Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami nitoe mchango wangu kwenye Bajeti Kuu ya Serikali kufuatia hotuba ya hoja ya bajeti ambayo iliyowasilishwa na Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba Madelu wiki iliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo ameendelea kutoa uongozi uliotukuka katika taifa letu kwa muda huu mchache ambao ameanza kufanyakazi kama Rais. Kama ingekuwa kwenye mchezo wa mpira tungesema mama anaupiga mwingi sana kwa jinsi ambavyo anachukua hatua nyingi mbalimbali ambazo ni sahihi kwa nyakati sahihi. Nasema hivyo, kwa mfano hili ambalo amelizungumza Mheshimiwa Sanga (Jah People); kwamba mama jana tu ametoka kuzungumza kwamba riba kwenye mabenki ishuke na isiwe zaidi ya asilimia 10, hilo tu peke yake ni jambo kubwa sana kwenye kuchochea ukuaji wa uchumi katika taifa letu, hilo tu na mengine mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia hatua mbalimbali ambazo zimewekwa kwenye bajeti ya mwaka huu zinaonesha wazi kwamba mama ana dhamira ya dhati kabisa ya kutaka kukuza uchumi, kuchochea ukuaji wa uchumi, kutoa ajira nyingi pamoja na kuboresha huduma za kijamii kwa watu wetu; na kwa hili nina kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Lile alilolisema Mheshimiwa Sanga kwamba watu waache kufikiria mambo mbalimbali nadhani halipo. Mama anafanyakazi nzuri na sidhani kama kuna mtu ambaye atajaribu kukiuka utaratibu ambao tumejiwekea kwenye chama chetu, kuvuta fomu ya kuomba nafasi yoyote ile ya juu mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo kwa wale Wabunge wenzangu tuendelee kupambana majimboni, kwa wale ambao ni Mawaziri wapo kwenye front bench waendelee kupambana majimboni, waendelee kuchapa kazi wamuache mama afanyekazi kwa sababu anafanyakazi nzuri, na hakuna sababu ya kutikisa Taifa kwa uchaguzi ama kwa fununufununu zisizo na maana katika kipindi hiki ambacho mama anafanya mabadiliko makubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya kwanza baada ya utangulizi ni kwamba, taifa ili liendelee linahitaji mambo mengi, lakini katika mambo makubwa ambayo taifa linapaswa kuyatumia kama chachu ya kuleta maendeleo ni pamoja na maliasili zake (natural resources). Natural resources zinapaswa kuwa chanzo cha taifa lolote lile kuendelea. Sisi tumejaaliwa gesi lakini pia tumejaaliwa dhahabu. Pia taifa ili liendelee linapaswa kutumia nguvu kazi yake, kwa maana ya watu wake. Sasa haya mambo mawili ninayaona katika uchumi wetu bado hatujaya-exploit fully, hatujayatumia ipasavyo kuweza kuturusha kwenda mbele kwa kasi zaidi katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na nasema hivyo kwa sababu bado hatujaweza kutumia uchumi unaotokana na maliasili zetu kama dhahabu, kwa maana ya kuongeza thamani; jana tumefurahi kuona mama amezindua kiwanda kikubwa kule Kanda ya Ziwa cha kufanya refinery ya dhahabu, ni uelekeo sahihi; lakini tunaweza tukafanya vizuri zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunapaswa tuongeze speed ya uwekezaji kwenye sekta ya gesi ili maliasili ya gesi ambayo tumejaaliwa tuweze kuitumia kwa faida, kwa maana ya kuongeza thamani ili kutengeneza mbolea na baada ya kutengeneza mbolea hiyo gesi itaenda kuwa chachu ya kukua kwa uchumi wa mkulima ambaye atatumia ile mbolea. Kwa hiyo tuna haja pia ya kuwekeza kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mbali na hivyo jambo lingine kubwa ambalo linakosekana katika uchumi wetu ni mfungamanisho (linkage) kati ya sekta ya kilimo na sekta ya viwanda; hapa tuna changamoto kubwa, na changamoto hii inasababishwa kwanza na viwango viwango vikubwa vya kodi, lakini pili kuwepo kwa regulation ya hali ya juu na Serikali kuingilia kwa kiasi kikubwa sana kwenye utendaji wa sekta ya kilimo, kitu ambacho kinasababisha biashara iwe ina imbalances nyingi kutokana na kanuni nyingi ambazo zinatungwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo ili tuweze kuendelea na kuendeleza watu wetu ambao ni zaidi ya asilimia 65 na ambapo zaidi ya milioni 40 wanategemea sekta ya kilimo ni lazima tufanye value addition, tuongeze thamani kwenye mazao yanayolimwa na wakulima wetu. Sasa tukiweza kuongeza thamani ya mazao maana yake