Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuhitimisha hoja. Kwa kuanzia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hii, imechangiwa na zaidi ya Wabunge 23 kwa kuongea na Wabunge watatu wamechangia kwa maandishi. Niwahakikishie tu kwamba hoja ambazo huenda hatutazitolea majibu hapa zingine tutazitolea kwenye hotuba kuu ya Serikali na zingine tutazitolea kupitia Finance Bill zile ambazo zimekaa kwa muundo wa masuala ya kisheria na zingine tutaendelea kuzitolea majibu kwa njia ya maandishi.

Mheshimiwa Spika, la pili, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kutoa ufafanuzi wa kina wa hoja. Navyomuona Mheshimiwa Naibu Waziri wangu kadri tunavyoenda na yeye atapata ubatizo kama ule aliopewa Waziri wa Ulinzi ambaye ni Mhasibu lakini alishabatizwa na alishapewa degree kwamba yeye ni engineer, namuona Naibu Waziri wangu akiwa mchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianzie pale alipoishia Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa King aliuliza ile asilimia tatu ya VAT ambayo inatofautiana kati ya asilimia 18 ya Mainland na ile ya 15 ya Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa zile bidhaa ambazo haziko kwenye kodi ya Muungano na zile ambazo ziko kwenye masuala ya VAT kwa ngazi ya bidhaa za viwandani ambazo kwa sheria ambayo ilikuwa inatumika mpaka hivi sasa ziko zero rated. Kwa maana hiyo, mwananchi anaponunua hizo bidhaa ambako zipo zero rated hatozwi kodi huko anakonunulia anakwenda kutozwa kodi ya VAT kule kwa mtumiaji. Kwa maana hiyo ile tofauti ya VAT hiyo asilimia 18 na 15 inakuwa haimgusi kwa sababu anakuwa hakutozwa kule wanakotoza 18 anakwenda kutozwa kule wanakotozwa 15, kwa hiyo, anakuwa ametoa tu ile ile ambayo inastahili.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa bidhaa zile ambazo bei zake ama utozwaji wake unatozwa maeneo tofauti, hilo ni jambo ambalo kama alivyoelezea Mheshimiwa Naibu Waziri limefanyiwa kazi na tuko kwenye hatua za mwisho za kulimalizia. Tunaamini ndani ya hizi siku mbili tutakavyokuja kwenye hatua zinazofuata tutakuwa tumeshakamilisha utekelezaji wake utakavyokuwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa King na nimpongeze kwa uchangiaji wake. Nimhakikishie kwamba kipengele cha kwanza ambacho tumekielezea kipo vile lakini kile ambacho kilikuwa na matatizo kidogo kwa zile bidhaa ambazo hazikuwa zero rated tutakipatia majibu tunavyokuja kwenye hizo hoja kubwa zinazokuja hapo baadaye.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa King aliongelea pia zile fedha na alitaja kiwango kama shilingi bilioni 28, kama nimempata vizuri, ambazo zilitakiwa zirudishwe Zanzibar. Ni kweli kulikwepo na jambo la aina ile na kama alivyoeleza mawasiliano kati ya Wizara ya Fedha na Mamlaka ya Mapato yamefanyika na kiasi cha fedha tayari kilishapelekwa Zanzibar ambacho kilikuwa kinatokana na Excise Duty. Kwa upande wa kiwango kikubwa kile ambacho kilikuwa bado hakijapelekwa lilikuwa jambo la mawasiliano na mimi nielekeze leo hii Kamishna wa Mapato Tanzania pamoja na pacha wake wa Zanzibar wakae wamalize usuluhishi wa takwimu zile ambazo zilikuwa zinawakwamisha ili waweze kutatua tatizo hilo. (Makofi)

