Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu. Nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu ya wataalam ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Kwa kuwa muda ni mchache, niombe nijikite katika maeneo kama mawili, matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, niiombe Wizara kuna mbuga mpya ambayo imetangazwa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambayo zamani ilikuwa ni pori la hifadhi. Niombe Wizara mbuga hii ni kubwa ina wanyama wengi, ina wanyama wakubwa na wazuri ambao inaweza kuwa ni kivutio kikubwa kwa watalii katika nchi.

Ombi langu kwa Wizara ni kwamba utangazaji wa mbuga hii bado haujakuwa mkubwa kiasi cha kuwafanya watalii wengi wafike kule. Ukiangalia bado tunatangaza mbuga ambazo ziko kaskazini wakati mbuga hii ni kubwa inaweza ikaongezea mapato makubwa Serikali na kufanya kwamba mambo yawe mazuri katika pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile naamini kabisa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambalo linajengwa kule nalo linaweza likawa ni moja ya kivutio kikubwa cha watalii. Kwa hivyo niombe sana Wizara iangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ambalo ningependa kuchangia na sisi Morogoro kule kuna eneo linaitwa Kisaki majimoto. Kuna maji ambayo yanachemka na mayai yanachemshwa. Niombe nacho ni kivutio ambayo Wizara kwa namna moja au nyingine watume wataalam wakaangalie jinsi gani wanaweza wakakitumia kivutio hicho kuongeza mapato kwenye Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo ningependa kuchangia katika Wizara hii, kati ya mwaka 2016 na mwaka 2021, kuna watu 46 wameuawa na mamba, kuna watu 15 katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro Vijijini wamepata vilema vya kudumu kutokana na ongezeko kubwa la mamba katika Mto Ruvu na Mto Mvuha ambao unapita katika Vijiji vya Tununguo, Mkulazi, Selembala pamoja na Kijiji cha Mvuha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu ni kwamba, idadi kubwa ambayo imetokea katika vifo kutokana na mamba imetokea katika Kata ya Selembala. Mwaka 2016 kumetokea vifo vya watu watatu; mwaka 2017 kumetokea vifo vya watu tisa; mwaka 2018 watu watano; mwaka 2019 watu sita; mwaka 2020 watu 14 na hadi Mei mwaka huu, watu tisa wameshakufa katika Kata ya Selembala. Kuna taharuki kubwa kwa watu na hasa ukitilia maanani watu wengi vijijini wanatumia maji ya mto wanashindwa kwenda kuchota kwa sababu wakienda wanakumbana na vifo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali, naamini kwamba mamba wamekuwa wengi na naamini kwamba ni wakati muafaka kwa sasa kwenda kuvuna mamba hao ili tuepushe vifo vya watu, lakini wakati huo huo tukapata fedha katika kuuza ngozi za mamba hao. Sambamba na hili vile vile nikuombe kupitia Wizara kwamba, tunaomba vifuta jasho kwa watu hawa ambao wamepoteza maisha kwa mujibu wa taratibu na sheria za maliasili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe vile vile kupitia Bunge lako Tukufu, kwa Wizara ya Maliasili na Utalii isaidie Halmashauri ya Morogoro Vijijini kwa vitendea kazi vya magari, lakini vile vile Askari wa Wanyamapori ili waweze kwenda kutusaidia ongezeko la wanyama ambao wamefanya uharibifu mkubwa kwenye Kata ya Kisaki, Kata ya Bwakila Chini, kata ya Serembala, Kata ya Mvuha. Nashukuru na naipongeza Wizara katika mwaka 2019 tumelipwa kifuta jasho kwa wakulima ambao waliharibiwa mazao na wengine ambao wamepoteza maisha wamepata kifuta jasho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado katika mwaka 2020 hatujapata kifuta jasho kwa wakulima ambao ekari 572 zimeathiriwa na ongezeko la wanyama hao waharibifu na wengine ambao wameshambulia watu. Ombi langu kwa Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)