Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, pacha wangu ambaye tunategemeana. Kwanza naunga mkono hoja hii kwa sababu watu wangu hata wakizalisha namna gani, kama bajeti ya pacha wangu haijapita watakosa mahali pa kupeleka bidhaa zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niseme kwamba bajeti hii ya leo tunayoipitisha ni jambo jema sana kama Waheshimiwa Wabunge wote tutaelewa dhana yake halisi iliyomo kwenye bajeti hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, kwanza hii ni bajeti ya kwanza ikiwa imebeba dhana hii ya kwenda kwenye Tanzania ya Viwanda na hivi tunapopitisha tunatengeneza pamoja na miundombinu yake ambayo inahusiana na suala hili la kukuza viwanda.
Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wote tuelewe kwamba suala la viwanda siyo suala la Serikali peke yake wala si suala la Waziri wa Viwanda peke yake, ni suala ambalo linaanzia kuanzia uzalishaji, linakwenda mpaka kwenye kujituma kwa Watanzania na linakwenda mpaka kwenye uwekezaji ambao unatumia sekta binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno mengi ambayo yamesemwa na Waheshimiwa Wabunge, Wizara imezingatia na mimi kwa sababu pacha wangu nakaa naye karibu hapa, kuna hatua ambazo ameendelea kuzichukua hapa ambazo ni maelekezo ya ufanyiaji kazi wa mawazo ya Wabunge hata kabla hajasimama kujibu hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nijibu baadhi ya hoja ambazo zimejitokeza ambazo zinalenga kwa pamoja kwenye Wizara yangu na pamoja na mwendelezo wa ushirikiano wa Wizara yangu pamoja na Wizara ya Viwanda Biashara na Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye jambo alilolisema Mheshimiwa Leonidas Gama, Mbunge wa Songea Mjini ambalo lilikuwa linahusisha kiwanda cha kuchakata mihogo kifanyikie hapa hapa Tanzania badala ya mihogo kusafirishwa. Wizara zetu tayari zimeshachukua hatua kwenye hilo kuanzia kwenye mahitaji ambayo yanahitajika katika kuhakikisha jambo hilo linafanikiwa. Nimpongeze sana kwa hoja hiyo na kwa concern yake, lakini nimhakikishie kwamba hicho ndicho ambacho kitafanyika. Hivi tunavyoongea mwekezaji mmoja wa Tanzania Agricultural Export Processing tayari alishajenga kiwanda Pwani, na anategemea kujenga Lindi, Mtwara, lakini hivyohivyo ndivyo itakavyofanyika katika maeneo mengine ambayo yanalima muhogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninatoa rai kwa Waheshimiwa Wabunge, tuwahamasishe wananchi wetu waweze kujikita katika kilimo hiki kwa ajili ya soko lililopatikana, lakini pia kwa mimi wa kilimo niseme kama moja ya chakula cha akiba ambacho kinastahimili katika maeneo mengi ambayo yana mtawanyo hafifu wa mvua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka Mheshimiwa Mbunge Mukasa wa Biharamulo, Mheshimiwa Innocent Bashungwa Mbunge wa Jimbo la Karagwe na Mheshimiwa Mbunge wa Innocent Bilakatwe Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum mgeni kabisa hapa Mheshimiwa Oliver na yeye amesema, pamoja na hawa wanaotokea Ukanda wa Tabora pamoja na Shinyanga wameongelea zao hili la muhogo. Sisi kama Serikali tunawahakikishia uhakika wa soko, lakini pia maabara ambayo imeshapitishwa ya kisasa kabisa ya kuweza kufanyia tathmini zao hili, ili liweze kuuzwa popote pale duniani. Kwa maana hiyo, Waheshimiwa Wabunge, tunapoongelea viwanda Serikali tumedhamiria na tuna uhakika hatubahatishi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe tu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania siyo mara ya kwanza kwa Serikali ya CCM kuamua jambo na likafanikiwa. Tuna mambo mengi ambayo yamefanikiwa na ninyi ni