Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Esther Edwin Maleko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii nyeti ya Maliasili na Utalii. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi kwa Waziri Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Mary Masanja kwa kazi nzuri wanayoifanya. Pia nitoe pongezi za dhati kwa timu nzima ya Wizara kwa sababu wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye kuchangia kwa sababu mud ani mfupi sana. Naomba nichangie kupitia utalii kwa sababu kwa kwetu sisi Tanzania ni nchi ya pili duniani kwa kuwa na vivutio vingi vya asili ikianza Brazil ambayo ni nchi ya kwanza duniani kuwa na vivutio vingi vya asili. Pamoja na hayo sekta hii ya utalii inachagia pato la 17% katika pato la Taifa. Si hivyo tu, inachangia ajira zisizopungua milioni 1.6, zile za moja kwa moja na ambazo siyo za moja kwa moja. Kwa hiyo, Wizara hii ni nyeti kwa sababu pia inaingiza asilimia 25 ya fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye kuchangia kwenye vivutio vyetu vya asili. Tuna kivutio kikubwa sana katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro. Kivutio hiki ni mlima Kilimanjaro, mlima huu kwa takriban watalii 45,000 mpaka 50,000 wanapanda kwa mwaka. Hata hivyo, kiikolojia mlima huu unaweza kupokea takriban watalii 300,000 kwa mwaka mmoja. Hivyo, unaona idadi ya watalii wanaopanda mlima huu ni 45,000 mpaka 50,000, ina maana kuna nafasi hapo ambayo hatufanyi vizuri. Nadhani hatutangazi vizuri mlima wetu au matangazo yako chini sana, kwa hiyo tujitahidi sana kutumia media. Leo media ni kitu kikubwa sana, watu wanashinda kwenye media, tukiweza kutumia tu Instagram kuutangaza mlima wetu, ambapo hatutumii gharama yoyote kubwa, tunaweza kuutangaza kwa kiasi kikubwa lakini pia hatuwezi kutumia gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tukachukua watu maarufu mfano Ronaldo, Messy na wengine wengi tukawafanya wao wakaja Tanzania, tusiwatoze hata senti tano, tukachukua wao wanapokuja Tanzania wakalala bure wakapata huduma zote bure, lakini yule mtu aka-post tu kwenye page yake yenye followers zaidi ya milioni 50 kwamba yuko Kilimanjaro, tayari tumetangaza mlima wetu na hatutumii gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, nimeona Wizara inafanya vizuri sana, wamemleta Mamadou kama balozi wa utalii, lakini si hivyo tu jana amekuja Zari the boss lady kama balozi wa utalii. Namshukuru Mungu nilipata nafasi ya kuzungumza naye na kubadilishana mawazo. Kama Mbunge ninayetoka Kilimanjaro nilimwalika aweze kuupanda Mlima Kilimanajro na amekubali, hivyo nawahamasisha Wabunge tuungane pamoja kwenda na Zari kuupanda Mlima Kilimanjaro kwa sababu sisi ni vivutio na sisi ni wawakilishi wa wananchi. Wananchi wakiona sisi tunaenda kupanda mlima Kilimanjaro, nao watahamasika na wataenda kupanda mlima. Kwa hiyo nawaomba Wabunge tuungane pamoja kupanda mlima Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, tunapaswa pia kuboresha rescue system katika mlima wetu wa Kilimanjaro. Watalii wanapokuja wakapata shida wakiwa kule mlimani wanapaswa kupata huduma sahihi. Ninaposema rescue system iboreshwe, naamini Wizara inajua namaanisha nini. Kwa hiyo ninaomba Wizara iboreshe rescue system iwape wale watoa huduma elimu bora zaidi ili iweze kuwahudumia watalii wanaopata shida wakiwa kule mlimani.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu tuwe na information center…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga.

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Sasa Mheshimiwa Ester hujatuambia kama na wewe utakuwa unapanda, kwa sababu wako Wabunge hapa ambao watatamani kujua kama na wewe unapanda ili waambatane na wewe.

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nimewahamasisha kwa sababu na mimi nitakuwa mmojawapo kwa sababu nimemhamasisha Zari apande Mlima Kilimanjaro, nitakuwa pamoja nao. Ahsante sana. (Makofi)