Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuweza kunipa nafasi kuwa mchangiaji katika bajeti hii ya leo. Natumia nafasi hii kuwapongeza sana watendaji wa Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kulihakikishia Taifa hili linapata maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu ningependa ujikite zaidi katika suala zima la uendeshaji sekta ya utalii. Duniani kote wataalam wa utalii wanapozungumza suala zima la utalii wanaainisha vitu vitano wanaita A5; kuna vitu vitano ambavyo ndivyo uti wa mgongo wa utalii. Kitu cha kwanza ni amani na utulivu tuliokuwa nao; Kitu cha pili ni vivutio duniani kote ambavyo vinapelekea watalii kwenda kutembelea; Kitu cha tatu miundombinu inayoweza kufikika katika sekta hiyo na kitu cha nne ni good service. Katika suala la good service Tanzania bado hatujakuwa more advance; na Kitu cha tano ni suala la promotion and marketing.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu mimi zaidi nitajikita katika suala zima la promotion and marketing. Tanzania takriban tupo nchi ya pili kwa kujaaliwa kuwa na vivutio vingi vya utalii duniani. Nchi ya kwanza Brazil, lakini cha kushangaza na cha kusikitisha sisi bado hatujajiwekeza zaidi katika kutangaza biashara hii. Ukiangalia duniani kote utalii siku zote unaletwa na matamasha, maonyesho pamoja na festivals, lakini sisi Tanzania mpaka hii leo tuna matamasha yasiyozidi manne wakati wenzetu Brazil wana matamasha yasiyoshuka 58. Ukija nchi kama Spain wana matamasha 48 na Uingereza wana matamasha 54.

Mheshimiwa Naibu Spika, tusitarajie sana kutangaza utalii wetu kwa kutegemea zaidi labda Tanzania Safari Channel ya TBC, inawezekana hata hiyo TBC hata Dubai watu hawawezi wakaisikia. Unapoangalia channel kama vile CNN pamoja na Sky News utaona utaona nchi za wenzetu kama vile Belarus, Bulgeria wameweka clip zao ndogo ndogo kuonyesha jinsi gani nchi zao zilivyokuwa na vivutio vingi vya utalii. Tuangalie mfano nchi ya Jirani hapa hii wanayoita Rwanda ni nchi ndogo sana, tumewazidi kwa vivutio vingi sana vya kitalii, lakini wao wanatumia bajeti kubwa katika kuwekeza katika sekta hii. Wameweza kuisaini Memorandum of Understanding na timu kama ya Arsenal, unapoangalia jezi za Arsenal mkononi hapa wameandika visiting Rwanda. Kwa hiyo wanatumia bajeti yao katika kuitangaza hii sekta nzima ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawashukuru sana ndugu zetu Simba, kama wenzetu wengi walivyokwisha kuelezea, wakati ambapo walipoenda kushiriki hizi ligi za klabu bingwa barani Afrika walijaribu sana kuitangaza Tanzania. Hata hivyo, lazima tukubali utalii wetu wa Afrika hususan Tanzania unategemea zaidi watalii kutoka Magharibi mwa Ulaya pamoja na nchi za Amerika na Nordic countries, sasa huko Simba bado hawajaweza kufika. Kwa hiyo, lazima tutafute njia nyingine za kuweza kuwekeza kama vile tunaweza kutangaza utalii wetu katika ligi kubwa kama vile ligi za Bundesliga Uingereza kule pamoja na nchi nyingine kama vile Ufaransa tukiwa tuna clip zetu za kuweza kututangaza tunaweza kufanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Tanzania tumebahatika kuwa na vyanzo vingi vya maji, lakini Watanzania bado hatujaelimishwa namna gani tunaweza kuvitumia vyanzo vya maji kama ni sehemu moja ya utalii. Katika vyanzo vya maji tuna uwezo wa kupata utalii wa water sport, hauhitaji gharama nyingi wala hauhitaji bajeti kubwa ukilinganisha na utalii wa aina nyingine. Tanzania tuna visiwa ambavyo havitoshuka 220, havishuki hapo, lakini duniani kote utalii ambao una thamani zaidi ni utalii wa kivisiwa, lakini ukitizama huku kwetu sisi visiwa hatujaweza kuviorodhesha kama ni sehemu ya kitalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wanatumia visiwa kama sehemu ya kitega uchumi, lakini sisi badala ya kujaliwa neema hiyo tutumie kama ni sehemu ya kitega uchumi tunaenda katika migogoro. Nimpe mfano Mheshimiwa Waziri; kuna kisiwa kimoja kinaitwa Latham Island ambacho kwa jina maarufu tunaita tunaita Fungu Mbaraka, watembezaji wa watalii wanapotoka kule Zanzibar kwenda kuangalia kile kisiwa pale wakiwa na wageni mara nyingi wanazuiliwa sana, kumekuwa na malalamiko ya aina yake kwa watu wa TMA (Tanzania Marine Authority) kwa kushirikiana na fisheries, wanakuwa wanawazuia kwa sababu wana leseni za kibiashara kutoka Zanzibar. Wanafanya kitendo kile hali ya kwamba wale watembeza wageni wanao wageni na wageni wanafahamu kile kinachozungumzwa, hii inatuharibia, sisi sote tunajenga nchi moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwa kuongezea kuna suala zima la miundombinu. Utalii ni sekta ambayo haiwezi ikajitegemea yenyewe lazima inategemea sekta nyingine. Mtalii anapotoka kwao haji hapa na embe, haji hapa na wali katika hotpot, wala haji hapa na gari ya kutembelea, anatarajia aje hivyo vitu avikute hapa. Cha kusikitisha sehemu nyingi ambazo zimepitiwa na sekta hizi za utalii wanafanya biashara…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)