Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia chochote kuhusiana na bajeti ambayo ipo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Rais wetu Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya pamoja na wasaidizi wake wote. Kwa kweli, ametuheshimisha sana wanawake wa nchi hii, wanawake sasa hivi wamekuja juu, wamepata ujasiri mkubwa, lakini yote hayo ni kutokana na mwongozo wake vile anavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu Waziri na timu yake yote, kwa namna ambavyo wameandaa bajeti. Bajeti ni nzuri, bajeti ambayo inawagusa wananchi wote wa nchi hii, kuanzia wakulima, wafanyakazi, wafugaji, pamoja na watumishi wote. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa namna ambavyo mmepokea maoni ya Wabunge, hatimaye mmeweka kwenye bajeti suala la fedha za Madiwani pamoja na Watendaji wa Kata na Maafisa Tarafa, kulipwa moja kwa moja katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni muhanga wa Madiwani. Katika Jimbo langu la Newala Vijijini, Madiwani waliomaliza muda wao wanadai Halmashauri posho zao, mpaka leo hawajapata. Kwa hiyo, sasa hii ni tiba, tunashukuru na tunatumaini kwamba Madiwani sasa watafanya kazi kwa moyo, watakuwa na ari kubwa kwa sababu wanajua unapofika mwisho wa mwezi watapata posho zao bila shida. Sasa katika hilo, nami nashauri kwamba tuangalie pia zile posho angalau ziongezeke kidogo kwa sababu kiasi kile kwa kweli ni kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye masuala muhimu, masuala ya ukusanyaji wa mapato. Natambua kabisa nchi hii ina miradi mikubwa ya Kitaifa inayotekelezwa ambayo inahitaji fedha nyingi. Pia ipo miradi katika Halmashauri zetu ambayo nayo inahitaji fedha za kutosha, lakini kuna Madiwani ambao watalipwa posho kupitia Serikali Kuu, kuna Maafisa Tarafa, kuna Watendaji wa Kata, fedha hizi ukiangalia zinatakiwa zikusanywe ili hii miradi pamoja na hizi posho ziweze kupatikana. Kama hazitakusanywa vizuri, kwa usimamizi imara, haya ambayo yamewekwa kwenye bajeti yanaweza yasitekelezeke vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, tuweke namna nzuri ya ukusanyaji wa mapato ili yasivuje, tuweze kutekeleza miradi yetu kwa ufanisi mkubwa. Naomba nitoe mfano mdogo. Kupitia Ripoti ya CAG hii ambayo ameitoa ya mwaka 2019/2020 kuna fedha zaidi ya shilingi bilioni 1.2 ambazo zilikusanywa nje ya mfumo kupitia katika vyanzo mbalimbali vya mapato. Sababu ambayo CAG ameitoa ni kwamba fedha hizi zilipita nje ya mfumo kwa kukosekana kwa mashine za POS. Pia kulikuwa na fedha nyingine ambazo zilikuwa zinatumika, zile fedha mbichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana haya, matatizo ya POS tujiimarishe sasa, tuhakikishe tuna vifaa vya kutosha ambavyo vitaenda kutumika kila eneo linalohusiana na ukusanyaji wa mapato yetu ili malengo yetu yakapate kutimia vile ambavyo tunatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, naipongeza sana Serikali kwa kuamua kwa dhati sasa kuanza mpango wa utoaji wa huduma za afya kwa maana ya Bima ya Afya kwa wananchi wote. Ni jambo jema kwa sababu Taifa ambalo litakuwa na wagonjwa wengi, basi halitaweza kuzalisha vile ambavyo tunatarajia. Kwa hiyo, kupitia mpango huu ni matumaini yangu kwamba wananchi watakuwa na afya bora, watafanya kazi zao vizuri na hatimaye Taifa litaweza kujipatia fedha nyingi katika kutekeleza miradi. (Makofi)