Muungano wa Tanzania Bara na Zanzibar ni Muungano wa kindugu, hatuwezi tukatofautiana kwa kushindwa tu kuzioanisha takwimu hata tukaenda kwenye manung’uniko. Huu siyo Muungano wa Amri ya Mahakama, ni Muungano wa kindugu, kwa hiyo, takwimu haziwezi zikatupa hiyo shida na hata tukashindwa kuziweka sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilitolewa na Mheshimiwa Mpina kuhusu ukusanyaji na akaelezea kuhusu hizo taasisi alizozitaja TANAPA, Ngorongoro, TAWA na kama je, kushuka kwa makusanyo kwa kiwango hicho ni Covid peke yake? Ni kweli kunaweza kukatokea matatizo mengine hasa katika taasisi zingine lakini kwa kesi ya TAWA, Ngorongoro pamoja na TANAPA hizi ni moja ya taasisi ambazo ziko kwenye sekta ambayo iliathirika kwa kiwango kikubwa zaidi na masuala haya ya Covid. Hii inatokana na idadi ya watalii waliotembelea katika hifadhi hizo, baadhi ya nchi mliona zilifungia wananchi wao kutoka. Kwa hiyo, ni dhahiri kwenye eneo hilo kidogo tunaweza tukapata matatizo ya aina hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini hoja zingine zilizotolewa, kulikuwepo na hoja kama misaada ambayo inaenda Zanzibar ni lazima ipokelewe na Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? Ndugu yangu mpaka alianza kusema Waziri wa Fedha wa Tanzania Bara. Kwenye hili sheria imeshaweka wazi na utaratibu ule ndivyo unavyotumika. Waziri wa Fedha wa Zanzibar sheria imempa nafasi ya kukasimiwa kupokea misaada pamoja na taasisi nyingine ambazo zimeelekezwa kwenye sheria ambazo zenyewe si lazima Waziri wa Fedha aweze kupokea.

Mheshimiwa Spika, maeneo pekee ambayo Waziri wa Fedha anahusika ni yale ambayo yanatumia Kamati ya Madeni kama ambavyo Kamati ya Bajeti ilisema, yale ambayo Kamati ya Madeni ni lazima ishauri kuna umuhimu wake. Maana hoja ilikuwa inatolewa kwamba kwa nini hata misaada ipitie kwenye Kamati ya Ushauri. Jambo hili liliwekwa kwa makusudi kwa sababu kuna mazingira ambapo misaada inaweza ikawa na masharti ndani yake ambayo kwa ukubwa wake ama kwa ugumu wa masharti yale yasipofanyiwa tathmini ya kina yanaweza yakawa na athari kwenye Taifa. Vilevile kuna baadhi ya misaada katika utekelezaji wake kwa sheria zilizokuwepo ina masharti ya kikodi ndani yake kwa maana hiyo na yenyewe lazima implication zote ziwe zimepitiwa na zimeridhiwa kuweza kuona namna ya kutumia.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kipengele hiki kinachohusisha masuala ya misaada kinafanyiwa kazi kwa kina na ndani ya siku hizi mbili tutakuwa na majibu kuhusu baadhi ya maeneo. Pia baadhi ya misaada inaweza ikawa na masuala ya kiusalama ambayo lazima yawe yamezingatiwa ili kuweza kuhakikisha kuwa inaenda kutumika huku tukiwa na uhakika na matumizi yake.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo liliongelewa, Kamati imeshauri Serikali kuhamasisha Serikali za Mitaa kuwa na mabadiliko na maandiko ya miradi ambayo ina sura ya kibiashara itekelezwe kwa mfumo wa PPP. Siku hizi mbili, tatu tumekaa na mabenki yote yaliyoko hapa na tume-share nao utaratibu huu unaopendekezwa na Kamati na tumeshirikiana nao na tumegawanya miradi ambayo ni zaidi ya miradi 75 wameichukuwa na baadhi yao wameshafika hatua ambazo ni za juu tunategemea baada ya hapo watasema kila mmoja ambao wameona wanaweza wakatekeleza. Hili ni wazo jema tu ambalo linaweza likafanyika, miradi ile ambayo ni ya kibiashara kama masoko, stendi pamoja na vitu vingine ambavyo vinaweza vikawa vya kisasa vinaweza vikanyiwa tathmini za kina na vikafanywa kwa utaratibu huu wa PPP. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri mwingine ambao umetolewa ni mtizamo hasi kuhusu miradi ya PPP ni changamoto kubwa kwa Serikali katika kutekeleza miradi ya PPP, Serikali itatue changamoto hii. Hili suala la mtazamo hasi kwenye miradi ya PPP si jambo la Serikali peke yake, hii ni mindset ya nchi nzima, ni mindset ya wananchi. Kwa hiyo, upande wa Serikali, Serikali inaundwa na wananchi, viongozi walioko Serikalini wote wanatokana na wananchi, viongozi wanatokana na Watanzania, hili suala la mindset kuhusu PPP ni jambo kubwa ambalo na lenyewe lazima tuanze kupeana elimu kuhusu utekelezaji huu.

