Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Serikali ya mwaka 2021/2022. Kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi leo kuwepo hapa kwenye Bunge lako Tukufu. Vile vile naomba nichukue nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa utendaji wake mzuri uliotukuka ambao anasimamia na kuhakikisha kwamba kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile nichukue nafasi hii nimpongeze Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kutupa shilingi milioni 500 kila jimbo kwa ajili ya kuondoa changamoto au kupunguza changamoto kwenye barabara zetu kupitia TARURA. Kwa kweli naomba nimpongeze sana.

Naomba nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu wake Engineer Masauni, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kuandaa taarifa ya bajeti ya mwaka 2021/2022 ambayo imetuonesha kwamba inajibu changamoto zinazotukabili katika maeneo mbalimbali hasa kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Daniel Sillo, Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Makamu wa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kigua pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ya Bajeti kwa maandalizi mazuri ya taarifa na kwa kushirikiana bega kwa bega na Wizara ya Fedha kuandaa na kukamilisha bajeti ya mwaka 2021/2022. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwapongeze Mawaziri kupitia Wizara zote na Manaibu pamoja na Makatibu Wakuu kwa sababu bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2021/2022 inajumuisha Wizara zote ili kuhakikisha kwamba sasa tunasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie kusema kwamba kwa ujumla bajeti ya mwaka 2021/2022 imejibu changamoto nyingi na sehemu kubwa ya changamoto ambazo Waheshimiwa Wabunge tulikuwa tunachangia katika Wizara mbalimbali itatusaidia sana sisi kuonekana kwamba mwaka huu tumefanya kazi ya maana na tumejitahidi kushirikiana na Serikali; na kama Serikali itatekeleza bajeti hiyo kama ilivyoandaliwa, nina uhakika kwamba tutakuwa tumefanya jambo la maana sana kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Wizara ya Fedha kwa maono ya kuhakikisha kwamba tunakusanya kodi za kutosha ili kuweza kukidhi bajeti ambayo ipo mbele yetu. Binafsi naunga mkono mapendekezo yote ya makusanyo ya kodi yaliyopendekezwa, nina uhakika kwamba hatutaweza kufanya masuala ya maendeleo bila ya kuwa na fedha za kutosha. Kwa hiyo, lazima tupate maumivu lakini tutakuja kufurahia baada ya changamoto nyingi kuondolewa kwenye maeneo yetu ya majimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhima ya utaratibu wetu wote tulioupanga, lengo kubwa ni kujenga uchumi shindani wa viwanda kwa maendeleo ya watu na kuondoa umasikini. Suala hilo haliwezi kutekelezwa kama mambo yale yanayohusu jamii na shughuli zote zinaohusu maendeleo yetu hazitasimamiwa na kutekelezwa kwa wakati. Tunaweza tukafanikisha tu kukamilisha dhima hiyo na siku ya mwisho lengo letu, tunachohitaji ni kuona kwamba wananchi wote tumeondokana na umaskini ambao umeenea kwenye maeneo mengi ya vijijini. Siku ya mwisho tutakapopima sasa kama malengo yetu tumefikia ni kuhakikisha kwamba huyu mwananchi sasa ameondokana na umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuimarisha viwanda vyetu, naipongeza sana Serikali kwa kuondoa tozo kwenye maeneo mbalimbali ili kuhakikisha kwamba viwanda vyetu sasa vinaimarika. Vile vile naomba niipongeze Serikali kwa sababu imeweka tozo kwenye bidhaa mbalimbali zinazoingia ndani ya nchi zikiwa na lengo kubwa la kuhakikisha tunalinda viwanda vya ndani. Tusipolinda viwanda vya ndani ina maana hatutaweza kufikia lile lengo ambalo tumelipanga la kuondoa umasikini na kuleta maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika upande huo wa viwanda naomba sana Serikali kuweka mazingira bora ya kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanafanya biashara katika mazingira yanayokubalika. Kwa mfano kuna vikwazo vidogo vidogo, unaweza kukuta mwananchi wa kawaida anataka kuanzisha biashara ndogo, lakini mchakato anaotakiwa apitie mpaka aanzishe hiyo biashara, unamkatisha tamaa. Kwa mfano mtu leo ana mtaji wake mdogo, anataka aanze biashara, masharti anayopewa kama anahitaji leseni, lazima aende TRA akafanyiwe assessment. Kwa hiyo, ina maana mwananchi huyu anaanza kulipa kodi kabla hata hajaanza kufanya biashara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumbe Serikali ingeweza kutengeneza mazingira ya kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanaweza kufanya biashara na baada ya kuanza kufanya biashara ndipo waanze kufikiriwa kwamba wanatakiwa wachangie kwenye pato la Taifa. