Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hii hoja ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Naomba nianze kwa kuipongeza Wizara kwa kazi muhimu ya kuhifadhi rasilimali yetu ya Taifa wanayoifanya, lakini specifically nimshukuru pacha wangu Waziri Dkt. Ndumbaro na Naibu wake Mary Masanja kwa kitu kizuri nilichojifunza kutoka kwao. Tangu waingie katika Wizara hii wameanzisha mtindo mzuri wa kusikiliza kero za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa sababu Mheshimiwa Waziri alisikiliza kero ya wananchi na mwekezaji wa Green Miles akaja mpaka uwandani kushuhudia mwenyewe na matokeo yake yamewafariji wale wananchi. Sasa kilichobaki tu ni yule mwekezaji naye kwa sababu alimpa kibali cha kurudi katika lile eneo, akajipatanishe na wananchi maana yeye ndiye aliwakosea na ndiyo chanzo cha ule mgogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kulikuwa na changamoto kubwa ya eneo ambalo Wizara ya Maliasili katika awamu iliyopita ya Uongozi wa Awamu ya Tano, walilitwaa kabisa na kutaka kuligeuza kuwa pori la akiba katika Wilaya ya Longido. Eneo lile ni mahsusi la wafugaji wa Wilaya ya Longido, maeneo ya kuhemea wakati wa kiangazi la kupatia maji na majani, lakini Wizara ikaja na pendekezo bila kuwashirikisha wananchi la kutaka kugeuzwa kuwa pori la akiba. Ni eneo la Game Controlled Area ambalo limekuwepo tangu enzi ya ukoloni na wananchi waliendelea kufuga huku uwindaji ukiendelea bila bughudha, lakini baada ya Waziri kuingia na kupokea hicho kilio amewapa wananchi matumaini kwamba hilo jambo linahitaji kurejelewa na bahati nzuri au mbaya pia taarifa na kilio cha wananchi kimeshafika mpaka Ikulu, kimefika kwa Waziri Mkuu na kwake, lakini ile namna yake ya kusikiliza wananchi ni jambo la kupongeza sana. Nawapongeza sana Wizara ya Maliasili kwa hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nitoe ushauri sasa katika maeneo machache kulingana na hotuba waliyoitoa wenzetu ya bajeti na mambo ambayo yanastahili kufanyiwa marekebisho. Eneo la kwanza hizi kanuni za kifuta jasho na kifuta machozi zinahitaji kurejelewa, kiwango ni kidogo mno na muda wa kusubiri mpaka hata hicho kidogo kinachotolewa kitoke ni muda mrefu mpaka hata inakuwa haina maana tena. Naomba hilo suala lirejelewe na namwomba Waziri atakapokuja kutoa mrejesho hapa hebu atuambie kwamba ni utaratibu gani amejiwekea wa kuongeza kile kipato na kuharakisha ulipwaji wa wale watu ambao wameathiriwa na wanyamapori.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, Serikali iangalie uwezekano wa kupunguza tozo zinazotozwa Kampuni za utalii wa uwindaji. Hiyo tasnia imeshuka kabisa na ukiwasikiliza wawindaji wanasema ni kwa sababu ya tozo, VAT ilipokuwa introduced mwaka 2016, idadi ya watalii imeshuka kutoka 1,500 kwa mwaka mpaka wakafikia kwenye 500 tu kwa mwaka. Mbaya zaidi ulipoingizwa ule mtindo wa kuuza vitalu kwa njia ya mnada vitalu vingi vimekaa bila wawekezaji na mapato ya Serikali na ya wao wenyewe na ya jamii ambayo walikuwa wanaisaidia kupitia ule mfumo wa uwajibikaji kwa jamii pia yameshuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano katika taarifa ya wanaitwa TAHOA, Chama cha Wawindaji; wanasema kwamba katika minada mitatu ambayo imeshatangazwa tangu huo mfumo uanze na vitalu 60 vilivyowekwa mnadani ni 11 tu vimepata wawekezaji vile vingine vikabaki idle kwa sababu hakuna watu waliokuwa na interest navyo. Sasa naomba kuishauri Serikali kwamba wapange tu bei ambayo ni reasonable ili kila mtu anayetaka kitalu kwa sababu kina bei tayari iwekwe price tag kuondoa utata wowote wa rushwa na nini aweze kuingia na mapato yakapatikana badala ya kuvifanya vikose wawekezaji na vikose ulinzi na mazingira yetu yakazidi kuharibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wa tatu kwenye mfumo wa marejesho ya mapato kwenye WMA’s, wakati corona ilipoingilia Mataifa na pia nchi yetu ikaathirika, mapato yote yanayokusanywa kwenye vyanzo vya hifadhi yakawa yanapelekwa Hazina. Utaratibu wa kurudisha zile fedha zije zisaidie uendeshaji wa WMA, kuwapa vijiji mgao wao, ulivurugika kabisa na WMA nyingi karibu zishindwe ku-operate kwa sababu mfumo ulikuwa haupo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia Waziri atueleze leo kwa sababu najua kilio cha wenye Jumuiya za Hifadhi za Wanyamapori za Jamii kwamba walikuwa wamekwama kabisa katika uendeshaji. Sasa Wizara imeweka mkakati gani wa kuwasaidia, mapato yaweze kurejeshwa na Hazina waweze kujiendesha na wananchi waendelee kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu wa nne, ni kuimarisha mahusiano baina ya wananchi na maeneo yaliyohifadhiwa. Kwa huu mtindo sasa hivi ulioko wa kwamba TANAPA wakiona eneo ambalo limeiva wanataka tu walinyakue, hautusaidii, inatakiwa washirikishe na watambue uhifadhi jumuishi, uhifadhi wa mseto maana ndiyo itakayotusaidia katika karne hii ya ongezeko la watu na haja ya maeneo mbalimbali kwa matumizi mbalimbali ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)