Mheshimiwa Spika, mwanzoni wakati tunapata Uhuru ni dhahiri kwamba Serikali ingeweza kutelekeza miradi yote na wakati uleule ikatoa huduma za jamii, kwa sababu idadi ya wale ambao walikuwa wanatakiwa kupewa huduma chukulia mathalani elimu walikuwa wachache tu, ngazi zote unazozitaja walikuwa wachache tu, ukienda kwenye afya hivyo hivyo walikuwa wachache. Pia hata kwenye huduma zingine kama za maji, katika enzi ile maji yalikuwa yanapatikana tu kila eneo. Kwa maana hiyo Serikali ingeweza kutekeleza vizuri miradi yote ya maendeleo kwa kutumia mkono wa Serikali na wakati uleule ikatoa huduma. Sasa kwa mabadiliko haya niliyoyasema ni dhahiri kwamba uhitaji wa kutekeleza miradi kwa kutumia PPP ni mkubwa zaidi ili Serikali iweze kutekeleza majukumu ya kutoa huduma za jamii ambayo ni ya msingi na ni majukumu ya lazima kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, hili la mindset ni jambo ambalo linatakiwa lianze kidogokidogo kueleweka kwa Watanzania. Kwa sasa hivi Tanzania akitokea mwekezaji yuko na mtaji kamili, tutolee mfano tu, anataka kuleta meli ya uvuvi kwenye kina kirefu (deep sea fishing), ana mtaji kamili wa kuleta meli. Wale samaki wapo pale msipowavua wanaweza wakatembea wakavuliwa kwingine na anapanga aweke hiyo meli. Akitoka kwenye meli, natoa mfano, ajenge na bandari ya uvuvi kwa ajili ya lile limeli likubwa la kwenda kuweka nanga pale na kupakua. Akitoka pale aweke na kiwanda cha kuchakata samaki; awe na mtaji wote ule uko kamili. Kwa mindset ya Kitanzania tulio wengi, swali la kwanza utakuwa unasikia; hivi huyu ana mtaji kweli huyu, siyo tapele kweli huyu?

Mheshimiwa Spika, wakijiridhisha siyo tapeli, swali la pili, hivi huyu hatatuibia kweli? Wakijiridhisha na hilo, kwamba hivi huyu hatatuibia, maswali yakiwa mengi akitokea mmoja akasema nadhani hili wazo ni zuri, swali la tatu kwa Watanzania walio wengi litakuwa hivi huyu anayesema hivi hajala chochote kweli?

Kwa hiyo ni mlolongo wa maswali matatu ndiyo unaoua PPP. Moja, je, siyo tapeli? Wakigundua siyo tapeli, la pili; hatatuibia? Wakibishana akatokea mmoja akasema nadhani hatatuibia; hivi huyu anayesema hatatuibia hajala chochote kweli huyu? Hii ndiyo inayoua PPP. Haya masuala ya PPP ni lazima yaendeshwe kwa kuaminiana.

