Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 iliyowasilishwa hapa Bungeni na Waziri wa Fedha tarehe 10, Juni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kidhati kuipongeza Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuja na bajeti iliyobeba matumaini mapya kwa Watanzania.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee maeneo mawili makubwa ambayo bajeti hii imekuja na matumaini mapya. Mosi; bajeti hii imekuja kujibu lile swali ambalo Watanzania wamekuwa wakijiuliza kuhusiana na uendelezaji wa miradi yetu ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiisoma bajeti hii – naomba kunukuu – inasema hakuna mradi hata mmoja utakaokwama bila kusimama hata kwa mwezi mmoja. Na maneno haya yanachukua uhalali wake kwenye maneno aliyoyasema Rais wetu tarehe 06, Aprili, pale Ikulu, Dar es Salaam akiapisha Makatibu Wakuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema, naomba kunukuu;

“Tuna urithi aliyotuachia marehemu Rais wetu; miradi mikubwa miwili” – akimaanisha Mradi wa Bwawa la Nyerere na Mradi wa Standard Gauge – “na miradi mingine midogomidogo.”(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais anaendelea kusema; wanasema ukifanya vibaya kwenye urithi, Mungu anakulaani. Aliyekuachia urithi hana radhi na wewe, na Mungu atakulaani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ingawa siyo maneno ya Mheshimiwa Rais, lakini naamini neno urithi unaweza ukaliondoa ukaweka neno wosia. Kwa maana yako maneno aliwahi kuyasema mwendazake. Naomba kunukuu;

Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliwahi kusema, akizungumzia miradi hii mikubwa ya kimkakati, alisema;

“Mimi ni dereva tu, lakini pia najiuliza, ikiwa siku moja Mungu atanichukua hawa wanaokuja watakuja kuyamaliza kweli?”(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni imani yangu tarehe 06, April wakati Mheshimiwa Rais anaelezea ule urithi, alikuwa anazungumzia kauli hii. Na ukisoma sentensi hizi, maneno aliyoyasema Hayati Magufuli, liko neno ikiwa siku Mungu atanichukua. Hakuelezea kwamba ikiwa atafika mwisho wa ukomo wa utawala wake kwa mujibu wa Katiba; ni maneno mazito sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nasema bajeti hii imekuja kujibu kiu ya Watanzania, imekuja kujibu wosia aliotuachia Hayati Magufuli na imekuja kutekeleza kauli ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inakwenda kutekelezwa na kukamilika kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili; bajeti hii imekwenda kutoa majibu ya kero zilizosemwa hapa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge. Ukiangalia mijadala yote, kuanzia tunajadili Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, mjadala wa bajeti mbalimbali, siamini kuna Mbunge yeyote alisimama hapa hakuzungumzia barabara zetu zinazotekelezwa kwa kusimamiwa na TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge hapa waliongea kwa hisia kubwa. Na mimi nilikuwa mmoja wao na nilikuwa nasubiri bajeti hii niangalie Serikali imejipangaje kuongeza fedha kwa TARURA. Ukurasa wa 72 zimetengwa shilingi bilioni 322,158,000,000 kwa ajili ya barabara zetu za TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku hapa hakukosi swali la Wizara ya Maji. Na hisia za Wabunge zilijionesha sana kwenye bajeti ya Wizara ya Maji. Bajeti hii imekuja kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la afya; kwenye majimbo yetu wananchi wamejenga maboma, Serikali imeshindwa kumalizia. Pamoja na ujenzi mkubwa wa miundombinu ya afya, vituo vya afya, vifaatiba, wataalam, dawa; bajeti hii imekuja na mwarobaini wa kutatua kero hizi za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yako maeneo mengi ambayo bajeti hii imeyagusa. Lakini naomba niseme; ili kufadhili miradi ya maendeleo – wataalam wa uchumi wanafahamu na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni mtaalam wa uchumi – ziko njia nne. Njia ya kwanza ni mikopo, ya pili ni misaada, ya tatu ni fedha zetu za ndani, na ya nne ni venture capital ama PPP ama miradi inayosajiliwa na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hii tunayoikopa tukisema tutatekeleza miradi yetu kwa mikopo tunabebesha Taifa letu mzigo wa uchumi wa sasa, watoto wetu na wajukuu zetu. Leo kwenye bajeti hii deni la Taifa ni himilivu kwa mujibu wa international standards ambazo zinataka deni la nje lisizidi asilimia 50; deni la Taifa letu ni asilimia 17. Deni la nje na ndani ukichanganya kwa pamoja kwa vigezo vya kimataifa halipaswi kuvuka asilimia 70; leo sisi tuko asilimia 27, tunafanya vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ziko nchi za majirani zetu, takwimu hizi zipo, zimekopa mpaka sasa ziko nje ya vigezo hivi. Lakini maeneo mawili salama, ukiacha eneo la misaada ambalo wote mnafahamu misaada hii inakuja na masharti, na masharti mengine ni magumu, hatuwezi hata kuyataja humu kwenye Bunge hili, tunabaki na maeneo mawili salama zaidi ya ku-finance miradi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo kwanza ni kodi zetu sisi wenyewe. Naomba ninukuu maneno ya Hayati Dkt. Magufuli aliyoyasema kule Kyela; alisema tunajenga vituo vya afya, barabara kwa fedha zetu. Alisema Tanzania inatakiwa iwe mfano kiuchumi katika dunia, yale mawazo ya kufikiri kuna mtu ataleta misaada tuyapoteze kichwani, ule ni ugonjwa mkubwa. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliwahi kusema; Serikali isiyokusanya kodi ni Serikali ya wala rushwa. Lakini pamoja na TRA na Serikali kupambana kuongeza wigo wa kodi, mpaka sasa walipa kodi walioko kwenye tax base ya TRA ni watu milioni mbili na laki saba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini? Kwa sababu tulikuwa kwenye semina pale Ijumaa; sekta kubwa ya Watanzania iko kwenye sekta isiyo rasmi. Kwa hiyo, ukisema unapanua wigo wa kodi utabaki palepale kwa watumishi, palepale kwa walimu wetu, palepale kwa wafanyakazi wetu, palepale kwa kuwaumiza wafanyakazi kwa kodi za mishahara yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini upande wa pili…

NAIBU SPIKA: Sekunde 30.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini upande wa pili, tunao mtandao mkubwa wa watumiaji wa simu za mkononi kwa laini zisizopungua milioni 52; hawa ndi Watanzania wanaoteseka kukosa dawa. Tunayo miamala ya fedha kwa Januari mpaka Desemba, 2020 ya jumla ya trilioni 201; hapa wako wanaotuma miamala tukiwemo wale tunaotuma na ya kutolea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Watanzania tukubaliane kugharamia bajeti yetu sisi wenyewe. Waziri wa Fedha ameupiga mwingi sana tarehe 10, ametoa hotuba nzito sana, ameupiga kama Bernard Morrison, siyo Morrion huyu, Morrison yule aliyekuwa Dar Young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi/Vigelegele)