalamikia sana eneo la fedha ndogo inayopelekwa TARURA ili iweze kuhudumia barabara zetu za vijijini. Eneo hilo limeangaliwa vizuri sana. Tulikuwa tunalia vyanzo vingine vipatikane ili tupate fedha zaidi; hilo limeangaliwa, lakini zaidi sana tumepewa shilingi milioni 500 kwa kila jimbo. Huu ni usikivu wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelia sana eneo la maji. Wakati wa kampeni sisi Hanang hatukuwa na ajenda nyingine; ajenda ya kwanza kwetu sisi ilikuwa maji, ya pili ilikuwa maji na ya tatu ilikuwa maji. Eneo hilo nalo limeangaliwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa tuna changamoto bado zipo, naamini nalo litakwenda kukamilishwa vizuri kwani wapo watu wataalam, wabunifu ambao wanaipenda kazi yao na wanaifanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la umeme; wakati tunajinadi ili tupate kura tulikuwa tunafanya reference ya jinsi umeme ulivyokwenda vijijini kupitia REA, lakini kabla ya bajeti ya Nishati kusomwa tulipewa jinsi wakandarasi watakavyokwenda kutekeleza miradi mbalimbali ya REA kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwenye eneo hili, kwamba ni nyeti zaidi, bado kuna maeneo mengi hatuna umeme. Tunatarajia kukusanya fedha kwenye eneo la kodi za nyumba, kwenye LUKU na hasa kuwapelekea watu wengi zaidi, wapate umeme ili tupate kodi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango ambao tumepelekewa wa nyumba 20 na kuendelea kwenye vijiji vyetu hautatusaidia sana kukusanya kodi za kutosha kwenye kodi za nyumba. Tupeleke umeme kwa watu wengi zaidi ili tupate kodi zaidi kwenye nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hilo pia nashauri sana tuwashirikishe na viongozi wa chini ili tuwaangalie watu tunaowachaji ni watu halisi ambao wanapaswa kulipa kodi. Inaweza ikatokea kwamba tunapeleka kodi kwenye nyumba na nyumba zina wapangaji. Nao ndio wameanza kulalamika kwenye mitandao ya kijamii, kwamba wao hawamiliki nyumba lakini wanapelekewa kodi. Eneo hilo tuwashirikishe viongozi wa chini kwa sababu Serikali ipo mpaka chini. Tuwatambue wale Wenyeviti wa Vitongoji, Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji, tuwatambue na wenzetu walioko kwenye Kata ili tuwashirikishe vizuri wanaofahamu maeneo hayo vizuri ili tukusanye kodi bila kuleta kelele kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wanahanang ni wakulima na wafugaji. Naishukuru sana Serikali yetu ya Awamu ya Sita, eneo la kilimo imeliangalia vizuri sana. Sisi tunategemea kilimo cha ngano na kilimo cha alizeti; maeneo haya yote yameangaliwa vizuri. Naomba mwendo huo twende nao ili angalau wananchi wetu waendelee kunufaika, tupate manufaa kwenye kilimo tunachokilima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliongea sana wakati wa nyuma kuhusu mwekezaji ambaye tunaye kwenye shamba lile lililokuwa la NAFCO zamani, kwamba tupate mwekezaji ambaye yuko makini; naona juhudi zinaonekana, kazi zinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la mifugo wafugaji wanachohitaji, mifugo yao tuwasaidie kitaaluma. Tuboreshe mifugo, tujenge majosho na malambo, tupeleke chanjo na dawa za uhakika ili hatimaye waweze kufuga kisasa na tupate tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeongelewa mara nyingi sana; maeneo kwa sasa yamekuwa finyu, Serikali iache kufuga. Serikali iache kuchunga ng’ombe. Kazi ya kuchunga watuachie sisi ambao tuna uzoefu wa kuchunga. Yale maeneo, Ranchi za Serikali zile wapewe watu ambao wana asili ya ufugaji, watu wenye nia ya kufuga, ili tupate tija ya kutosha kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naomba niongelee kidogo eneo la utafiti. Mara zote tumekuwa tukisema kama hujafanya utafiti huna haki ya kusema. Sisi tuna mashirika yetu; TIRDO, TEMDO na CAMARTEC. Ili haya mashirika yaweze kutusaidia, Kamati imesema fedha ambazo wametengewa, bilioni 3.5, ni kidogo sana na ni kweli ni kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatutawekeza kwenye utafiti maana yake tutategemea fedha za wafadhili na mfadhili akileta fedha zake maana yake atataka yale anayoyataka yeye ndiyo yasemwe. Serikali iamue sasa kuwekeza kwenye eneo la utafiti ili utafiti utakaofanyika uwe kwa manufaa yetu sisi na uweze kutusaidia katika kutatua changamoto tulizonazo sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na eneo la ardhi. Kwenye eneo la ardhi tumekuwa tukiongea suala la kupima ardhi yote ya Tanzania ili angalau tuweze kupata mapato kwenye ardhi, lakini unakuta kuna ardhi maeneo mengine tumeyapima tumemilikisha watu. Baada ya kumilikisha ardhi ile utakuta ina kodi zaidi ya miaka 10, 15 haijawahi kulipiwa. Ina malimbikizo kibao, mtu yule akitaka kuuza ardhi ile hawezi kuuza kwa sababu tayari ina madeni ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba tuangalie eneo hilo; je, yale madeni ambayo tunayo katika ile ardhi tuyatafutie namna, ama kufuta yale madeni ili tuanze upya, tuwape watu wapya ambao wako serious na kuendeleza yale maeneo ambayo tumewapatia watu. Au vinginevyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango wako mzuri.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)