Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunipa afya tele mpaka naweza kuchangia bajeti hii.

Pili, niishukuru familia yangu, lakini kipekee kabisa nimshukuru mke wangu aliyenipa uwezo mkubwa sana wa kuwajibika na kuweza kutimiza majukumu yangu ya kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba, bajeti hii ni bajeti ambayo itaendelea kusomwa na kusifiwa kuwa ni bajeti nzuri kabisa katika bajeti zilizowahi kujadiliwa katika Bunge hili Tukufu. Siyo nasema hivyo kwa sababu tu ya kutaka kusifia, lakini ukiangalia jinsi hii bajeti ilivyotengenezwa, unaweza ukalithibitisha hilo nia ya bajeti ukiiangalia lakini pia ukiangalia dira lakini ukiangalia dhamira na pia ukiangalia pia utayari wa Mheshimiwa Jemedari wetu Mama Samia Suluhu Hassan, hiyo inakuashiria moja kwa moja kwamba hii bajeti itakuwa bajeti nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti yenyewe naanza kwa kusema kabisa kwamba itatekeleza na kusimamia mazuri yote ambayo awamu tofauti tofauti za uongozi imeyatekeleza. Mazuri katika awamu hizo yako mengi sana, kila awamu iliyopita imekuwa na jambo zuri sana la kuigwa na kulisimamia kwamba liendelee kuwepo. Hata hivyo, kwa hali jinsi ilivyo kutokana na ufinyu wa muda sitaweza kuzungumzia kila zuri la awamu iliyopita, lakini kipekee tu nitaweza kuzungumzia jinsi walivyoweza kusimamia yale waliyotaka kuyatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, Awamu ya Kwanza ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, yeye aliamini katika Taifa lenye uchumi imara kupitia sera ya Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea lakini hali kadhalika nchi huru yenye fikra huru, yenye uchumi huru, yenye siasa huru bila kujifungamanisha na nchi yoyote ile. Hili lilikuwa ni jambo jema kabisa ambalo awamu hii pia italitekeleza kwa njia ya kipekee kupitia staili yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu iliyofuatia ilikuwa ni awamu ya Mheshimiwa Rais Ally Hassan Mwinyi na yenyewe ilikuwa na dhamira nzuri kabisa uchumi huria, lakini yenye watu ambao wako proactive, kukimbilia fursa ambazo zitawawezesha wao kuijenga nchi yao kikamilifu hasa katika masuala ya kibiashara. Fikra hii ililenga katika kuimarisha dhana ya kuwa uchumi au suala la biashara lishughulike na watu binafsi, lakini wakati huo huo Serikali ikijikita katika kutekeleza mambo ya msingi ya kijamii na kuendeleza miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Awamu ya Tatu, ya Mheshimiwa Benjamin William Mkapa na yenyewe ilikuja na fikra pevu, nzuri kabisa ambayo yenyewe ililenga kabisa katika utekelezaji wa uwazi, lakini seriousness katika utekelezaji huo. Lengo lilikuwa ni kuwajenga wananchi waweze kujitambua, lakini pia kuona kwamba kila wanachokifanya wanakifanya kwa ajili ya manufaa ya nchi yao na uzalendo wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia awamu iliyokuja, Awamu ya Nne ya Mheshimiwa JK. Awamu hii pia ililenga katika kutengeneza uchumi uliokuwa imara, bora kabisa, ilijihakikishia kwamba inaweka miundombinu yote ya kuchochea uchumi na maendeleo, ilijaribu kuweka mkakati pia wa mahusiano ya kimataifa ambayo yalikuwa mahusiano bora kabisa na nchi za nje. Hii yote ililenga katika kuweka uchumi uliokuwa imara uchumi endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Awamu ya Tano, awamu ya jembe, tuliona kabisa awamu hii ilikuja kwa kasi kubwa. Hii ilikuwa ni awamu ya kazi lakini hali kadhalika ilikuwa ni awamu ya viwanda ambavyo vimejielekeza katika