Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu sana Wizara ambayo inatunza rasilimali za Watanzania na niseme tu nampongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyoendelea kwamba mpaka sasa hivi hatuna mradi wowote ule ambao una sua sua miradi yetu ya kimkakati yote inaendelea vizuri certificate zote zinalipwa kwa wakati kwa hiyo ni pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais wetu, lakini zaidi pia kwa kutenga fedha bilioni 372.6 kwa ajili ya kipande cha Isaka Mwanza cha SGR, na kama hiyo haitoshi kwa kutoa fedha bilioni 187 kwa ku-support TARURA kupata miradi ambapo kila Jimbo limepelekewa Milioni 500 na mimi za Jimbo langu nimeshataarifiwa zimeshafika na mipango kule inaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tukitoka hapo tunazungumza suala leo la Wizara ambayo inakusanya mapato ya nchi yetu na changamoto zake tumepokea changamoto nyingi hapa wakati tukipokea taarifa za kila Wizara, baadhi ya Taasisi kushindwa kufikia malengo sababu wanaeleza ni Corona, na mimi niseme kwamba ni kweli kabisa Corona inaweza kuwa imechangia kupunguza mapato yetu. Lakini haiwezi kulingana na maeneo pengine ambazo waliweka lockdown wakazuia kila kitu hali zao ni mbaya zaidi. Na kwa hili ninataka nimpongeze sana Hayati tinga tinga Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alivyotusimamia vizuri sana katika hili eneo madhara ya Corona sisi hatujadhulika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninachotaka nitahadharishe hapa pia isije ikawa kinga watu wamekuwa wazembe kule kukusanya mapato ya Serikali alafu wanakuja hapa wanasema Corona, na Wizara ya fedha mnafuatilia namna gani kwenda kujiridhisha kweli sababu hizi zinazotolewa ni za kweli mnajiridhishaje mnafuatilia mkiambiwa Corona tu mnasema ni Corona kweli au kuna sababu zingine? Kwa mfano, tumeelezwa anguko kubwa sana la Taasisi za TANAPA, NCAA pamoja na TAWA ambao walipanga kukusanya bilioni 584 wameweza kukusanya bilioni 89 tu katika kipindi cha kufikia mwezi wanne, sasa kweli sababu ni hizo tu sababu ni Corona au zipo sababu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Wizara ya Mifugo na Uvuvi wamepata anguko la bilioni 12.5 ikilinganishwa na mwaka jana kwa kipindi kama hiki Je, sababu ni hiyo Corona kweli au kuna sababu nyingine mnaenda kufuatilia na ndio maana Mwenyekiti wa Kamati hapa akasema ile monitoring and evaluation inayofanya na Wizara ya fedha inausahihi gani, katika kuhakikisha kwamba inakwenda kubaini chanzo cha matatizo kinachosababisha kodi yetu kushuka.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la pili ambalo ni Bandari bubu, tuna bandari bubu 693 hizi bandari bubu zote zinatumika kuingiza shehena ya mizigo zinatumika kuingiza shehena za mizigo bila kuhakikiwa, bila kukaguliwa ubora na kama kama hazihakikiwi wala kukaguliwa ubora tunategeema kwamba watu wanaingiza mizigo hiyo bila kulipa kodi, watu wanaingiza bidhaa fake na bandia na kama wanaingiza bidhaa feki na bandia usalama wa viwanda vyetu uko wapi, lazima viwanda vyetu vitakufa ni lazima ajira zetu zitakufa, zitapotea sasa hili jambo linashughulikiwaje.

Mheshimiwa Spika, mbona hizi bandari bubu zimekuwa muda mrefu sana na zinaleta madhara makubwa sana kwenye Taifa letu kodi zinapotea. Bandari bubu kila leo zinaripotiwa. Bunge lako hili lingetarajia leo kuambiwa ya kwamba;

(i) Bandari bubu zote zimerasimishwa na vimekuwa bandari rasmi.