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali yangu, kwa sababu ni Serikali Sikivu, imetusikiliza kwa mambo mengi, nina uhakika kwamba hilo mtalifanyia kazi ili kutengeneza mazingira mazuri kwa wananchi wetu waweze kufanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile katika maeneo hayo ya viwanda naishauri Serikali isimamie miundombinu ambayo ipo katika maeneo haya yaliyotengwa ya viwanda yawe katika hali nzuri. Kwa mfano barabara, umeme, maji kwenye maeneo haya yaliyotengwa kwa ajili ya viwanda naiomba Serikali iweke mazingira mazuri ili tuhakikishe kwamba shughuli zetu zinaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo mambo yote hayawezi kufanyika kama kuna nyanja nyingine za kiuchumi pamoja na kijamii hazitatendewa kazi. Kwa mfano, ukiangalia kwenye suala la afya, ili hawa wananchi baadaye tuweze kuwapima maisha yao kwamba yako bora au yanaenda vizuri lazima kwenye afya wawe kwenye hali nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Serikali kwa kuhakikisha kwamba inaendelea kujenga hospitali, vituo vya afya pamoja na zahanati na kupeleka dawa na vifaa tiba kwenye hospitali hizo. Yote hiyo lengo lake ni kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanakuwa kwenye hali nzuri kiafya. Kwa hiyo, naipongeza Serikali na ninaomba sasa tuendelee na juhudi hizo kwa sababu bajeti tayari imetengwa na itekelezwe ili tuhakikishe kwamba wananchi hawa wanaishi katika maisha mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni elimu. Naipongeza Serikali kwa kusimamia sana kutengeneza miundombinu kwenye suala la elimu, kujenga madarasa na sasa hivi tunategemea kupata fedha nyingine kwa ajili ya kujenga Shule za Sekondari kwenye kila Jimbo. Hiyo itatusaidia kwanza ku- rescue situation ya wanafunzi wengi ambao walianza kuingia kupitia mfumo wa Elimu Bila Malipo ambao wanaanza kutoka mwakani, kwa hiyo, hii itatusaidia kupunguza changamoto kwenye suala hili la elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimpongeze mama yetu Waziri wa Elimu, Mheshimiwa Prof. Ndalichako kwa kutusikiliza sisi Wabunge, tulikuwa tunapiga kelele na kusema kwamba mitaala yetu irekebishwe. Tayari nimeona tangazo tarehe 18 wadau wameitwa kwa ajili ya kuanza kuchangia mawazo kwenye masuala ya mitaala ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali, naomba tuendelee ili tuhakikishe kwamba tunafikia malengo. Kuna suala lingine la umeme. Unakuta kwenye Majimbo yetu, kwa mfano mimi kwenye Jimbo langu kuna vijiji 27 havijapata umeme, lakini katika hivi vijiji 27 kuna kata mbili hazijapata kabisa umeme. Kwa hiyo, naomba sana baada ya bajeti hii Serikali isimamie wananchi wale wapate umeme na vijiji vile vyote vipate umeme ili tuweze kuhakikisha kwamba tunafikia maendeleo ya kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni maji. Naiomba sana Serikali, kwa sababu tutapitisha hapa bajeti; na ninaomba Wabunge wenzangu tushirikiane kuipitisha hii bajeti, ili sasa ile miundombinu ya maji na mambo mengine yasaidie tuweze kumtua mama ndoo kichwani. Kwa hiyo, naomba niishukuru sana Serikali kwa jitihada hizi, lakini naiomba sasa kutekeleza haya kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kilimo. Naiomba sana Serikali izingatie kilimo ambacho kinaleta tija. Tuangalie kwanza kwenye uzalishaji ambao unaleta tija. Vile vile naomba Wizara ya Kilimo watumie vituo vya utafiti ili sasa tuweze kufanya kilimo ambacho kitaleta tija kwenye wananchi watu. Kwa mfano, kuna mashirika ya utafiti kama TARI, TIRDO, TEMDO, CAMARTEC, Serikali ihakikishwe kwamba mashirika hayo yanapata bajeti ya kutosha ili sasa utafiti utakaofanyika na majibu yale ya utafiti yaweze kuwafikia wananchi kwa ajili ya kuendeleza kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la UVIKO 19. Kwenye suala la UVIKO 19 tumeathirika sana kwenye upande wa utalii na usafiri hasa kwa upande wa ndege, lakini kwenye taarifa ya bajeti ambayo imetolewa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, sijaona kama Serikali imeweka mikakati ya dhati na kutenga fedha za kutosha kuhakikisha kwamba inatibu majeraha hayo yaliyotokana na UVIKO 19. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Serikali ifikirie kwa upande wa ndani tunafanya nini? Badala ya kutegemea mikopo kutoka nje au na misaada, sisi wenyewe tumejidhatiti namna gani kuhakikisha kwamba tunasimamia na kudhibiti suala hili la UVIKO 19? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwenye suala la sensa, kwa sababu sensa ni suala la msingi sana kwenye maendeleo ya jamii na ili baadaye tuweze kupata taarifa sahihi za idadi ya watu na makazi, ningeomba sana Serikali iweke nguvu za kutosha katika kusimamia na kuhakikisha kwamba tunapata sensa ya idadi inayokubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)