kutekeleza uchumi wa nchi hii. Pia awamu hii ilikuwa awamu ya uwajibikaji lakini na u-champion katika kupambana dhidi ya rushwa na ufisadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia awamu hizi zote zilikuwa zimefanya vizuri na kama alivyosema Mheshimiwa jembe letu, mama yetu, jemedari wetu mkubwa, kwamba atajielekeza katika kutimiza mazuri yote, tunaona mazuri haya yanajenga msingi mkubwa na imara katika kutekeleza yale yote ambayo tunayategemea katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uzuri wa hayo yote, nina shaka kidogo hasa nikiangalia kwa kadri jinsi tulivyoweza kutekeleza bajeti zetu zilizopita. Ukiangalia bajeti zetu zilizopita unaweza katika hali ya ubinadamu ukaona kwamba kunaweza kuwa na shaka. Kwa mfano, kwenye kilimo kilitekelezwa kwa asilimia 13 tu ya bajeti nzima. Halikadhalika viwanda, ile dhamira ya kutekeleza uchumi wa viwanda, bajeti zilizopita zilitekeleza kwa takriban ya wastani wa asilimia 20. Kwenye mifugo, ilitekeleza kwa takriban ya asilimia 18.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mazingira hayo yanaweza yakakupelekea ukawa na wasiwasi. Hata hivyo, wasiwasi huu unatoka moja kwa moja kwangu na imani niliyokuwa nayo ni kutokana na ile hali ya utayari wa mama yetu, hapo peke yake naamini kabisa kwamba hakutakuwa na wasiwasi kila kitu kitakwenda kama vile kilivyopangwa katika bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusisitiza kwenye hili ni nini? Nasisitiza katika utekelezaji. Naomba utekelezaji uwe wa umakini kabisa. Tukizungumzia utekelezaji hasa hasa unajikita katika maeneo matatu. Eneo la kwanza ni katika kutoa pesa inayohitajika, kusudi kila sekta ambayo imeomba pesa ipewe kwa kadri ya wakati na vile inavyohitajika na kwa kiwango kinachostahili. Awamu nyingine ni awamu ya utekelezaji, ambapo Wizara husika na watendaji kupitia sekta zake binafsi pamoja na halmashauri wawe wanawajibika kikamilifu kabisa kuhakikisha kila kitu wanachotakiwa kukifanya wanakifanya kama inavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nataka kulizungumzia zaidi ni eneo la usimamiaji na hilo ndiyo jukumu letu sisi Wabunge pamoja na Madiwani. Sisi kisheria tumetambulika kwamba ni wasimamiaji ambao tunatakiwa tuisimamie Serikali kikamilifu kabisa. Kazi hii haiwezi kufanyika kikamilifu kama hatutapata taarifa zinazostahili katika kusimamia mambo haya. Kumekuwa na changamoto kubwa sana katika eneo la usimamiaji hasa hasa ukiangalia kwamba watendaji wameamua kupokonya kazi hii ya kusimamia. Mara nyingi wamekuwa hawatoi taarifa kwa Wabunge ambao ndiyo wanaostahili kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu haya wanajikabidhi wenyewe na wewe kama Mbunge ukijaribu kufuatilia kupata taarifa stahiki kutaka kujua ili uweze kusimamia, kunakuwa na changamoto ya usiri na unaonekana kama wewe ni kama vile kizabizabina, lakini halikadhalika unaonekana kama wewe unajipendekeza, lakini pia unaambiwa kama wewe unajipa madaraka ambayo hustahili wakati hili ni suala letu au ni kazi ambayo sisi tumeambiwa kisheria kabisa tunatakiwa tuifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba sana Wizara, naomba sana na Mawaziri wafanye kazi ya kutupa taarifa kabla hawajapeleka pesa ya mradi wowote, sisi tunastahili kujua mapema kuliko mtu mwingine yeyote.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja, sina shaka bajeti hii itakuwa ni bajeti yenye kuzungumzwa na kutekelezwa, lakini na kusifiwa duniani kote na miaka yote. Ahsante. (Makofi)