(ii) Tungetarajia bandari bubu zote zimepigwa pini hazipo tena lakini kuendelea kuwa na Bandari bubu ambazo zinahatarisha uchumi wetu wa Taifa hili tatizo ni nini na kwenyewe mtasema tatizo ni Corona?

(iii) Kushindwa kufunga Bandari bubu tatizo ni Corona kushindwa kurasimisha hizi bandari tatizo ni Corona? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo jingine la nne ambalo shehena za nguo zinapoingia hapa nchini zinapimwa kwa kutumia urefu tunakokotoa kodi kwa kutumia urefu mfumo huu wa kukokotoa kodi kwa kutumia urefu kwanza, hauwezi kuhakiki inabidi ukubaliane na kile kilichoandikwa na yule aliyeingiza mzigo. Sasa kama ndio tunatoza kodi kwa kutumia urefu uwezekano ni mkubwa sana wa kufanya under declaration kwa wale watu ambao wanaingiza mizigo mizigo hiyo ya nguo hapa nchini. Na wanapofanya under declaration maana yake ni nini, maana yake tutakosa kodi kwa sababu hatuwezi kupata kodi sahihi katika eneo sahihi.

Mheshimiwa Spika, na vile vile maana yake watakapoingiza nguo hapa viwanda vyetu vya nguo haviwezi ku-survivor viwanda vyetu vya nguo vitakufa Serikali imekosa mapato, ajira za watanzania zimeuwawa, lakini pia hata mapato ya Serikali na yenyewe hayawezi kupatikana na ajira zenyewe zitaendele kufungwa. Na hili jambo limelalamikiwa muda mrefu kwanini halishughulikiwi na kwenyewe tutasema tumeshindwa kukusanya mapato kwasababu ya Corona. (Makofi)

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, Taarifa!

SPIKA:Taarifa, endelea.

T A A R I F A

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimwa Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji ndugu yangu kwamba anachokisema kuhusu sababu zinazopelekea kuanguka kwa makusanyo tuhoji kama ni Corona tu ama kuna lingine kwa sababu mwaka jana mpaka mwisho wa mwaka Tanzania ndio nchi pekee ambayo ilikuwa ina uchumi chanya kati ya nchi zote nane zinazoizunguka, kwa hiyo, lazima kipo kitu kingine zaidi ya Corona, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Unaipokea hiyo taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ninaipokea vizuri kabisa, na niseme katika hili suala hili ninalolizungumzia hili la shehena za mizigo kwamba tunaweza tu kupima hizi shehena kwanini zisipimwe kwa uzito ambapo hakuna namna yeyote ile ya kukwepa sasa huwezi ukachukua zile kanga ukaanza kupima zile mita kujiridhisha matokeo yake tunaibiwa sana, tunapigwa sana kwenye eneo hili? Marekebisho haya kwanini hayafanyiki? Kwanini Wizara ya Fedha haibadilishi utaratibu huu kwanini TRA hawabadilishi utaratibu huu.

Mheshimiwa Spika, marekebisho haya kwanini hayafanyiki? Kwanini Wizara ya Fedha haibadilishi utaratibu huu, kwanini TRA hawabadilishi utaratibu huu?