SPIKA: Hata Spika akisema wanasema inaelekea kahongwa huyu. Ndipo tatizo letu lilipo hapo. (Kicheko)

Mheshimiwa Waziri, endelea tafadhali.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utaratibu wa PPP kwenye miradi ambayo inaweza ikawa ya kibiashara ni jambo ambalo linatakiwa litolewe elimu na watu waelewe na ni utaratibu ambao unaweza ukaipa nafasi Serikali kutekeleza miradi ya maendeleo. Kwa hiyo hata waandaaji pia wa kwenye miradi bado iko vile. Hata Serikalini hilo bado lipo pia; kukiwa na line moja inahusisha PPP na kukawa na line nyingine kwamba inaweza ikatumia bajeti ya Serikali, itakayochangamkiwa ni ile ya bajeti ya Serikali. Hayo ndiyo mazoea. Hata kama itasuasua itakuwa tu hiyo ndiyo ambayo inapewa kipaumbele kikubwa kwa sababu ni mazoea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili ni jambo ambalo linatakiwa liangaliwe na sisi huku tutaendelea kuwasisitizia wataalam wetu wafuate vile vigezo ambavyo vinatakiwa, wafanye miradi ambayo inaweza ikawa ya mfano, lakini pia waendelee kutoa elimu kwa kutumia miradi ambayo ni ya mfano ili watu waone kwamba ni jambo ambalo linawezekana.

Mheshimiwa Spika, Kamati inashauri Serikali kuacha utaratibu wa kutenga fedha Fungu 21 zinazohusu watumishi kwa ajili ya kupandisha madaraja; utaratibu uliopo sasa hivi ni kwamba, fedha za kupandisha madaraja zinatengwa kwenye Mafungu husika. Hata hivi sasa katika mwaka huu wa fedha, zaidi ya bilioni 209 zimetengwa katika Mafungu husika, isipokuwa fedha ambazo zinawekwa kwenye Fungu 21 ni zile tu ambazo watu wake hawajajulikana watakaopandishwa.

Mheshimiwa Spika, kama haijajulikana ni akina nani watakaopata uteuzi, ni akina nani watakaokuwa katika fungu hilo mahususi; zile fedha ndiyo zinawekwa pale kwa ajili ya kusubiria hitaji kamili litakavyokuwa wakati utakapofika.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo limeongelewa kwa kiwango kikubwa ni hili la kwamba Kamati inashauri Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba inapitia kanuni na taratibu za utolewaji wa misamaha ya kodi, ifanyike haraka kuepuka ucheleweshaji. Jambo hili linaendelea kufanyiwa kazi, liko hatua za mwisho. Kama nilivyosema, tutakavyokuja katika siku hizi mbili zijazo tutakuja na jambo hilo tukiwa tumelisemea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Waheshimiwa Wabunge wameliongelea kwa kiwango kikubwa, lilikuwa ni ile miradi ambayo ni pamoja na wa Mara, wa Zanzibar na wa Dodoma. Nitoe tu taarifa kwamba hatua ambazo Wizara ya Fedha ilitakiwa kuzifanya ilishafanya. Wizara ya Fedha ilishafanya mapitio na kuona umuhimu wa miradi hiyo katika kukabiliana na athari za tabianchi. Tarehe 12, Aprili, ilitoa vibali vyote kwa NEMC kuendelea na utekelezaji wa miradi hiyo. Kwa sasa NEMC wanaendelea kukamilisha taratibu zake za ndani kwa ajili ya kuhakikisha kwamba fedha hizo zinatoka BOT na kuendelea katika utekelezaji wa miradi husika. Hata hivyo, tunaendelea kutafuta jawabu la kudumu ili kuondoa huo ukiritimba ambao umejitokeza katika jambo hili na siku si nyingi tutatolea kauli jambo la aina hiyo.

