Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Taifa letu. Taifa la Tanzania limeendelea kuwa imara wakati wote. Lakini tunamshukuru zaidi kwa sababu Mwenyezi Mungu ameendelea kutupa viongozi wazuri toka kipindi cha Uhuru mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema ahsante sana Mwenyezi Mungu kwa sababu pia hata sisi waja wake tumeamua kumtumainia. Na wanasema uchaji wa Mungu ni baraka kuliko vyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo furaha sana baada ya kuona kwamba tulikuwa na kiongozi shupavu, jemedari, marehemu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Lakini Mungu alimuonesha kumchagua mtu wa kuwa mgombea mwenza wake ambaye pengine Mwenyezi Mungu alifunga tu kauli ile ya kumwambia kwamba huyu ndio atakayekurithi, lakini alihakikisha anapata mtu ambaye ni mwenye maadili, mwaminifu, mchapakazi, mshauri sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hivyo, hata ilipofikia kwenye kubadilisha uongozi, hajapata nafasi kwamba eti aende kozi ya kumfundisha kuwa Rais; kuna mahali amefundishwa jamani? Hakuna. Ameendelea kuchukua kasi ileile, ameendelea kuchukua uthubutu uleule, ameendelea kututia moyo na kuonesha kwamba Taifa liko katika misingi ileile. Tunamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa ajili yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi, alivyoingia madarakani amejipambanua wazi akasema suala la rushwa silitaki, na sitaki kusikia… shetani na ushindwe! (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maandiko pia tunaambiwa kwamba rushwa ni udhalimu na utafutwa mbali, bali uaminifu utakaa hata milele. Ndiyo maana rushwa ameikataa toka asubuhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, niseme kwamba, alisema, sitaki mapato ambayo ni ya dhuluma. Na maandiko pia yanaungana na hilo, yanasema kwamba mapato ya mwovu – maana yake ukifanya dhuluma ni mwovu – yatakauka kama mto, na kama ngurumo penye mvua inayopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hayo yote napenda tu kuunganisha hali halisi ya viongozi wetu walivyo wanyofu, na hasa huyu sasa tuliyenaye, naye amekwenda katika mstari huohuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu amesifiwa kwa mambo mengi, lakini mimi napenda sana ile misemo yake, naifuatilia, mara kwa mara anafundisha kwa mifano na kwa misemo. Kuna wakati aliwahi kusema kazi lazima iendelee. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kazi iendelee. Lakini mimi naongezea iendelee na nani, na mama Samia Suluhu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haikuishia hapo, akasema kuwe na upepo kusiwe na upepo, jahazi lazima likafike. Jamani mambo si haya, jahazi linakwenda kufika. Kwa hiyo, baada ya kutafakari haya nimejirejesha pia katika malengo endelevu ya maendeleo ambayo tunatarajia tuondoe umaskini kufikia 2030. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kwamba bado kuna tofauti kubwa sana ya kimaendeleo kati ya watu walioko mjini na walioko vijijini. Ukifuatilia unakuta kwamba hata hali ya umeme bado vijijini ilikuwa iko chini, sasa hivi ndiyo tunakwenda kumaliza. Lakini hali ya maji bado ni changamoto kubwa, hasa katika maeneo ya vijijini; hali ya barabara na miundombinu mingine ni hivyohivyo. Kwa hiyo bajeti hii inalenga kwenda kusawazisha hizi changamoto ambazo zinafanya hali ya vijijini iwe ni ngumu zaidi kuliko hali ya mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna akinamama wako kule vijijini hawajawahi kuona kituo cha afya au kujifungulia hospitali. Bajeti hii inakwenda kuondoa hayo yote; inakwenda kupunguza kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kuipongeza sana, napenda kumpongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango, lakini pamoja na timu yake yote. Siyo rahisi kumtaja mmojammoja, lakini nawapongeza, wamekuja na bajeti iliyotutia moyo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii ni tofauti na wadau wengine walivyokuwa wanashauri, wanasema akiingia kiongozi mpya inabidi na yeye aache legacy yake, kwa hiyo, aache yale ya mwanzo yaliyotangulia aanze ya kwake, matokeo yake kunakuwa hakuna uendelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bajeti hii imejiweka wazi namna gani itakwenda kumalizia ile miradi yetu mikubwa ya kimkakati ambayo ilianzishwa na hawa majemedari wawili; jemedari wetu marehemu, na jemedari mama yetu, Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan. Na kwa misingi hiyo niseme tu kwamba hilo ndilo ambalo tunalihitaji Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala ambalo tulifanya kubwa katika kipindi hiki ni uthubutu wa hii miradi mikubwa ambayo ilikuwa inawezeshwa na fedha yetu ya ndani. Kwa misingi hiyo uthubutu ule umeendelea ambao sasa tunajipangia malengo mengine ya kuhakikisha kwamba miundombinu mingine inapatikana kwa kuhakikisha kwamba kila mwananchi anachangia katika kupata fedha hizo; hatuna mjomba, hatuna shangazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hatuwezi kuendelea kuusifia umaskini au sisi kufurahia kuitwa maskini kwa sababu eti kuna mtu yuko pale pembeni atatuchangia sisi fedha zake. Lazima sasa tuondoke na tujue kwamba sisi tunao wajibu mkubwa wa kuhakikisha kwamba tunapata fedha kwa ajili ya kuhudumia maendeleo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo hilo tunazo fursa. Fursa ninayoiendea sasa ni ya Soko Huru la Afrika ambalo tayari Tanzania tumeshasaini mkataba wake, bado kuridhia. Na ninaamini pengine Wizara husika ya Wizara ya Viwanda na Biashara mtajitahidi kufanyia kazi suala hili ili huu mkataba tuuridhie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na suala hili sasa linapojitokeza, niwaombe Watanzania, kuna mambo hatuwezi kuyakimbia. Ni lazima na sisi tujiweke katika mpango na mstari wa kuhakikisha hiyo fursa tunaitumia vipi. Hata kama sisi hatutataka lakini wenzetu watakuja kutumia fursa zilizopo nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hatutawakaribisha wawekezaji kuwekeza hapa nchini basi watawekeza pembeni ya nchi yetu na sisi tutakuwa soko lao, watu wanataarifa kiasi gani kuhusiana na suala hili, mambo gani ambayo yanaweza kuwa ni vikwazo kwa hawa wananchi kuweza kushiriki kwenda katika nchi nyingine kutafuta masoko na kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu tukiwawezesha wanawake wakapata elimu ya kutosha, wanawake najua wao siyo waoga wanauwezo wa kwenda nchi yoyote ile wakafanya biashara na ndiyo maana hata Mheshimiwa Rais amesema katika sehemu anayotaka kufanya ni kuhakikisha kwamba anawezesha wanawake kiuchumi katika kupitia majukwaa mbalimbali ya kwenye mikoa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe kwa sababu hawa wanawake ni kundi kubwa ni jeshi kubwa na lina uwezo huo na wanawake hatuogopi hata tukiamua kuolewa nchi yeyote tunaenda kuolewa huko na tunajenga mataifa huko. Kwa hiyo, hata biashara ukitaka biashara za nje zifunguke ni pale tutakapowezesha makundi haya ya wanawake. Tukifanya hivyo kweli tunaweza kufanya biashara yaani katika soko la Afrika, lakini pia tutaweza kupata maendeleo tunayo yahitaji kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)