Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyeiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Utalii. Kwa kuwa muda ni mfupi, nitaongelea jambo moja tu, suala la kumbukumbu za Vita vya Majimaji. Naona nilipoongea Vita vya Majimaji, au kule kwetu Kilwa Kaskazini wanavitambua kama Ngondo ya Machemache, naona Mheshimiwa Jenista Mhagama ameshituka kidogo pamoja na Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vita hivi vilianza tarehe 15 Julai, 1905 katika Kijiji cha Nandete Jimboni kwangu Kilwa Kaskazini, Tarafa ya Kipatimu. Ilihusisha; kama ilivyokuwa kule Songea, kulikuwa na Machifu 12, huku kwetu kulikuwa na viongozi wa koo tisa, ndio ambao waliongoza hivi vita. Naomba niwataje, alikuwepo kiongozi wa Kiroho aliyejulikana kwa jina la Kinjeketile Ngwale, alikuwepo ambaye alikuwa anaishi Kijiji kinaitwa Ngalambilienga, alikuwepo Jemadari wa vita hivyo, alikuwa anaitwa Sikwako Mbonde, alikuwa anaishi Kijiji cha Nandete.

Pia alikuwepo Ngulumbali wa Mandai, alikuwa anaishi Nandete; Lindimio Machela, Mabiga Nandete, Bibi Ntabilwa Naupunda ndiye ambaye alibeba ile dawa ya maji, Nandete na vile vile alikuwepo Mpeliadunduli Kipengele; alikuwepo Libobo Mpanyu Kipengele; alikuwepo Mataka Nkwela Mwiru; alikuwepo Kilambo Mpetamuba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa miaka mingi wenzetu wa kule Songea Jimboni kwa Mheshimiwa Waziri, wamekuwa wakiadhimisha miaka karibu takriban 114 kuhusu Uwepo wa vita hivi au kumbukumbu za vita hivi, lakini kwa upande wa Kilwa Kasakazini hili jambo limekuwa halifanyiki. Hata miundombinu ya utalii imejengwa kule Songea. Kuna kumbukumbu; National Museum ipo, lakini kwa upande wa Kilwa Kaskazini haipo. Kwa hiyo, hata kumbukumbu za hawa wazee maarufu ambao walikuwa na uthubutu wa kupambana na Wakoloni wa Kijerumani mpaka sasa haipo. Kwa maana hiyo, hii historia imekuwa ikififia na hatimaye kutoleta tija katika sekta ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, siyo tu vita vya majimaji peke yake, bali kulikuwa na mazingira ambayo yaliambatana na hivyo vita. Kulikuwa na mapango; Pango kubwa la Nang’oma ambalo ni kubwa Kusini mwa Jangwa la Sahara, Barani Afrika, lipo pia lile la Namaengo; lipo kaburi la mzungu ambaye alizikwa kutokana na vile vita vya majimaji. Kule tunaita lisikolian nungu, lipo katika Kijiji cha Kinywanyu, Kitongoji cha Mbongwe, Kata ya Chumo. Pia lipo boma la Mjerumani mahali ambako Wajerumani waliweka makazi yao kwa ajili ya kudumisha utawala katika eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, hivi vivutio ni vivutio vizuri vya utalii, naomba tuvisimamie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri, hivi vivutio vya utalii ni vizuri. Naomba tuvisimamie, tuvitangaze, lakini tuviwekee miundombinu bora na kuhakikisha kwamba kunakuwa na makumbusho kwa ajili ya kudumisha kumbukumbu za vita vya majimaji na kuvutia watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)