mashahidi. Niwaambieni siyo miaka mingi sana ilikuwa ukitaka kupiga simu inabidi uende kusubiria simu za kuzungusha zile. Hili sijasimuliwa nimeshuhudia mwenyewe, lakini kwa sasa hivi hata wanafunzi wa shule za msingi wana simu za mkononi, hiyo ndiyo CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo siku nyingi ilikuwa mtu akitaka kusafiri kutoka eneo moja kwenda eneo lingine inabidi apange safari ya wiki nzima kwa hiyo, kama ana bidhaa zake atazipata baada ya mwezi mmoja. Lakini tuliposema tutaunganisha nchi hii Mikoa kwa Mikoa ili watu waweze kuwekeza na kusafirisha bidhaa, sasa hivi unaweza ukatoka na taxi Mtwara na taxi na ukaenda mpaka Mtukula kule kwa taxi. Ama ukatoka mpaka wa Zambia ukaenda Holili kwa taxi. Kwa hiyo, tunaposema tunaenda kwenye Tanzania ya viwanda tuna uzoefu wa kuamua jambo na tukatekeleza likafanikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaanza kuhamasisha uzalishaji kwa sababu, viwanda tunavyotaka kujenga siyo viwanda vya kuzalisha kwa wiki moja, tunataka viwanda ambavyo vitazalisha katika msimu wa uzalishaji na vizalishe katika msimu ambapo vina akiba ya malighafi. Kwa maana hiyo, jambo hili ni vema Watanzania wote tukaiitikia kauli ya Mheshimiwa Rais ambaye ameshatoa dira kwamba tunaenda kwenye Tanzania ya viwanda badala ya kuanza kauli za kukatishana tamaa ambazo zinaweza zikawaacha wengine wasijue ni lipi la kufanya. Ni vema tukawa na kauli moja kwa sababu nchi hii ni yetu sote na mafanikio haya yakiwa ya Taifa itakuwa ni heshima kwetu sisi sote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hili tulilosema la jembe la mkono kupelekwa makumbusho, jamani ni jambo ambalo linawezekana. Hatuwezi tukaendelea kujilaani kila leo kwamba sisi tutakuwa watu wa jembe la mkono. Tumedhamiria, tutatumia sekta binafsi, tutatumia jitihada za Serikali, tunaunganisha zote za sekta binafsi pamoja na jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba, tunaenda kwenye kilimo cha kisasa kwa sababu hatuwezi tukazalisha bidhaa za kutosha viwanda kwa kutumia jembe la mkono. Jambo hili lazima liwe na mwanzo na sisi tumepanga mwanzo ni sekta binafsi pamoja na sisi wenyewe Serikali, tayari tunakaa pamoja na Wizara ya Viwanda kwa ushirikiano wa Wizara ya Mambo ya Nje pamoja na Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba tunaweka mikakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayasema haya kwa sababu ndiyo tunaanza. Huu ndiyo wakati wenyewe wa kusema tumepanga nini na baada ya hapo tunaenda kwenye kutekeleza. Watu ambao mnakuwa na mashaka niwaambieni hiyo hairuhusiwi hata kwenye vitabu vya Mungu maana Mungu mwenyewe anasema mwenye hofu hatapokea kitu kwangu; and a person who is incapable of even trying, is incapable of everything. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie, nimeshuhudia nikiwa mdogo Mkoa wa Singida watu walikuwa wanaenda kusaga unga wa kula mara moja katika miezi sita, lakini sasa hivi lile jiwe la kusagia lilishapotea. Kwa hiyo, hata jembe la mkono nina uhakika litabaki maeneo matatu; eneo la kwanza kwenye makumbusho, eneo la pili makaburini kwenye kuchimba makaburi na eneo la tatu kwa ajili ya kumbukumbu litabaki kwenye bendera ya CCM, ili itukumbushe tulitoka wapi.! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nitumie fursa hii tunapochangia bajeti ya Viwanda na niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote tuzingatie, tuwahamasishe wananchi wetu waepuke kuibiwa, wanaibiwa kwenye uuzaji wa mazao kwa lumbesa. Nimesikia malalamiko hayo kwa Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, kwa Mheshimiwa Bosnia kule, nimesikia malalamiko kwa Jah People kutoka kule Njombe, kwa Mheshimiwa Hongoli pamoja na ndugu zangu wa Ludewa na maeneo mengine ambako wanazalisha mazao hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwaelimishe wananchi wote watumie vipimo rasmi. Hii wanayouza kwa lumbesa ni namna ambayo wanunuzi wasio waaminifu wanawadanganya kwamba hii ni namna ya kupakia lakini ndivyo ambavyo wanawaibia wakulima wetu. Baada ya kuwa tumeshaanza mwaka mpya wa fedha, vyombo vya dola visimamie ili wakulima wetu waache kuibiwa, likienda sambamba na wale wanaonunua mazao mashambani wakiita wanachumbia, kwamba kama ni migomba inakuwa bado ndizi hazijawa tayari kwa ajili ya kuuza, wao wanawekeza fedha kwa bei ndogo wanaita kuchumbia na baadaye soko likiwa zuri wanakuwa tayari walishazinunua zikiwa bado ziko mashambani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine limesemwa na shangazi yangu, Mheshimiwa Hawa Ghasia, la kuhusu kiwanda cha mbolea. Katika ukurasa wa 24 wa hotuba ya Waziri limeongelewa na hii ndiyo connection ambayo Mheshimiwa Zitto alikuwa anaitafuta. Niseme tu kwamba kwenye kitabu kuna maeneo ambayo yameongelewa connection ya uzalishaji pamoja na viwanda, mojawapo ni hili la kiwanda cha mbolea ambacho sisi tunakitegemea sana na liko katika ngazi ya Serikali pamoja na wawekezaji na Mheshimiwa Waziri atalielezea pia, atakaposimama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utitiri wa tozo, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha ameliweka vizuri na niseme tu tayari Waziri mwenye dhamana alishaelekeza kupitia kwa Katibu Mkuu anayeshughulikia mambo ya uwekezaji kwamba ataratibu ile timu ya Makatibu Wakuu, ili kuweza kujua tozo gani za kuondoa, lakini pia na kuweza kuunganisha zile ambazo zitaonekana zinatakiwa ziwepo ijulikane ni nani anatoza ili pasiwepo na huu utaratibu wa kila mmoja kwenda kwa wakati wake na kuleta usumbufu kwa wanaochangia ili waweze kufanya shughuli zingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili litaenda sambamba hata katika utaratibu wa kupata leseni ama vibali vya kufanyia kazi. Mtu akishamaliza eneo moja ajue kwamba tayari ameshamaliza katika utaratibu wa kupata vibali ili aweze kufanya shughuli zake za kibiashara. Serikali inalifanyiakazi kuweza kutengeneza mazingira ya kufanyia biashara katika nchi yetu ambayo ina fursa kubwa kuliko nchi nyingi za Ukanda wa Afrika Mashariki na Ukanda wa Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limeongelewa, amelisemea sasa hivi Mheshimiwa Mwamwindi linalohusu kinu cha Iringa. Vinu vingi vya Serikali vilikabidhiwa kwa Bodi ya Mazao Mchanganyiko na utaratibu huu tuliona pamoja na kwamba tuna NFRA ambayo yenyewe ni Hifadhi ya Chakula, tuliona tuwe na chombo kingine ambacho kinashughulika na mambo ambayo yanaweza yakawa ya kibiashara zaidi na hapo ndipo ambapo ilianzishwa hii Bodi ya Mazao Mchanganyiko. Katika jambo hili tumesema hawa wakiwa sehemu ya ununuzi na tukachukua na lile wazo alilolisemea Mheshimiwa Serukamba la kuunganisha na sekta binafsi wanaotaka kufanyakazi katika maeneo haya ya kununua mazao, tuna uhakika kwamba wakulima wetu watakuwa wamepata soko pia, watu hawa wataweza kuweka uwiano wa bei, wakati bei ziko chini waweze wao kujitokeza na wakati bei ziko juu waweze wao kujitokeza ili wakulima wetu wasipate hasara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wazo lake tunalipokea na wafikishie wana-Iringa kwamba, hoja yako uliyoitoa Mawaziri wote wawili mapacha wamelipokea kwa nguvu zote na watalifanyia kazi na waendelee kukupa heshima ya kukuchagua kwa sababu