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni baadhi ya taasisi zetu zinazokusanya mapato kuna mashirika ambayo yanakusanya mapato mengi sana sasa hivi, kwa mfano, wanapokusanya mapato wanapata mpaka mapato ya ziada mapato ya ziada haya maana yake nini? Mapato ya ziada ni kwamba umefanya matumizi yako yote lakini ukabakiwa na fedha hayo ndiyo mapato ya ziada ninayoyazungumza, baadhi ya taasisi zinakusanya fedha nyingi sana. Kwa mfano, TASAC katika kipindi cha mwaka 2017/2018 mpaka 2019/2020 walikusanya mapato ya ziada zaidi ya bilioni 119.48 lakini kilichoenda Serikalini ni bilioni 50.48, bilioni 69 zilienda wapi? TPA na wenyewe hivyo hivyo wlaikusanya mapato ya ziada bilioni 36, sasa haya ni mapato ya ziada kwamba matumizi yote umeshafanya, kila kitu ulichokipanga kwenye mwaka huo, hizi fedha ambazo hazikuwasilishwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali zilienda wapi na kwa nini Wizara ya Fedha inaruhusu haya mambo kutokea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina anasimamiaje hili eneo katika Taifa ambalo lina changamoto nyingi, tuna changamoto kubwa za maji, tuna changamoto kubwa za elimu, changamoto za afya madawa hamna fedha zinakusanywa zinaenda wapi, kwa nini haizendi kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali ziende kupangiwa matumizi Watanzania wakanufaika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ni tathmini ya matumizi ya OC, hivi tunapo bajeti kila mwaka matumizi ya OC siku zote yamekuwa kwa mwendo wa ukomo wa bajeti, mwendo wa ukomo wa bajeti wanazungumzia tu ukomo wa bajeti, kwamba mwaka huu bajeti yako imeongezeka kwa asilimia Tano imepungua kwa asilimia ngapi. Lakini huu mwenendo tutaenda nao mpaka lini? Kwa nini OC zisitolewe kwa umuhimu wa mahitaji ya kila Wizara? Matokeo yake katika hili eneo tumekuwa tukipoteza fedha nyingi sana, wizi mwingi unaandaliwa kwenye bajeti, pesa zinaandaliwa zinawekwa fungu mahsusi kwa ajili ya kuchotwa baadaye, mfano wake ndiyo hili sakata ambalo ameliibua Waziri Mkuu katika Wizara ya Fedha bilioni 1.6 zimepigwa pale na huu ni mkakati ambao umeandaliwa kuanzia kwenye bajeti hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa Majaliwa kwa kuliibua hili Sakata. Sakata hili mwanzo wake ni mipango ambayo imeandaliwa kutoka kwenye bajeti, fedha zimelundikwa kwenye kazi fulani, kazi ambayo haina umuhimu na mwisho wa siku ni lazima zile fedha zitumike kugawana kwa sababu njama zimefanyika kuanzia kwenye mpango wa bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Taifa kama hili tutaendelea kuwa na mipango ya namna hiyo mpaka lini? Kwa nini hizi OC zisipangwe kwa umuhimu wa matumizi, kwa Wizara inahitaji matumizi hayo kwa ajili ya jambo gani tunajiridhisha nacho kuliko ilivyo sasa hivi, kwamba tunazungumza tu ukomo wa bajeti basi fedha zinaidhinishwa. Tukienda kwa namna hiyo kwa Taifa changa lenye mapato madogo kama haya, tutapata matatizo makubwa sana. Wizara ya Fedha follow up yenu iko wapi? Wasimamizi wa mambo haya mko wapi katika kusimamia mambo haya mpaka yaendelee kutokea katika Taifa hili changa ambalo tunamahitaji makubwa ya kitaifa lakini fedha zinagawanwa tu?(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la mwisho ni kwamba hata taarifa zetu za mapato zinapowasilishwa kwa nini taarifa zinazowasilishwa za mapato kila zikiwasilishwa zinawasilishwa za TRA tu. Kwa nini taasisi zingine mapato yake haya wasilishwi kwa mwezi? Kwa nini taasisi zingine na Wizara zinazokusanya mapato yake kwa nini hatuletewi mkeka wote wa wahusika wote wanaokusanya mapato yetu, tukaletewa ili kama Taifa tukawa tunajua mwenendo wetu na safari yetu tunayoenda nayo ya ukusanyaji wa mapato na hasa tukijua kwamba hakuna matumizi bila mapato na nchi haiwezi kuendeshwa bila mapato? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo eneo la ukusanyaji wa mapato ni eneo muhimu sana ambalo Taifa linatakiwa kuwekeza na kuweka kipaumbele. Wizara ya Fedha mipango yenu katika kuweka mikakati ya kuhakikisha mapato yanakusanywa iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)