Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye hoja hii iliyopo mezani, ya Bajeti yetu Kuu ya Serikali. Nitumie fursa hii kuipongeza sana Wizara hii chini ya uongozi wa ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu wake Mheshimiwa Hamad Masauni na watendaji wote, kwa sababu kazi mliyofanya kutuletea bajeti hii iliyofurahisha taifa hili lote, na inawezekana hata mataifa ya jirani sio kazi ndogo, hongereni sana. Lakini pia nimpongeze Rais wangu, Mheshimiwa mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa sababu bajeti hii imeakisi maono yake; na nadhani ndiyo maana Mheshimiwa Waziri kila wakati ulisema mama amesikia kilio chenu akafanya hiki, amesikia kilio chenu akafanya kile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamshukuru sana kwa sababu amesikia kilio cha Watanzania ambao tunawawakilisha hapa Bungeni na amefanya mambo makuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sina haja ya kuangalia mambo mazuri yaliyofanywa kwenye bajeti hii kwa sababu mengi yameshasemwa. Mimi nadhani kazi yangu hapa ni kutoa tu ushauri katika maeneo madogo madogo ambayo nadhani yangeweza kuboreshwa ili Watanzania waendelee kuneemeka na bajeti hii ambayo miongoni mwa vipaumbele katika miradi ya maendeleo ni kuwawezesha wananchi kiuchumi. Kuna mambo ambayo tusipoyazingatia tukayaweka sawa tutakuwa hatujawatendea haki baadhi ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika eneo la mifugo kuna changamoto kubwa kwa sababu, kwanza bajeti yao ni ndogo, bilioni 16, kwa sekta ambayo ina rasilimali ya mifugo ambayo ni ya pili katika Bara la Afrika na malengo waliyojiwekea?

Ninaunga mkono kabisa maoni ya Kamati wamesema kwamba miongoni mwa malengo makuu ambayo wamependekeza Wizara ya Mifugo ifanye ni kuwezesha upatikanaji wa maeneo ya malisho, kuwezesha upatikanaji wa maji kwa ajili ya mifugo, kutenga na kupima maeneo ya malisho, kusimamia suala la utafiti wa mifugo, kutatua migogoro kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi, kuimarisha vikundi, kuboresha mbegu na mambo kama hayo. Sasa, kwa bilioni 16 utafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi nilikuwa napenda tu kuwashauri basi wasimamiaji wa utekelezaji wa bajeti hii katika sekta husika na Wizara yenyewe kwa ujumla, Wizara ya Fedha, kwamba tuangalie maeneo mahususi ya kipaumbele ili basi tuone kama na mfugaji naye atakwamuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, hili suala la migogoro ya ardhi kati ya watumiaji wengine wa ardhi ni suala nyeti sana. Napenda kuishauri Serikali kwamba, Wizara ambazo zinaguswa moja kwa moja na migogoro inayozuka zikae pamoja, zipitie sheria na kanuni na taratibu, zije na mfumo sahihi ambao utasaidia kutatua migogoro hiyo ili upatikanaji wa ardhi ya malisho iweze kubainishwa na maeneo ya watumiaji wengine yaweze kuwekwa wazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Wizara ya Ardhi ambao ndio wapimaji wa ardhi, Wizara ya TAMISEMI ambayo ndiyo wenye vijiji, Wizara ya Maliasili ambao ndio wananyakua nyakua hati za watu bila hata kuwashirikisha wengine, wakae pamoja na Wizara ya Mifugo, ili kumaliza migogoro ya ardhi ambayo inajitokeza kila wakati na kupunguzia wafugaji maeneo yao. Na nina-reference nzuri kwa sababu kumbukumbu tuliyonayo sisi watu wa Longido kuna eneo linalotaka kutwaliwa la malisho. Eneo mahususi la malisho wakati wa kiangazi, eneo la Lake Natron na milima yote inayozunguka huo uwanda wa Longido. Haiwezekani Wizara moja ikachomoka ikaenda kutangaza eneo kwamba wanataka kulifanya pori la akiba, na ni la wafugaji na Wizara ipo, TAMISEMI waliotambua vijiji wenye hiyo ardhi wapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ni masuala ya msingi ambayo lazima tuishauri Wizara ya Fedha na Mipango, waangalie wanapotenga fedha ielekezwe kwenye yale masuala ya msingi ambayo yatatusaidia kusonga mbele na kupata maendeleo ya Watanzania wote kama yalivyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia, ningependa kushauri Serikali katika maeneo mengine mahususi; kama kwenye hii sekta ya maliasili ambayo Mbunge mwenzangu wa Arusha ameshasemea na kutoa takwimu. Mimi napenda tu kuiomba Serikali, kwamba itoe kitu kinachoitwa incentive package ya kuchochea utalii ili uweze kurudi; kwenye sekta zote, utalii wa kuona wanyama, utalii wa uwindaji, wapunguze bei ili watalii warudi. Maana sasa hivi pamoja na corona South Africa wao wanapata watalii kwenye maeneo yao ya kiwindaji mpaka milioni tisa kwa mwaka. Namibia wanapata mpaka milioni nane, na hata Zambia ambao wote kwa pamoja hawana maeneo mengi ya uhifadhi kama sisi na ya uwindaji lakini kwa sababu, sisi bei zetu tumeziweka juu na hatuna mpango wa kupunguza bei ili kuvutia tumeendelea kuathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuchochee utalii wa ndani. Utalii wa ndani utaimarika pale ambapo packages zitatangazwa, ziwekwe bayana kabisa kwamba watoto wa shule, watu wazima, ma-group yanapoungana wakienda kutalii kwa bei ndogo kabisa, hapo kila mtu atataka kuona hifadhi zetu