umewasemea vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo lilisemewa na Mheshimiwa Sabreena, amelisemea suala la zao la mchikichi kwamba halina Bodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, sisi kama Serikali jambo pekee ambalo tunaungana naye, Mheshimiwa Zitto Kabwe na yeye amelisemea mara nyingi kuhusu zao la michikichi ni kwamba tunahitaji kuimarisha uzalishaji wa mazao haya ambayo bidhaa zake tunaagiza kutoka nje. Jambo la kusema tuanze na Bodi kabla ya zao lenyewe halijaanza kuzalishwa ama halijaanza kuwa na tija, tutaleta mgogoro na tutaleta gharama ambazo hazihitajiki. Kwa hiyo, jambo ambalo tunalifanya kama Wizara ni kuhamasisha wakulima waone kwamba pana fursa katika jambo hilo. Sisi kama Serikali kuweka kila jitihada kusaidia pale ambapo patahitaji msaada kuhakikisha kwamba wakulima hawa wanasaidiwa, lakini tukianza kusema kila zao tuliwekee bodi hata ambayo hayajaanza kufanya vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema hata juzi wakati nahitimisha hotuba yangu, nikasema ni lazima tufanye tathmini, kila taasisi tunayoiunda uhalali wake uonekane kutokana na kazi unazozifanya. Leo hii kwenye mpunga hatuna bodi, lakini nchi yetu inapiga hatua, inajulikana hapa Afrika na inajulikana hapa duniani, kwenye mahindi hivyohivyo tunafanya vizuri, hatuna kesi ya kuibiwa, hatuna kesi ya wizi, hatuna kesi ya utapeli. Leo hii tukiwaza kwamba uwepo wa Bodi ndiyo utaibua mchikichi au utaibua alizeti, hili ni jambo ambalo mimi mwenye sekta nawashawishi lazima tutathmini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasema kwenye mpunga, kwenye mahindi, wanayo tu bodi inaitwa Bodi ya Mazao Mchanganyiko, tunasema bodi zisipoweza kuondoa uozo unaojitokeza kwenye mazao haya yenye bodi na kwamba kama uwepo wao haujaweza kusaidia, tutawaza uwepo wa chombo kimoja ambacho kitaitwa Bodi ya Mazao Mchanganyiko ili kuweza kuhakikisha kwamba tunaondokana na haya ambayo yanawakera watu wanaovuja jasho kila leo huku wakitozwa makato mengi kwa ajili ya uwepo wa taasisi nyingi ambazo tukienda kwenye uhalali haziwasaidii ama zimepunguza uhalali wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameongelea kuhusu kushuka kwa uzalishaji wa pamba. Mheshimiwa Ndassa, Mheshimiwa Kiswaga, Mheshimiwa Kemirembe, Mheshimiwa Njalu pamoja na Mheshimiwa Nyongo na Wabunge wengine wanaotoka maeneo yanayolima pamba akiwemo Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Dkt. Kalemani ambaye nimemuona ameongelea vizuri sana suala la umeme, akanikumbusha enzi za Mheshimiwa Rais akiwa Waziri, jinsi alivyoweza kutaja maeneo yale anayoyasimamia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wameliongelea kwa machungu suala hili la zao la pamba akiwemo ndugu yangu Mheshimiwa Kangi Lugola kutoka kule Mwibara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema tunarejea katika misingi tujue kitu gani kimepotea hapa hata uzalishaji ukashuka. Tumeshaweka timu yetu na tunategemea baada ya kuwa tumeshamaliza bajeti na pacha wangu hapa akamaliza ya kwake tunaenda sasa kwenye utekelezaji ili kuhakikisha kwamba tunatengeneza hii chain kuanzia kwenye uzalishaji tunaenda kwenye kutunza iliyozalishwa, tunaenda kwenye ku-process ambayo ndiyo inayoangukia kwenye Wizara yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Wabunge tumpitishie Mheshimiwa Waziri bajeti yake, tumpe kazi, ili tuweze kuanza hii ramani ya kwenda kwenye Tanzania ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja mia kwa mia na niendelee kusema kama mnaitaka mali mtaipata shambani na mali yenye tija inapatikana kwenye viwanda.