Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nakupongeza sana kwa wadhifa huo. Pia nawapongeza sana Wizara ya Maliasili na Utalii; Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote kwa kazi nzuri mliyoifanya hasa kudhibiti ujangili kwa asilimia 90. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza pia kwa kutuhakikishia kwamba mnaenda kuanzisha vituo vya askari wa kudumu katika maeneo hatarishi ya wanyama wakali na waharibu kwa maana ya tembo. Sasa hili nendeni mkalitekeleze, nasi tunawapongeza sana kwa kazi hiyo nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ni suala la wafugaji walioshinda kesi Mahakamani, lakini Serikali imekaidi kurudisha mifugo yao. La kwanza, katika Pori la Maswa na WMA ya Makao, ng’ombe walikamatwa 1,739, walipoenda kwenye Mahakama Kuu Shinyanga wafugaji hawa walishinda, wakaenda kwenye Mahakama ya Rufaa Tabora, wakashinda. Ng’ombe jumla 1,739 mpaka leo hawajarejeshwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama ya Kanda Dodoma kwa kesi ya jinai ya 136 ya mwaka 2017 ng’ombe 466 zilikamatwa katika Pori la Akiba la Swagaswaga ambapo ni ng’ombe 113 tu walirudishwa, lakini wengine wote katika 400 na kitu hawajarudishwa mpaka sasa. Pori la Akiba la Moyowosi ambapo ng’ombe 216 walikamatwa mpaka leo hawajarudishwa na Serikali. Katika ile hesabu ya ng’ombe 6,000 hii ni mifano tu ya wafugaji wetu ambao wameshashinda kesi Mahakamani, lakini Serikali haijarudisha mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza wakati nachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais hapa kwa uchungu mkubwa nikijua kwamba Serikali italichukulia hili maanani. Nimesoma hotuba ya Waziri, hakuna hata mstari mmoja alipozungumzia juu ya mifugo hii. Wewe unajua kwamba haki inatolewa na chombo gani? Nanukuu kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara 107 (a) (1) Mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji wa haki katika Jamhuri ya Muungano itakuwa ni Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama imeshaamua ng’ombe warudishwe, wahusika hawajarudisha mpaka leo hii hawa ng’ombe wa wafugaji. Waziri wa Maliasili na Utalii hajarudisha mifugo ya wananchi, Waziri wa Katiba na Sheria amekataa kurudisha mifugo ya wananchi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali amekataa kurudisha mifugo ya wananchi, Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali DPP amekataa kurudisha mifugo ya wananchi. Hawa wote wamevunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo wao wameapa kuitetea na kuilinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Mawaziri wote wanne na hawa watendaji wengine wamevunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo wao wameahidi kuilinda. Kwanza ni wasimamizi wa haki na sheria, inakuwa vipi waivunje sheria hiyo? Kama sheria imevunjwa, kama Katiba ya Jamhuri imevunjwa, Bunge hili ambalo limeapa kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Katiba imevunjwa…

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, naomba tupokee taarifa.

T A A R I F A

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa kwamba mchangiaji wakati ule alikuwa Waziri wa Mifugo na hizi kesi zimetokea akiwa Waziri. Tunataka kujua ni kwa nini yeye hakurudisha? (Kicheko)

MWENYEKITI: Hilo ni swali au taarifa! Mheshimiwa Mpina endelea.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, acha niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Mawaziri wamevunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano Ibara ya 107 (a). Kama Katiba ya Jamhuri ya Muungano imevunjwa na Mawaziri hawa, Bunge lako lichukue nafasi. Hatuwezi kukubali wananchi wakadhulumiwa kwa namna hiyo inayoendelea sasa. Ng’ombe 6,000 wamekamatwa, wananchi hawa wameshinda kesi Mahakamani halafu mifugo hii inaendelea kushikiliwa…

MHE. MUSUKUMA J. KASHEKU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Musukuma.

T A A R I F A

MHE. MUSUKUMA J. KASHEKU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa taarifa tu mzungumzaji kwamba maneno anayoyazungumza yananikumbusha Bunge lililopita wakati tukichangia kuhusu suala la uvuvi, lakini alishindwa kutusaidia kwa sababu alikuwa anatekeleza sheria. Sasa nadhani angejikita kushauri kama Bunge tubadilishe sheria kuliko kumu-attack Mheshimiwa Waziri. Akiendelea hivi, kuna watu tutalia humu, tumechomewa mitego, Mheshimiwa Mpina uliapiza humu.(Kicheko/Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mpina, unaipokea taarifa?

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna taarifa pale ya kupokea, itanipotezea muda. (Kicheko)

MWENYEKITI: Haya endelea.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja nitaomba adjourning motion nizungumze kidogo haya maeneo yanayochomekwa haya kwa sababu muda wote niliisimamia hiyo Sheria ya Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wananchi hawa wameshinda kesi Mahakamani, Mahakama Kuu zimeamua mifugo irudishwe; Mahakama ya Rufaa imeamua mifugo irudishwe; nani tena mtoa haki mwingine ambaye anasubiriwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Bunge lako liamue leo, azma ya mifugo ya wananchi hawa irudishwe kwa wananchi ambao wamepata mateso makubwa sana kwa muda mrefu na Serikali imeshindwa kurudisha mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilizungumze hapa ni suala la utanuzi wa maeneo. Maeneo ya malisho yaliyo mengi mipaka ya hifadhi ilitanuliwa, ikachukua maeneo mengi sana ya malisho. Baada ya kutanuliwa, kwa mfano, ukienda kule Nsumba kule Ushetu; msitu ule wa Nsumba umeingizwa GN juu ya GN. Waziri wa Maliasili akatangaza GN wakati ule ni msitu wa wananchi wa eneo hilo na ulikuwa ukitumika kulishia mifugo. Huo ni mfano tu mmojawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tujue katika nchi yetu, tumeanzisha WMA zaidi ya 22, nadhani kwenye hotuba ya Waziri inaonyesha ni 38; na hiyo 38 imechukua hekta 3,062,300. Vile vile kuna shida kubwa sana katika hayo maeneo ya WMA ambapo vijiji 37 wameomba kujitoa, lakini hawasikilizwi. Bado kuna vijiji vingine walitoa eneo la WMA la zaidi ya asilimia 78 ya maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Vilima Vitatu kule Manyara, ukaenda Ipona kwenye Pori la Akiba la Mara, asilimia 75 imechukuliwa. Wananchi wale wanaomba muda wote kwamba maeneo yao yaweze kuangaliwa kufanyiwa tathmini, lakini hawaendi. Waziri wa Maliasili kuna shida gani kwenda kuwasikiliza wananchi wenye malalamiko haya? Waziri wa Ardhi ambaye ndio refa wa ardhi nchini, unafanya nini kwenda kumaliza migogoro ya wananchi hawa tukaimaliza kabisa, mpaka mwishowe tuwe na malalamiko ya kudumu ya muda wote huo mrefu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wamechukua maeneo, kama ninavyozungumza hekta 3,062,300, yote haya tujue kabla ya WMA yalikuwa ni maeneo ya kulishia mifugo. Kwa nini leo hii maeneo haya wananchi wanaomba kwenda kufanya tathmini yasiende kufanyiwa tathmini ili sehemu nyingine ya ardhi ambayo inaweza ikapatikana wafugaji hawa wapewe? Sasa wananchi hekta zao 3,062,300 zimechukuliwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)