na mapato yatapanda kwa njia hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Sekta ya madini. Napenda kuishauri Serikali kwa sababu watu waliposikiliza hii bajeti wakaanza na wao wananchi ambao tunawakaribisha kurusha kero zao. Kwa mfano, Ninalo andiko hapa watu wa madini wanasema kuna kitu kinaitwa kodi ya pay as you earn na kuna kodi inayoitwa SDL ambayo nadhani hiyo inahusika na masuala ya Skills Development Levy, sijajua Kiswahili chake. Wanasema kwamba TRA hasa kwenye migodi ya madini haya ya Tanzanite, wanawalazimisha wale wachimbaji wawalipe watu mishahara, wakaweka na viwango na kumbe makubaliano yao huwa ni kwamba wanalipana baada ya mali kupatikana na ni mfumo ambao ulishakubalika. Kwa hiyo ingebidi TRA wasiwalazimishe watu hawa wa madini kulipa fedha ambayo wenzao wanaochimba bado hawajapata na watambue kwamba kuna utaratibu waliokwishajiwekea tayari.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni tozo la huu Wakala wa Meli Tanzania inaitwa TASAC. Wao huwa wana- charge fedha tu lakini hawa-track ule mzigo, wao wakishapokea tu wakishalipwa basi hawana taarifa ya ku- track huo mzigo mpaka umfikie mnunuzi katika nchi aliyopo. Watu wa sekta ya madini hawa nao wanaotuma madini nje, wanaomba kwamba hilo Shirika la TASAC halina msaada wowote kwao, charge hizo wanazo-charge hazina maana kwa hiyo ziachwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu eneo la ongezeko la thamani kwenye biashara kati ya wafanyabiashara wa ndani, kwenye soko lile kuna watu wanaouuza na kununua mlemle. Wenzao wale wanaowauzia wanatoza VAT na VAT ilishaondolewa, kwa hiyo nalo pia liondolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa, kuna kitu napenda kuongeza kabla ya muda wangu haujakwisha, kwamba Madiwani walivyowaongozea maslahi yao na Watendaji wa Kata imekuwa ni nderemo, vifijo na furaha kwa nchi nzima. Hata hivyo, kuna watu ambao ndio wako kwenye ground, kule ambako ndio tyre inagusa lami. Watendaji wa Vijiji hawajafikiriwa katika kuwawezesha. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiruswa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Francis. Karibu.

MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba Madiwani hawajaongezewa fedha bali wamewekewa kulipwa na Serikali Kuu kwenye Akaunti zao. Posho zao sio kwamba wameongezwa, ili taarifa zikae vizuri.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, unapokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea hiyo taarifa, nashukuru kwa sahihisho lakini kile kitendo cha wao kulipwa moja kwa moja kimewaondolea adha na kero kubwa sana. Kile kitendo cha Watendaji wa Kata kupewa dhana, vitendea kazi, mafuta pia imewaongezea ari ya kufanya kazi kwa bidii sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kundi ambalo limesahaulika, Watendaji wa Vijiji na wao wanafanya kazi kubwa, ingefaa katika bajeti hii na wao wafikiriwe. Kwanza katika vijiji vingi katika nchi hii likiwemo Jimbo la Longido, sisi asilimia 75 hawajaajiriwa wana kaimu kwa miaka mingi sana, sijajua bajeti wanawaweka wapi na kama shida ilikuwa ni fedha itafanyika nini ili Watendaji wa Vijiji waajiriwe katika nchi nzima ambapo kuna Makaimu wasiohesabika na kwa miaka na muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kuchangia hoja yangu ya mwisho kwamba katika kupanga haya maendeleo ambayo hii bajeti inakwenda kutekelezwa, wananchi wanaoishi katika maeneo ya uhifadhi jumuishi kama Ngorongoro kuna haja kubwa ya Wizara ya Maliasili hata Wizara ya Fedha wasaidie ili fedha inayotolewa kwa ajili ya miradi kama shule, hospitali, barabara, wakati wa mchakato wa kutafuta namna sahihi ya kufanya uhifadhi jumuishi au wa mseto zikiendelea, wale wananchi nao waangaliwe maendeleo yao yasirudi nyuma. Nasema hivyo kwa sababu kuna vikwazo vikubwa na watu Ngorongoro hawapati maendeleo kwa ajili hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo basi, ili kuleta umoja kati ya wahifadhi na wafugaji kuna haja sasa ya kusahau sera za zamani za kuona kwamba mifugo na wanyamapori ni maadui. Sio maadui ni kuweka tu mpango wa matumizi bora ya ardhi ili wanyamapori na mifugo kwa utaratibu wa matumizi bora ya ardhi ambayo yanaweza yakapangwa wakashirikiana nyanda za malisho katika maeneo mahsusi kama Ngorongoro ama katika maeneo ya uwindaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hizi tozo ambazo watu wanatoza watu wa maliasili ile Sh.100,000; ningeomba hata sasa leo wakati baadaye hii hoja inajumuisha, tuambiwe ni sheria gani hiyo ilipitishwa na Bunge gani linaloruhusu mfugaji atozwe 100,000 kwa kila ng’ombe anapokutwa ameingia katika eneo la hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, kuna pia kero kubwa kwa sababu bajeti haijazingatia matakwa ya wafanyabiashara wa mifugo. Kodi yao haijaguswa popote kupunguzwa. Naomba kodi yao iangaliwe hasa kupeleka mifugo nje maana bado soko la ndani ni hafifu, ni duni ili na wao wapate punguzo, wapate ahueni na maisha yao yaboreke kutokana na bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)