tutakuwa tumeongeza vyanzo vya mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa hivi ilivyo uchumi wetu Pato la Taifa linachangiwa kwa kiasi cha asilimia 25 mpaka 27 na watu zaidi ya milioni 40. Kwamba wale asilimia 65 ambao wanategemea shughuli za kilimo wanaokaribia milioni 40 ya Watanzania wote wanachangia kwenye Pato la Taifa kwa asilimia takriban kati ya 25 mpaka 27 tu. Sasa hawa ni watu ambao kwanza hatuwatozi kodi, kwa sababu hakuna mchungaji anayetozwa kodi ya mifugo zaidi ya milioni 30 ambayo tunajivunia kuwa nayo, lakini pia wakulima hawatozwi kodi. Sasa ili tuweze kupata kipato kutokana na hawa watu zaidi ya milioni 40 ni lazima kuwe kuna namna ambavyo kuna value addition kwenye ile shughuli kubwa ya kiuchumi wanayoifanya ili sasa kule ndiko tukapate kodi, kwa sababu kwenye mazao hatutozi kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ushauri wangu ni kwamba, tunakoelekea huko itafutwe namna ya hawa watu zaidi ya milioni 40 kuchangia kwa kiasi kikubwa kwenye Pato la Taifa. Tutaweka kodi gani, maswali hayo wataalam wanaweza wakayatazama, lakini kwamba tutafanya nini kuna uwezekano mkubwa, kama tutafanya value addition kwa kuwezesha ujenzi wa viwanda ambavyo vinafungamanisho la moja kwa moja na shughuli ya kilimo, mifugo na uvuvi, basi kule kwenye viwanda tutapata kodi ambayo itasaidia kuchangia kwenye uchumi wa taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye fungamanisho napenda kutoa mfano, amezungumza Mheshimiwa Mbunge mmoja hapa wakati anachangia, kwamba kulikuwa kuna kongamano jana la alizeti pale Singida; na nina-declare interest, mimi nina kiwanda cha kusindika mafuta ya alizeti. Nilikijenga mwaka 2009 huko kabla sijaingia kwenye siasa. Tangu nimekijenga kiwanda hicho mpaka leo hatujawahi kufikisha uzalishaji wa mafuta kwa zaidi ya tani walau elfu 10, na kiwanda kikubwa ambacho kwa mwaka mmoja kinaweza kikafanya volume ya tani elfu 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu kubwa, ya kwanza tunafeli kwa sababu hakuna raw materials hakuna malighafi ya kuingiza kiwandani. Kwa hiyo tunaendelea kuhamasisha watu wawekeze kwenye uchumi wa viwanda, lakini watu wakiwekeza kwenye uchumi wa viwanda hakuna malighafi ya kupeleka kwenye viwanda. Sasa kwanini inakosekana malighafi ilhali Watanzania zaidi ya milioni 40 ni wakulima? Maana yake hapo kuna miss match, hapo kuna gap kubwa ambalo sisi kama Serikali tunapaswa kuliziba, tunapaswa kulifanyia kazi. Kwamba ni namna gani wakulima wetu watazalisha na hatimaye wanachokizalisha kiingie kwenye viwanda ambavyo vinajengwa? Kwa hivyo tunahitaji kufanyia kazi jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sababu kubwa nyingine ya pili ni kwamba, kwenye uchumi wa viwanda ukishakuwa tu mfanyabiashara kwenye nchi yetu unakuwa labeled kwamba huyu anataka kuwaibia wakulima, ana lengo baya na wakulima, anawaminya wakulima. Dhana hiyo inasababisha kwa kiasi kikubwa sana kutokushamiri kwa uwekezaji kwenye eneo la viwanda, lakini pia mahusiano hasi kati ya Serikali wakulima na wafanyabiashara; jambo ambalo kama lingerekebishwa, na ni jambo tu la mindset, basi tungeweza ku-unlock potential kubwa sana ambayo ipo kwenye uchumi ambao unategemea zaidi kilimo, kwa maana ya kufanya backward linkage kati ya kilimo na viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine kikubwa ambacho ningependa kukisema ni kwamba tax rate, kiwango cha kodi kama Mheshimiwa Mwigulu ataenda ku- review mchumi mmoja anaitwa Arthur Laffer akasoma ile Laffer Carve ataweza kutusaidia sana kama taifa kutunga viwango vya kodi ambavyo ni rafiki kwenye kukua kwa uchumi pamoja pia kwenye kuongeza kipato cha Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimalizie tu kwanza kwa kumpongeza kwa hotuba nzuri ambayo aliiwasilisha hapa; kiukweli hotuba yake ilikuwa kama muziki kwenye masikio ya Waheshimiwa Wabunge wakati akiiwasilisha na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante sana…

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALA: …ana-deserve credit zote japo kuwa Mheshimiwa Mwigulu ni Yanga hilo ndilo tatizo alilonalo tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwashukuru na ninaunga mkono hoja.