Mheshimiwa Spika, kulikuwepo pia na ushauri uliotolewa ambao ulikuwa unahusu michango ya watumishi kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ipelekwe kwa wakati. Huu ushauri tumeupokea na tutatoa majibu tutakapokuja kwenye hotuba hizi za siku mbili ili tuweze kutafuta jawabu la kudumu kwenye tatizo hilo lililotajwa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wameshauri kuhusu Wakaguzi kuhamia kwa CAG na wengine wamesema kuhamia kwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani. Kuna umuhimu wa Wakaguzi wa Ndani kuwa huru na kutoingiliwa na mamlaka wanazozikagua. Kwa mujibu wa muundo, Wakaguzi wa Ndani wote wapo chini ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali. Hata hivyo, utaratibu wa shughuli za utendaji na utawala za kila siku za Wakaguzi wa Ndani zipo chini ya mamlaka ya Maafisa Masuuli ili kusaidia kudhibiti mifumo ya mapato na matumizi ya taasisi husika.

Mheshimiwa Spika, aidha, taarifa za ukaguzi zinazoandaliwa na Wakaguzi wa Ndani kwenda kwa Maafisa Masuuli hunakiliwa kwa Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali. Hivyo, Wakaguzi wa Ndani ni sehemu ya muundo wa Mkaguzi Mkuu wa Ndani.

Mheshimiwa Spika, tumepokea ushauri na mapendekezo yaliyotolewa. Kilichokuwa kinatumika kwa sasa hivi, kuwapeleka moja kwa moja kwenda kwa CAG ingetengeneza line nyingine ya Wakaguzi wa Nje, kwa sababu tayari tuna safu ya Wakaguzi wa Nje na tuna safu ya Wakaguzi wa Ndani na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge alifafanua hapa, Wakaguzi wa Ndani kimsingi walitakiwa wawe jicho la kuonesha mambo yanavyokwenda na wawasaidie Maafisa Masuuli.

Mheshimiwa Spika, tukiwa hatuna pia Wakaguzi wa aina yoyote mule ndani kwenye ofisi zetu, kuna tatizo lingine litajitokeza, watakuwa wanafanya makosa yote yale wanasubiri mpaka waje wale wanaotoka nje kuja kuwaambia mmefanya makosa moja, mbili, tatu, nne. Kwa maana hiyo, kilichokuwa kinatakiwa, na hivyo ndivyo ambavyo inatakiwa na ndivyo ilivyokusudiwa, hawa wakaguzi ambao wako ndani mle wanapaswa kushauri na ku-control, lakini pia taarifa zao wanazipeleka katika line ile nyingine.

Mheshimiwa Spika, ni ajabu kwa wale ambao watakuwepo palepale ndani halafu waka-compromise taaluma zao wakashiriki katika uovu ambao utakuwa umejitokeza na kusubiri yule mwenzake ambaye ana taaluma sawa na yeye aje amwambie kwamba hapa mlikuwa mmekosea.

Mheshimiwa Spika, ikitokea Maafisa Masuuli wakafanya makusudi kwa kuwahamisha wale Wakaguzi wa Ndani ambao kimsingi wanatakiwa wawasaidie, nisitumie neno lingine, nitumie lilelile ambalo Mheshimiwa Kilumbe ametumia, itakuwa ni kukosa busara ama itakuwa ni bahati mbaya sana. Kwa sababu Serikali ni moja na Serikali ndiyo iliyoanzisha idara hizi zote na Serikali ina uchungu na fedha za walipakodi, kwa hiyo isingeweza kuogopa kukaguliwa, Serikali inahitaji kuona fedha zake zinatumika kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, hili la upande wa watumishi wa TRA, tumepokea ushauri huo na Naibu Waziri amelisemea vizuri, ni suala la kiutawala tutalifanyia kazi. Ni jambo ambalo kwa kweli lina umuhimu huo kwa sababu tunahitaji kuimarisha utaratibu vizuri sana kule kwenye upande wa mapato. Kwa sababu hatuwezi tukatekeleza miradi ya maendeleo bila kupata mapato.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo liliongelewa na Waheshimiwa Wabunge kuhusu kuweka ukomo wa uhakiki wa malimbikizo ya madeni. Tumelipokea hili la masuala ya madeni na lenyewe kama ambavyo unaweza ukaona, Serikali imeendelea kuweka uzito mkubwa unaostahili kwenye masuala ya madeni.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha huu unaomalizikia, Serikali ilitenga zaidi ya bilioni 600 ambazo zimekwenda kwenye kulipa madeni ya watoa huduma wa ndani. Hata katika bajeti hii inayokuja tumetenga fedha za kutosha ambazo zitakuwa zaidi ya bilioni 600 kwa ajili ya masuala ya madeni ya watoa huduma wa ndani. Hata hivyo, tunapanga kuharakisha utaratibu ule wa uhakiki ili kuweza kuhakikisha kwamba watu wetu hawakwamishwi na hawacheleweshewi malipo yao ama madeni yao wanayodai Serikalini kwa sababu tu ya suala zima la uhakiki.

