Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi jioni hii na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhana Wataala aliyeniwezesha kusimama leo hii na kuwa Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini, nimshukuru kipekee Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kukubali hisia za Wabunge wengi ambacho ndicho kilikuwa kilio cha muda mrefu kuanzia Bunge la Kumi na Moja na Bunge hili la Kumi na Mbili kuhusu suala la maji pamoja na TARURA nashurkuru sana, naamini ametoa heshima kwa Wabunge leo tunajisikia furaha sana, kuona namana ambavyo Rais ameyachukua yale yote ambayo tulikuwa tulikuwa tunayazungumzia katika kipindi chote na kuyaweka katika bajeti na katika utekelezaji halisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kuchambua bajeti hii kwa makusanyo yaliyopita ya Mwaka 2020/ 2021niwapongeze sana Wizara ya Fedha na wale wote waliohusika kukusanya fedha kwa kutumia mipango mbalimbali na kufikia asilimia 86 ya makusanyo yetu ya bajeti iliyopita. Kwa kweli hili jambo ni likubwa tunatakiwa tuwape pongezi hasa Wizara ya Fedha na wengine wote kwenye idara mbalimbali waliohakikisha kwamba fedha hizi asilimia 86 ya makisio ya Mwaka wa Fedha 2020/2021 yamefikiwa naomba sana Jambo hili tuliangalie na tuwape moyo hawa watu waendelee kufanya vuzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo nikirejea kwenye bajeti zilizopita za kisekta za Wizara mbalimbali sioni reflation hii ya asilimia 86 kwenye shughuli za maendeleo katika Wizara zingine, inaonekana kwamba kuna Wizara ambazo zimepata fedha za maendeleo chini ya asilimia 30 ambacho kwa kweli kwa hali ya kawaida hawasemi lakini inaonekana kama kuna Wizara zimekuwa ni muhimu zaidi kuliko Wizara zingine kwa kupewa fedha ya maendeleo ambayo iko chini ya asilimia 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama makusanyo yamekua asilimia 86 kwa tuliosoma hesabu tulitegemea na shughuli za maendeleo kwenye Wizara mbalimbali zifikie zaidi ya asilimia 50 lakini haikuwa hivyo, ina maana kwamba kuna Wizara ambazo zimependelewa zaidi kwa makisio yake kutekelezwa ya maendeleo zaidi kuliko vile ambavyo vimekisiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwa hali ilivyokuwa kwa miezi miwili iliyobaki makusanyo yanaweza yakafika asilimia 90 au 92 kwa mwenendo huu, kwa hiyo naomba zile Wizara ambazo hazijafikia angalau asilimia 50 nazo ziangaliwe zipewe fedha za maendeleo ili haja ile ya mipango yao iweze kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia na hili kuna jambo lingine naomba Wizara nalo uliangalie kwenye miradi hii ya maendeleo nashukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa milioni 500 kwa kila Jimbo. Siku zote huwa tunazungumza majimbo yetu yanatofautiana wote tuna furaha kila Jimbo limepata milioni 500, lakini kwa maeneo mengine ni kilio! Kwa sababu hiyo milioni 500 namna ya kuitumia na kilometa tulizo nazo ni kizungumkuti, tunaona kwamba hili jambo mlione mbele ya safari mnavyogawa hivi vipaumbele vya maendeleo angalieni na ukubwa wa Majimbo kama tunavyolia siku zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ugawaji wa fedha za majengo, majengo ya zahanati, shule za msingi na sekondari ni vizuri basi muangalie na ukubwa wa majimbo, wingi wa shule na Kata jinsi ilivyo kubwa ratio ni muhimu sana. Kwa sababu inaonekana mwisho wa siku kuna Majimbo yataenda mbele Zaidi kuliko Majimbo mengine kutokana na ukubwa wa Majimbo ulivyo. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri wakati unagawa mipango hii ya miradi muangalie na ukubwa wa Majimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano; Tunduru tuna Kata 39 Jimbo langu lina Kata 15 napata shule moja, mwingine ana Kata Nane anapata shule moja, hayo majengo kila mmoja anapata matano matano ina maana mwenye kata nane atamaliza mapema kujenga majengo kuliko wenye Kata 15 na 39. Kwa maana hiyo tunaomba ratios iangaliwe wakati wa kugawa miradi ya maendeleo ili kila mmoja afikie ile standard ambayo inatkiwa kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sana kulizungumza suala la kilimo, kwa watu wa Kusini, kilimo cha Korosho ni uti wa mgongo. Mkutano wa 18 uliona sakata la korosho lilivyokuwa, natamani sana ile sheria ya export levy iangaliwe upya ili kuhakikisha kwamba aidha ifutwe ili kile kiwango kinachotozwa kwenye export levy ambacho ni sehemu ya gharama ya nunuzi kirudi kwa mkulima au irudishwe yale yote yaliyokubaliwa na wadau na kuanzisha export levy basi yafuatiliwe ili sekta ya korosho iweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili mwaka 2018 lilipotokea uzalishaji wa korosho umeshuka kwa asilimia kubwa. Mara ya mwisho tumezalisha tani 330,000, lakini msimu uliopita tumepata tani 206,000 ni kwa sababu kwamba yale yote ambayo yalikuweko kwenye export levy yalitakiwa yarudi kwenye kutekeleza sera ile ya Bodi ya Korosho na makubaliano ya wakulima pamoja na wadau wa korosho hayakuweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ahadi ya Serikali kwamba yote yale Serikali itatekeleza lakini kwa masikitiko makubwa napenda kusema ndani ya miaka mitatu misimu mitatu, Serikali imetoa bilioni tatu kwenye kituo cha Naliendele na bilioni 10 kwa ajili ya kununua sulphur, yale mengine yote hayakuweza kutekelezeka.

Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie kwa namna moja aidha wafute export levy kwenye korosho kwa sababu hakuna zao lingine lolote la biashara ambalo linatozwa export levy, hii tulianzisha wenyewe kwa ajili ya kuona namna ambavyo zao letu la korosho linadumaa na tukaanzisha ili kutafuta fedha la kusaida zao liweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyeikiti, jambo hili kwa kweli Serikali inahangaika sana inatafuta kila aina, nawaonea huruma Wizara ya Kilimo wanatafuta kila aina na sasa hivi kuna mgogoro wa sulphur huko kwa sababu wakulima wetu wameshindwa kupata sulphur ili waweze kuhudumia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa nizungumzie ni suala la hili property tax. Niishukuru Serikali na niipongeze Serikali kwa kubuni jambo hili, lakini kuna changamoto ambazo mnatakiwa mzifanyie kazi hasa tunaotoka Majimbo ya Vijijini, Naibu Waziri wetu wa Nishati anasema wekeni umeme hata kwenye nyumba za matembe. Leo nyumba nyingi za matembe zina umeme, zina Luku tuna zi-charge shilingi 1,000 maana yake tunaongeza gharama kwenye zile nyumba za tembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wakati wa utekelezaji muangalie hizi nyumba ambazo kwa kweli hadhi yake hazistahili kulipa hii property tax kwa kutumia LUKU na hasa zile nyumba za ibada. Nyumba za ibada ni kweli vijijini zina umeme lakini hizo ni nyumba za ibada kwa hiyo mfanye chini juu muweze kutambua nyumba hizi za ibada mtambue nyumba hizi za matembe ambazo hazistahili kulipa hii property tax ili kuleta maendeleo kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka kuzungumza suala la Linganga na Mchuchuma. Namshukuru Rais ametoa mwanga wa kuendelea na mradi huu wa Linganga na Mchuchuma. Kwenye Linganga kwa maana ya makaa ya mawe kuna matatizo, naomba turejee mkataba ule, turejee sheria mpya ya Madini, Ngaka pale tunachima madini ya makaa ya mawe, lakini Serikali haipati chochote, hata NDC yenyewe hawapati chochote kutokana jinsi mikataba ilivyokaa na hawa wawekezaji ambao tumeingia nao mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili Serikali ifanyie kazi ipitie ile mikataba yote Ngaka, ipitie mikataba ya Kiwira, ipitie mikataba ya Mchuchuma ili kuhakikisha kwamba Serikali inapata mapato kutokana na makaa ya mawe ili kuendeleza nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)