Mheshiiwa Mwenyekiti, sasa hapa naomba nitoe rai kwamba, kwa sababu tumeshaweka huo mkakati, tuandae namna ambayo wale wanaokwenda kukusanya fedha za Bima ya Afya au watakaosimamia ujazaji wa fomu za Bima ya Afya wapatiwe mafunzo maalum, kwa sababu sasa itasambaa nchi nzima tofauti na ilivyo sasa hivi kwamba wanaopata huduma ya Bima za Afya ni wachache kuliko tunavyotarajia kama Taifa kwamba sasa watu wote wanakwenda kupata hizi huduma za Bima ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini naongea hivyo? Naongea hivyo kwa sababu ukienda kwenye Ripoti ile ya CAG, alibaini madai ya zaidi ya shilingi bilioni 2.1 ambayo Bima ya Afya yanaidai Serikali kwa sababu tu ya changamoto ya zile kasoro za ujazaji wa fomu. Sasa ukiangalia wanaopata hizo huduma sio wengi kiasi hicho, lakini fomu ambazo zina shida ya kulipwa fedha zake ni zaidi ya shilingi bilioni 2.1. Je, Watanzania wote watakapoingia kwenye huo mfumo, ni kiasi gani cha kasoro kitasababisha upotevu wa dawa kwa kiasi kikubwa? Kwa hiyo, naomba sana mafunzo yatolewe, watu wawe na ujuzi wa kujaza zile fomu ili changamoto hizi zisije zikajitokeza kule tunakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza tena Serikali, kwa kweli katika bajeti hii imeweka mambo mengi sana kuhusiana na masuala ya kilimo. Ukienda kwenye kilimo cha mihogo wameweka namna ambavyo watasimamia mazao ya mihogo, lakini pia hata kwenye korosho. Sasa changamoto yangu ni viwanda. Katika nchi hii kuna baadhi ya viwanda havifanyi kazi sawasawa. Kule kwetu Newala ambako tunazalisha korosho kati ya tani 20 hadi 30 kwa mwaka hatuna kiwanda cha uhakika cha kubangua korosho ili kuithaminisha korosho hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kiwanda cha Agrofocus, hiki kimebinafsishwa, lakini tuna kiwanda cha Micronox; kiwanda hiki kimepewa mtu ambaye uwezo wake tunadhani ni mdogo kwa sababu, kwa mfano msimu uliopita hakuwa na malighafi. Inaonekana hakuwa na fedha, kwa hiyo, yale ambayo tulitegemea tuyapate kutokana na kiwanda hiki yanashindwa kutekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vile wakati vinafanya kazi kule Newala, zaidi ya asilimia 80 ya waliokuwa wanafanya kazi pale ni wanawake. Sasa hivi viwanda havifanyi kazi, wanawake wamekaa chini, wanashindwa kuwasaidia akina baba, wanashindwa kutimiza majukumu yao. Naiomba sana Serikali, nimeangalia pia kwenye bajeti sijaona mkakati wa dhati wa namna ya kuinua viwanda vile vikaweza kufanya kazi kuanzia msimu unaofuata. Kwa hiyo, changamoto hii maana yake bado ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, tuna taarifa kwamba kulikuwa na mnunuzi kutoka nje alitaka kununua kiwanda kimojawapo na Serikali ina taarifa hiyo. Naomba basi Mheshimiwa Waziri wakati unakuja kufanya majumuisho utuambie hatima ya ununuzi wa kiwanda kile imefikia wapi? Hii itawasaidia wananchi wa Newala kujiajiri kupitia ubanguaji wa korosho wanazozizalisha kwa wingi katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo linaleta changamoto kubwa katika Mikoa au Wilaya ya Newala kwa ujumla ni suala la barabara. Wilaya ya Newala ipo Kisiwani, haina hata barabara moja ya lami kati ya wilaya na wilaya au wilaya na mkoa inayofika Wilaya ya Newala. Barabara zote ni za vumbi, lakini ni wakulima wazuri sana wa korosho na mihogo. Kwa hiyo, usafirishaji wa mazao yao ni changamoto kubwa kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya Serikali ilikuwa kuunganisha barabara za mkoa na mkoa kwa kiwango cha lami. Wilaya ya Newala inaunganisha Mkoa wa Lindi kupitia Mtama kwenda Mtwara, lakini barabara ya kutoka Amkeni – Kitangali mpaka Mtama yenye kilometa 74 ni ya vumbi. Tunaishukuru Serikali imeshajenga kwa kiwango cha lami kilometa 22. Tunaomba Serikali iboreshe barabara hii, ijengwe kwa kiwango cha lami sasa ikamilike ili wananchi wa Newala ambao wanapata huduma zao nyingi katika Jiji la Dar es Salaam nao waweze kutumia barabara hii ikiwa katika mazingira mazuri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Maimuna.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante.