Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nami nakupongeza kwa kupewa nafasi kubwa kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai siku ya leo. Pia nawashukuru wananchi wa Urambo wakiwemo ndugu zangu kwa ushirikiano wanaonipa. Nachukua nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Urambo kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na viongozi wote ndani ya Wizara yao. Hongereni kwa kazi kubwa mnayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii pia kwa niaba ya wananchi wa Urambo kuishukuru sana Serikali kwa kutupa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugala. Mwaka 2019 lilipitishwa azimio, kwa hiyo, sasa tuna Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugala. Hata hivyo, Serikali inapokuja na mambo mazuri kama haya ya Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugala, kuna umuhimu wa kuwapa elimu wananchi wanaohusika. Sasa tunajua wananchi wangapi wanajua faida ya kuwa na Hifadhi ya Msitu? Watanufaika vipi? Wataishije? Kwa hiyo, kuna umuhimu wa Serikali inapochukua hatua kubwa kama hizi, kuwaelimisha wananchi wajue wataishije? Watanufaika nini? Kwa sababu, lengo kubwa ni kujenga mahusiano kati ya Serikali na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka pia niwaambie kwamba Kata nne za Nsenda, Ukondamoyo, Ugala na Kasisi, maeneo yao yalipunguzwa na mwaka 2014 kulitokea mgogoro. Wao wanaamini kwamba jiwe lao halali ni Namba 23 ambalo lilikuwepo kabla maliasili na utalii haijaweka mipaka yake. Kwa hiyo, wakawa wamerudishwa nyuma kilomita zipatazo 10. Kwa hiyo, likawapunguzia nafasi ya kulima, kufuga mifugo yao yaani ng’ombe na kadhalika na pia kuweka mizinga yao ya asali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa eneo kama hili ambalo lilisababisha askari kuchoma nyumba zao na lililetwa mpaka humu Bungeni, kwa kupitia Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakati huo alikuwa Mheshimiwa Pinda na wakatoa pole kwa wananchi. Kwa hiyo, tayari kulikuwa na msuguano ambapo Serikali ingetafuta nafasi ya kuweka mahusiano mapya ili kuwe na ujirani mwema. Badala yake sasa hivi imekuja na hifadhi kabla haijaweka mahusiano mazuri na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na shukurani kwa Serikali kutupa hifadhi, bado kuna haja ya kwenda kuwapa wananchi elimu, wataishije baada ya kuwa na Hifadhi ya Taifa? Maeneo yao yaliyopungua sasa, kwa sababu wamerudishwa nyuma kilomita 10, watapata wapi eneo lingine? Kwa hiyo, naomba niwasilishe maombi yao wananchi wa Urambo hasa katika Kata hizo nne ambazo zimeathirika kwa njia mojawapo ingawa wamepata faida ya kupata hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, tulikuwa tunaomba wapewe elimu ya faida ya TANAPA na kadhalika na wataishije? La pili, naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge waliomo humu, walioiomba Serikali kufikiria upya kwa kuwaongezea maeneo ya kulima, kufuga na kuweka mizinga yao ya nyuki. Kwa hiyo, tunaomba kwa heshima na taadhima tupatiwe angalau kilomita tano kwa sababu, walirudishwa nyuma kilomita 10. Angalau tupate kilomita tano wananchi waweze kulima, kufuga na kuweka mizinga yao ya asali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, tunaomba baada ya kuongezewa eneo, tupate mashine za kuchuja asali, nasi tupeleke Urambo asali, kwa sababu ndiyo maendeleo yenyewe hayo. Watu walikuja pale wanaita Follow The Honey kutoka America, lakini sasa tena ndio mmetufukuza, haturuhusiwi kuweka mizinga ndani ya eneo. Kwa hiyo, tunaomba kabisa kwamba tupewe mashine za kuchuja asali lakini wakati huo huo tuweze kuruhusiwa kuweka mizinga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali imetupa ruhusa tarehe 6 mwezi huu wa Juni mpaka tarehe 6 mwezi wa Julai kuvuna asali, lakini baada ya hapo mizinga tunaweka wapi? Kwa hiyo, tunaomba tuongezewe eneo kama nilivyosema tulime, tufuge na tuweke mizinga yetu ya asali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala siyo la leo. Mheshimiwa Naibu Waziri na aliyekuwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Hasunga namwona pale. Alikuja, wazee wakamwonyesha mawe yao ya asili, alikuja Mheshimiwa Ramo akiwa Naibu Waziri, alikuja Mheshimiwa Naibu Waziri Angelina Mabula na yeye akawaweka wataalam, anajua. Kwa hiyo, suala hili siyo jipya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia alikuja Mheshimiwa Kigwangala lakini bahati mbaya siku alikuja, mvua ikanyesha akashindwa kuingia. Maana yake nini? Nataka kusema hili tatizo au mgogoro huu wa mipaka siyo wa leo, ni wa siku nyingi na tulileta hapa Bungeni kwa barua hii hapa, kwamba Serikali katika ile Tume iliyokuwa inapitia migogoro, nasi tulileta. Kwa hiyo, nashukuru Mheshimiwa Waziri wa Ardhi naye anasikiliza, naamini kabisa katika hili atatusaidia kwa kushirikiana na Waziri mhusika wa sasa ili tupate maeneo yale kama yalivyokuwa yamekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa heshima na taadhima kabisa, pamoja na kuipongeza Serikali kutupa hifadhi, bado tunahitaji waje wajenge mahusiano, watuongezee maeneo kama tulivyoomba, Serikali yetu ni Sikivu, inawapenda wananchi wake, tuongezewe eneo la kulima na kufuga na kuweka mizinga yetu. Tuna asali nyingi sana, karibuni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtajie Mheshimiwa Waziri maeneo ambayo atayakuta kule ambayo kweli yana changamoto katika hizo Kata nne. Atakuta Izengabatogilwe, Lunyeta, Mwagimagi, Msumbiji, Utewe, Mkola, Utenge, Mwengemoto na Holongo; katika hizo Kata nne ambazo nimezitaja hapo awali. Kwa hiyo, kwa heshima na taadhima, pamoja na kuunga mkono, nawapenda hawa Mawaziri kwa sababu ni wasikivu. Mheshimiwa Waziri mhusika, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, wote ni wahusika. Hayo matatu naomba nirudie kwa mara ya mwisho kabla kengele haijalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujenga mahusiano kwa kutupa elimu; pili, kuomba eneo, tuongezewe angalau kilomita tano, Serikali yetu ni nzuri; na tatu, tunaomba mashine ili mizinga tutakayoweka, tuweze kuchuja asali yetu, Urambo tupeleke asali duniani. Waamerika wanasema nzuri sana kwa ajili ya chocolate, kwa sababu ya kwetu ni nyeusi safii. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)