Mheshimiwa Spika, Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge wameongelea kuhusu utaratibu wa hatua za kuchukua kukabiliana na masuala ya COVID-19, hasa kwa taasisi ambazo zimeathirika pakubwa zaidi. Serikali imeendelea na utaratibu huo ikiwepo kushusha viwango vya riba vinavyotozwa na Benki Kuu wakati mabenki yanapokopa kutoka asilimia saba kwenda hadi asilimia tano, kushusha viwango vya chini vya kisheria ambavyo ni sehemu ya amana ambapo benki zingine zinatakiwa ziweke Benki Kuu kutoka asilimia saba kwenda asilimia sita.

Mheshimiwa Spika, pia hatua nyingine ambazo zimechukuliwa ni zile za kuendelea kugharamia mahitaji ya taasisi za utalii pamoja na TANAPA, TAWA na Ngorongoro, kuongeza kasi ya kulipa madeni kama nilivyosema, ili kuweza kuwawezesha wale ambao walikopa na wameshatoa huduma na wanatakiwa waweze kuendelea na shughuli zao ambazo walikuwa wanazifanya.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuongeza wigo wa kaya zinazonufaika na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kama ambavyo mliona katika hotuba ya Waziri mwenye sekta; Lingine ni kuongeza wigo wa upatikanaji wa mikopo ya gharama nafuu kwa wajasiriamali wadogowadogo na wa kati; na Lingine ni kuendelea kuhakikisha halmashauri zinatenga fedha za asilimia 10 ya mapato kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, haya yote ni hatua ambazo zinalenga kupunguza yale makali na kuweza kuchochea uchumi wetu kwa kuongeza ukwasi kwenye mzunguko wa uchumi ili shughuli za uzalishaji ziweze kuendelea na kuweza kulinda ajira za watu wetu katika kipindi hiki ambacho chumi zimepitia misukosuko kutokana na jambo hili ambalo lilikuwa linaendelea duniani kote.

Mheshimiwa Spika, kulikuwepo na ushauri uliotolewa kuhusu masuala ya watu wenye bureau de change na Mheshimiwa Mbunge alisema nitafute muda tukutane nao; bureau de change wale wa Arusha tulishakutana nao na tumeongea, tumewasikiliza, walikuja ofisini, tumeongea na tumewaelewa.

Mheshimiwa Spika, tutachukua hatua na tulishaelekeza timu ndogo inafanyia uchambuzi wa namna ya kuweza kushughulikia jambo hilo. Nakumbuka Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, alikuwa anakwenda mguu kwa mguu na Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Arusha Mjini; alikuwa anakwenda mguu kwa mguu na leo hii Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum amelileta hapa; tulishakutana nao.

Mheshimiwa Spika, nimesikia hata Mbunge wa Iringa Mjini alikuja nalo pia; ni jambo kubwa, linahitaji katahadhari katika kulibeba. Mheshimiwa Paresso, tumelibeba jambo hilo, tutalifanyia kazi kiutawala, pamoja na maeneo mengine ambayo yanahusiana na jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Tarimba aliniambia nimpe na dondoo kuhusu tarehe 3. Mheshimiwa Tarimba hilo ni dogo tu; tarehe 3 wale wakija na paka, wananchi ninyi nendeni na mbwa tu, paka wote wataondoka halafu muweze kufanya shughuli kama mnavyotaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naafiki.